Monday, October 19, 2009

JK ateua makatibu wakuu wanne wapya, ahamisha wawili, ateua katibu wa rais mpya

RAIS Jakaya Mrisho Kikwete amefanya mabadiliko katika safu ya maofisa waandamizi wa Serikali kwa kuteua Makatibu Wakuu wa Wizara wanne wapya, kuhamisha wengine wawili, na kuteua Katibu wa Rais mpya.

Taarifa iliyotolewa leo, Jumatatu, Oktoba 19, 2009, Ikulu, mjini Dar es Salaam na Katibu Mkuu Kiongozi, Bwana Philemon Luhanjo, imesema kuwa Mhe. Rais Kikwete amefanya mabadiliko hayo kufuatia kustaafu kwa baadhi ya Makatibu Wakuu wa Wizara.

Aidha, taarifa inasema kuwa mabadiliko hayo yanaanza leo, Oktoba 19, 2009.

Taarifa hiyo imesema kuwa Mhe. Rais Kikwete amemteua Bwana David Kitundu Jairo kuwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini. Kabla ya uteuzi wake, Bwana Jairo alikuwa Katibu wa Rais.

Bwana Jairo anachukua nafasi ya Bwana Arthur Mwakapungi ambaye amestaafu.

Katika taarifa yake, Bwana Luhanjo amesema kuwa pia Mhe. Rais Kikwete amemteua Bwana Sazi Salula kuwa Katibu Mkuu wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa. Kabla ya uteuzi wake, Bwana Salula alikuwa Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali.

Taarifa hiyo pia imesema kuwa Mhe. Rais Kikwete amemteua Bwana Mbarak M. Abdulwakil aliyekuwa Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Makamu wa Rais, kuwa Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi.

Bwana Abdulwakil anachukua nafasi ya Bwana Patrick Rutabanzibwa ambaye anahamishiwa Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kama Katibu Mkuu. Ndugu Rutabanzibwa anachukua nafasi iliyoachwa na Bi. Salome Sijaona ambaye amestaafu.

Kwa mujibu wa taarifa hiyo, Mhe. Rais Kikwete pia amemteua Bwana Christopher N. Sayi kuwa Katibu Mkuu wa Wizata ya Maji na Umwagiliaji.

Kabla ya uteuzi wake, Bwana Sayi alikuwa Naibu Katibu Mkuu katika Wizara hiyo hiyo, na anachukua nafasi ya Bwana Wilson Mukama ambaye ameanza likizo ya kustaafu kwa mujibu wa sheria.

Bwana Luhanjo amesema katika taarifa yake kuwa vile vile Mhe. Rais Kikwete amemteua Bwana Sethi Kamuhanda kuwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Utamaduni na Michezo.

Kabla ya uteuzi wake, Bwana Kamuhanda alikuwa Naibu Katibu Mkuu, Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa.

Anachukua nafasi Dkt. Florence Turuka ambaye anahamishiwa Wizara ya Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia kama Katibu Mkuu. Bw. Turuka anachukua nafasi ya Dkt. Naomi Katunzi, ambaye anamaliza mkataba wake wa utumishi wa Serikali mwezi ujao, Novemba, 2009.

Taarifa ya Katibu Mkuu Kiongozi pia inasema kuwa Rais Kikwete amemteua Prosper Mbena kuwa Katibu wa Rais. Kabla ya uteuzi wake, Bwana Mbena alikuwa Msaidizi wa Katibu wa Baraza la Mawaziri, na anachukua nafasi ya Bwana Jairo.

Imetolewa na:

Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,
Ikulu,
DAR ES SALAAM.

19 Oktoba, 2009

No comments: