Friday, October 9, 2009

Jalada kesi ya Jeetu kuhamishiwa Mahakama Kuu

MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kisutu imetoa uamuzi kwa kukubali maombi ya kupeleka Mahakama Kuu jalada la kesi ya kujichotea fedha za Benki Kuu ya Tanzania (BoT) inayowakabili mfanyabiashara maarufu Jeetu Patel na wenzake.

Mahakama hiyo chini ya Hakimu John Mgeta, jana ilikubali maombi kwa kukubali ombi la akina Jeetu la kutaka kesi zao zilizoko mahakamani hapo kusimama na kuruhusiwa kuhamisha jalada kwenda Mahakama Kuu kwa ajili ya usikilizwaji wa kesi ya kikatiba waliyoifungua mwaka huu.

Baada ya Hakimu Mgeta kukubali ombi lao ingawa upande wa mashtaka ulipinga, hakusema kama kesi hiyo imefutwa au itaendelea kutajwa, kama ilivyoelezwa katika uamuzi wa hakimu mwingine katika kesi kama hiyo inayowakabili washtakiwa hao mahakamani hapo ambapo waliruhusiwa pia kuhamishia jalada Mahakama Kuu kesi ya Kisutu ikiendelea kutajwa.

Washtakiwa katika maombi yao walidai kuwa tamko la Mwenyekiti Mtendaji wa IPP, Reginald Mengi Aprili 23 mwaka huu, akiwataja kuwa mafisadi papa, limeifanya jamii iwaone wana hatia.

Walidai wamenyimwa haki yao ya kuonekana kuwa hawana hatia mpaka pale upande wa mashtaka utakapothibitisha bila shaka.

Aidha, upande huo uliomba jalada la kesi kupelekwa Mahakama Kuu kwa ajili ya kuamua kama tamko la Mengi halikukiuka haki za washtakiwa na baada ya serikali kutoa tamko kwamba Mengi ameingilia uhuru wa mahakama, je ilikuwa sahihi kuendelea na kesi hizo badala ya kuzifuta na kumshtaki Mengi kwa kuidharau mahakama?

Upande wa mashtaka ulipinga maombi hayo ukidai kuwa maneno hayo waliyodai ni ya barabarani na hayana uhusiano wowote na kesi iliyoko mahakamani na kuiomba mahakama kuyatupilia mbali.

Jeetu ambaye jina lake kamili ni Jayantkumar Chandubhai Patel, katika kesi hiyo anashtakiwa pamoja na Devendra Patel, Amit Nandy na Ketan Chohan na wanadaiwa kughushi na kujipatia ingizo kutoka BoT la Sh bilioni 3.9 na wanadaiwa kujifanya kuhamishiwa deni na kampuni iliyoko Japan.

Washtakiwa hao wanadaiwa kwa kutumia Kampuni ya Bina Resorts walijifanya kuhamishiwa deni hilo kutoka C.Iton & Company Limited na kuitaka BoT kuwaingizia fedha hizo na benki hiyo ilifanya hivyo.

No comments: