Friday, June 22, 2012

Wakazi wa Kata ya Ijombe - Mbeya Vijijini watoa kilio chao kuhusu huduma duni za kijamii kutokana na uongozi mbovu


Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP), ni shirika lisilo la kiserikali linalopigania usawa wa kijinsia, haki za binadamu na ukombozi wa wanawake kimapinduzi. TGNP kwa kushirikiana na wadau mbalimbali inapambana na mifumo kandamizi ikiwemo mfumo wa kibepari, kibeberu, utandawazi na mfumo dume. Kuanzia mwaka 2008, TGNP imeelekeza nguvu zaidi katika ujenzi wa TAPO (vuguvugu) ngazi za kijamii, kama sehemu ya kutambua na kuchambua masuala ya vipaumbele kwa wanawake na wanaume walioko pembezoni.

Kuanzia tarehe 21 hadi 31 Mei 2012, kikundi cha waraghbishi kutoka TGNP wamefanya mchakato shirikishi wa uraghbishi katika vijiji vya Nsongwi Juu, Ifiga, Iwalanje, Nsongwi Mantanji na Ntangano Ijombe,Kata ya Ijombe, Wilaya ya Mbeya Vijijini mkoani Mbeya.

Wakazi wa Kata ya Ijombe wameelezea kero mbalimbali ikiwemo ya ukosefu wa masoko kwa mazao wanayolima, ambapo madalali hununua mazao kwa bei ndogo na kwenda kuuza kwa wafanyabiashara wakubwa bila wao kupata faida. Sambamba na hilo, ushuru pia ni kero kubwa.

Kuna ushuru wa aina mbili ukiwemo ushuru wa mazao shambani na ushuru wa mazao yakifika sokoni, ambao wanalipa bila stakabadhi kutolewa. Kwa ushuru wa shambani kila gunia ni shilingi 1000/- na ushuru wa mazao sokoni ni shilingi 200/- kwa mchuuzi. Wakati huo huo, wakazi wa Ijombe wamedai katika Kata yao hakuna utawala bora kwani baadhi ya viongozi hawaweki wazi taarifa za mapato na matumizi na huu ni uvunjaji wa sheria. 

Vilevile, wanawake wamedai kuwa wanakabialiana na ukatili wa kijinsia toka kwa wanaume ikiwa ni pamoja na kuuza mazao kinyemela, kutokuhudumia familia, kutolipa ada za shule kwa watoto, wanawake kupigwa kutokana na ulevi uliopindukia wa waume zao.

Huu umekuwa ni mzigo mkubwa kwa wanawake wa Ijombe na wameuomba uongozi husika hasa katika ngazi za vitongoji, vijiji na Kata waweze kufuatia kero hizi na kuweka sheria zitakazowabana wanaume kutokana na vitendo vyao. Pia wakazi wa Ijombe wameomba uongozi kufuatilia na kudhibiti muda wa kuuza pombe. Wanapendekeza vilabu vifunguliwe kwa muda maalum uliopangwa. Kisheria vilabu vinapaswa kufunguliwa saa kumi jioni na kufungwa saa tatu usiku, na sio kufunguliwa saa moja asubuhi kama ilivyo kwa sasa.

Kero nyingine waliyotoa ni mimba za utotoni kutokana na ukosefu wa mabweni kwa wasichana wanaosoma katika Shule ya Sekondari ya Kata ya Iwalanje.
Shule ya Iwalanje imekuwa mbali sana na makazi ya walio wengi. Wanafunzi wanatembea umbali wa kati ya kilometa 4 hadi 8 kutoka vijiji vinavyotumia shule hiyo. 

Tatizo hili la umbali limepelekea baadhi ya wanafunzi kupanga vyumba vinavyojulikana kwa jina maalum la ‘GHETO’.
Wakazi wa Kata hiyo wamedai kuwa kutokana na kuishi kwenye magheto kwa muda mrefu kumepelekea wasichana wengi kutokufanya vizuri katika masomo yao.

Wasichana walio wengi, wamegeuka kuwa wapishi na wanasaka maji, kuni kwa ajili ya kujipikia chakula.
Kwa maana hiyo wasichana wamekuwa wakitumia muda wao mwingi zaidi kufanya kazi zilizo nje ya masomo tofauti na watoto wa kiume ambao muda mwingi wamekuwa wakijisomea.
Zaidi ya hayo wakazi wa Ijombe wamekiri kuwa wasichana wengi wamepata mimba za utotoni kwa kukosa ulinzi kwani baadhi ya magheto wanaishi watoto wa kike na wakiume.

Pia kuna hatari kubwa ya kuongezeka kwa maambukiza ya magonjwa hatarishi kama vile Ukimwi.
Vilevile, wakazi wa Kata ya Ijombe wamedai kuwa michango ya shule imekithiri. Kwa mfano michango inayotolewa ni shilingi 10,000/- kwa kila kichwa kwenye kaya. Kwa wale ambao wanaoshindwa kutoa mchango huo, kwa ajili ya maisha kuwa magumu hukamatwa na kupelekwa mahakamani; na ili waachiliwe huru wakazi hao hutakiwa kutoa shilingi 67,000/=.

Pia wakazi wa Ijombe hutoa shilingi elfu ishirikini (20,000/=) kwa mwaka kwa wanafunzi wanaoishi nyumbani na kwenye magheto. Michango yote kwa mwaka kwa mtoto anayeanza sekondari ni zaidi ya shilingi laki tatu na elfu hamsini (350,000/-), zikijumuisha fedha za madawati, vitambulisho, bima za afya, tahadhari, sare za shule,madaftari na rimu za karatasi. Michango hii inakuwa ni kikwazo kwa wazazi ambao kipato chao ni kidogo.

Kwa wanafunzi wanaoishi mashuleni wanalipa laki nne na nusu (450,000/-) tu kwa mwaka.
Vilevile, Kata ya Ijombe hasa kijiji cha Iwalanje kuna tatizo la maji kwa muda mrefu . Wakazi wa Iwalanje wamedai kuwa kijiji chao kimekuwa kikitoa mchango kwa ajili ya kupata maji kwa takribani miaka kumi na nne iliyopita bila mafanikio.

Wanawake ndio waathirika wakubwa wa tatizo hili. Wanawake wa eneo hili wamesema wamekuwa wakiamka saa kumi alfajiri kwenda kusaka maji na kurudi saa tatu asubuhi, wakati huo huo wanawake wanapata kipigo toka kwa waume zao kutokana na kuchelewa kurudi.
Wanawake wa Ijombe wameiomba serikali kufuatilia kwa karibu tatizo hili kwani linawakosesha mapato kutokana na kutoweza kushiriki katika kazi za uzalishaji.

Mwisho wakazi wa Ijombe wamekiri kuwa kero zote zilizokithiri katika Kata yao, zinatokana na uongozi mbovu, hasa viongozi kutokufuatilia kwa karibu masuala yanayowagusa wananchi wao na kuwepo kwa ubinafsi zaidi, kuchanganya masuala ya kisiasa na masuala ya kimaendeleo.

Pia viongozi wametakiwa kujua wajibu wao kila mmoja katika nafasi yake Wakazi hao wameomba viongozi wawe na mawasiliano na wananchi kwa kujadili kero zinazowakabili na kutafuta ufumbuzi wa matatizo yao kwa pamoja.

Imetolewa na Waraghbishi, Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP)

No comments: