Tuesday, October 20, 2009

Shahidi kesi ya Liyumba mgonjwa

WATU wengi leo walitarajia kuanza kufahamu undani wa kesi inayomkabili aliyekuwa Mkurugenzi wa Utumishi na Utawala Benki Kuu ya Tanzania (BoT), Amatus Liyumba, lakini sasa itabidi wasubiri hadi Oktoba 22.

Upande wa mashitaka ulitarajiwa kuanza kutoa ushahidi katika Mahakama ya Hakimu Mkazi, Kisutu, Dar es Salaam, haukufanya hivyo kwa madai kuwa shahidi wa kwanza anaumwa.

Mahakama hiyo imefahamishwa kuwa, shahidi huyo alianza kuumwa tumbo ghafla leo asubuhi wakati anajiandaa kwenda mahakamani.

Wakili upande wa Serikali, Juma Ramadhan, amedai mahakamani kuwa, shahidi (hakumtaja jina) aliyestahili kuanza kutoa ushahidi wake aliumwa tumbo ghafla na akaomba kesi iahirishwe kwa siku mbili ili apate nafuu.

“Kesi hii ilikuja kwa ajili ya kuanza kutolewa ushahidi lakini shahidi wetu ameugua tumbo ghafla asubuhi hii wakati akijiandaa kuja kutoa ushahidi wake mahakamani hivyo tunaomba mahakama ipange tarehe nyingine ili shahidi wetu aweze kuja kuanza kutoa ushahidi wake”.

Wakili upande wa Utetezi, Majura Magafu, amesema upande wa mashitaka katika kesi hiyo unapaswa kuhakikisha kwamba unaanza kutoa ushahidi katika tarehe itakayopangwa kwa kuwa mteja wao anaendelea kusota rumande.

Magafu kama shahidi huyo ataendelea kuumwa, upande wa mashitaka utafute shahidi mwingine atakayeweza kutoa ushahidi wake mahakamani hapo.

Hakimu, Edson Mkasimogwa, ameuagiza upande wa mashitaka uhakikishe kwamba unakuwa na shahidi mahakamani Oktoba 22 ili kesi hiyo ianze kusikilizwa. Upande wa mashitaka una mashadihi 10 wakiwemo maprofesa watatu.

Mashahidi hao ni Mwanasheria wa BoT, Bosco Kimela, ambaye pia anakabiliwa na mashitaka ya kuidhinisha malipo kwa kampuni zilizochota fedha Katika Akaunti ya Malipo ya Nje iliyokuwa BOT, na kesi nyingine ya kuhujumu uchumi.

Maprofesa wanaotarajiwa kutoa ushahidi katika kesi hiyo ni Profesa Letice Rutashobya, Profesa Bruno Ndunguru, na Profesa Joseph Semboja.

Mashahidi wengine ni Michael Shirima, Seif Mohamed, Elisa Msangya, Jafar Uledi, Julius Ngelo na Yusto Tongola. Mei 28 mwaka huu, Liyumba alipandishwa kizimbani kujibu mashitaka mawili likiwemo kuhusika katika ujenzi wa ghorofa pacha za makao makuu ya BoT, akidaiwa kupandisha gharama.

Ameshitakiwa akidaiwa kutumia vibaya madaraka aliyokuwanayo na kuisababishia Serikali hasara ya zaidi ya Sh bilioni 221.

No comments: