Thursday, May 19, 2011

Mbunge apigwa mawe, Chadema yadaiwa kuhusika

MSAFARA wa Mbunge wa Tarime mkoani Mara, Nyambari Nyangwine na Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya Tarime, Amos Sagara, umeshambuliwa kwa mawe na wananchi wa Nyamongo na baadhi ya walinzi wa viongozi hao kujeruhiwa.

Wakati hali ikiwa hivyo, Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani, Balozi Hamis Kagasheki, amesema fujo hizo zilizotokana na mauaji ya wananchi wanne waliovamia mgodi hivi karibuni, zinachochewa kisiasa.

Akisimulia vurugu hizo, Nyangwine alisema yeye na Sagara, walikwenda kuwafariji wananchi wa Nyamongo ambao ndugu zao waliuawa na Polisi wakidaiwa kutaka kuvamia mgodi wa North Mara mwanzoni mwa wiki hii.

Kwa mujibu wa Nyangwine, walipanga kufanya mkutano na wananchi katika eneo la kituo cha mabasi cha Kewanja, Nyamongo.

"Tulifika na kukaa, lakini kabla hatujaanza kuhutubia, lilijitokeza kundi la vijana zaidi ya 100 na kudai kuwa wanachama tilioongozana nao wakiwa na sare za CCM wavue sare hizo na kuondoka maeneo hayo nikiwamo mimi na Mwenyekiti wa Halmashauri.

“Walitushambulia kwa mawe na walinzi wangu sita wakiongozwa na Godfrey Francis na Sutwa, walipambana nao nikafanikiwa kuingia ndani ya gari na kuondoka huku wakiturushia mawe na kujeruhi baadhi ya walinzi hao na kuharibu magari yetu," alisema Nyangwine.

Magari yaliyoharibiwa kwa kuvunjwa vioo katika vurugu hizo ni pamoja na gari la Idara ya Elimu aina ya Toyota Land Cruiser namba STK 8411, Toyota RAV4 namba T 299 ASW na Toyota Prado, namba T 239 DNW.

Nyangwine alisema, walishambuliwa saa tano asubuhi Kewanja na kuwataka wananchi wa Nyamongo wasikubali kutumiwa na baadhi ya wanasiasa wa vyama vya upinzani kuvamia mgodi huo na kushambulia viongozi wa umma kwa mawe.

“Suluhu inapatikana kwa kukaa pamoja wala si kurushiana mawe, tumekuja kwa nia njema kukufarijini, lakini baadhi ya wanasiasa wamegeuza maafa haya mtaji wa kupandikiza, jambo ambalo ni hatari kwa jamii ya Tanzania, nakemea na kulaani kitendo hiki," alisema Nyangwine

Alisema, katika mkutano huo, alitaka kuzungumzia mauaji ya mara kwa mara ya wananchi wa vijiji vinavyozunguka mgodi huo na sababu za kuvamiwa mgodi huo na baada ya hapo, walikuwa waungane kwenda kumpokea Katibu Mkuu wa CCM, Wilson Mukama.

Moja ya sababu za kuvamia mgodi huo kwa mujibu wa madai ya Nyangwine, ni malalamiko ya wananchi wa maeneo hayo kutolipwa fidia za mali zao na maeneo yao yaliyochukuliwa na mgodi wakikosa eneo la wachimbaji wadogo.

Malalamiko mengine ni vijana kukosa ajira na vifaa vya kisasa kwa wachimbaji wadogo, hali inayochangia ugumu wa maisha katika maeneo yanayozunguka mgodi huo.

Alisema, Serikali itaunda Tume huru itakayoshirikisha Wananchi, viongozi wa vijiji, wa Serikali, wazee wa kimila na wamiliki wa mgodi huo.

Wakati Polisi wilayani hapa, ikisaka watuhumiwa wa uhalifu huo, umati mkubwa wa zaidi ya watu 200 walikusanyika nje ya mochari ya hospitali ya Wilaya ya Tarime, wengi wao wakiwa ni wafuasi wa Chadema, wakizuia miili ya waliouawa kuchukuliwa na ndugu zao tangu mwanzoni mwa wiki.

Katika vurugu hizo za kutupiana mawe, Mwandishi wa ITV, George Marato, aliporwa kamera yake.

Kwa mujibu wa Lucy Lyatuu, Balozi Kagasheki akifafanua kuhusu tukio hilo, alisema mapambano hayo kati ya Polisi na raia yameanza kuchukua sura ya kisiasa, baada ya chama cha kisiasa kuanza uchochezi kikishawishi wanafamilia kutozika miili hiyo.

Serikali pia imepinga kufanyika kwa maandamano yaliyoandaliwa na chama hicho, bila kukitaja jina kutokana na ishara kuwa ni ya shari na yasiyo salama.

Balozi Kagasheki alisema hayo jana Dar es Salaam na kuongeza kuwa Serikali itagharimia mazishi ya wananchi waliokufa.

Kuhusu uchochezi wa kisiasa, alisema kuna shinikizo la kisiasa ambapo chama hicho kinataka kufanya maandamano katika eneo hilo na mkutano wa hadhara.

Alisema, chama hicho kimetuma ombi la kibali cha kufanya hivyo, lakini Serikali imekataa kutokana na ishara hizo na kauli za viongozi wa chama hicho, kuwaambia wananchi waliofiwa wazike baada ya maandamano na mkutano wa hadhara.

“Masuala ya siasa hadi kwenye maiti … kibali cha maandamano hakitokuwapo, tumieni muda huo kutatua matatizo mengine ya wananchi, ambayo yatasaidia kuleta maendeleo,” alisema Balozi.

Akizungumzia mgodi huo, alisema yamekuwepo matukio mbalimbali katika eneo hilo na Mei 7 mwaka huu wananchi walianzisha ghasia na kuvamia mgodi na kupora.

Mbali na siku hiyo, Kagasheki alisema Mei 14 wananchi pia walirudi katika eneo hilo na kuvamia na kupora ingawa walipambana na Polisi.

Kutokana na tukio hilo, Inspekta Jenerali wa Polisi (IGP), Said Mwema ametuma timu ya maofisa wake kuchunguza na kuzungumza na familia hizo, ili ziache siasa na Waziri wa Nishati na Madini, William Ngeleja, atalitolea tamko suala la wachimbaji wadogo.

Kuhusu sababu za Serikali kuzika watuhumuwa wa uhalifu, Kagasheki alisisitiza kuwa pamoja na kwamba ni wahalifu waliovunja sheria, bado ni Watanzania.

Wakati huo huo, Namsembaeli Mduma, anaripoti kwamba kampuni ya African Barrick Gold (ABG) inayomiliki mgodi huo, imesema itatoa elimu zaidi kwa jamii inayouzunguka kuhusu umuhimu wa machimbo hayo kwa maendeleo yao na ya nchi.

Kampuni hiyo imesema hiyo ndiyo njia salama ya kushawishi kuacha uvamizi, wizi na uharibifu dhidi ya migodi nchini.

Msemaji wa Kampuni hiyo, Teweli Teweli, aliliambia gazeti hili Dar es Salaam, kuwa licha ya uvamizi wanaofanyiwa na wananchi hao kila mara, hawataki kuendelea kuona vifo vikitokea au damu ikimwagika.

Akieleza sababu za kuvamiwa huko kila wakati, Teweli alisema ni kutokana na wananchi kufahamu siri ya ulinzi uliopo katika mgodi huo ambayo kwa asilimia 100 hawauogopi.

“Kampuni yetu ilikula kiapo cha kulinda haki za binadamu kwa mujibu wa matakwa ya Umoja wa Mataifa (UN), hivyo hairuhusu walinzi wake kuwa na silaha za moto au kutumia nguvu inayoweza kuhatarisha maisha ya mtu.

“Suala hilo limefahamika kwa kila mwanakijiji katika eneo la mgodi, na hivyo kuwafanya wasihofie kufanya uvamizi wakati wowote,” Teweli alisema.

No comments: