Thursday, June 21, 2012

Wabunge wajadili Bajeti, siyo kuporomosha matusi

TUNAPATA shida kuamini kwamba wawakilishi wetu bungeni wanaweza kulidhalilisha Bunge kwa kuendesha malumbano yasiyo na tija na kuporomosheana matusi badala ya kutumia  muda huo kujikita katika kujadili Bajeti ya Serikali iliyowasilishwa bungeni humo wiki iliyopita. Ni vigumu pia kuamini kwamba mporomoko wa maadili katika nchi yetu umesambaa kila sehemu kiasi cha kujipenyeza pia katika chombo nyeti kama Bunge.
 
Juzi na jana gumzo kubwa miongoni mwa wananchi na katika mitandao ya kijamii lilihusu aibu iliyotokana na vioja vya  wabunge wengi walipokuwa wakichangia mjadala huo kuhusu Bajeti ya Serikali ya 2012/13. Wakati wananchi wakitegemea kusikiliza hoja nzito za wabunge na uchambuzi wa kina kuhusu vifungu mbalimbali vya bajeti hiyo na namna ya kuondokana na na matatizo lukuki ya kiuchumi, walipigwa butwaa kuona  mijadala hiyo ikitawaliwa na vijembe, matusi na vitisho vya kila aina, huku ikionekana dhahiri kwamba wabunge wengi walikuwa wanapata shida kuweka kando tofauti zao za kiitikadi na kisiasa.
 
Lakini tatizo linalojitokeza hapa ni utashi wa kisiasa kwa upande wa Spika, Naibu Spika na wenyeviti wa Bunge ambao wanaendesha vikao vya Bunge. Zimejitokeza kasoro za hapa na pale wakati Spika, Naibu Spika na wenyeviti hao wanapoendesha vikao hivyo, kasoro ambazo zimeacha maswali mengi siyo kuhusu uwezo wao wa kuendesha vikao hivyo, bali utashi wa kisiasa wa kuhakikisha wanatenda haki kwa kila mbunge bila kujali itikadi yake au chama cha siasa anachotoka. Tofauti na wanavyofanya kwa wabunge wa upinzani, mara nyingi wameonyesha udhaifu wa kuhofia kuwawajibisha wabunge wa chama tawala wanapovunja Kanuni za Bunge.

 
Hiki ndicho chanzo cha kasheshe tunayoishuhudia bungeni hivi sasa. Ndiyo maana badala ya wabunge kuijadili bajeti hiyo kwa lengo la kuiboresha wamejipanga katika kambi mbili, moja ikiwa ya wabunge wa chama tawala ambao wameunga mkono bajeti hiyo ya Serikali kwa asilimia mia moja na nyingine ikiwa ya vyama vya upinzani ambayo imeikataa bajeti hiyo pia kwa asilimia mia moja. Kwa mtindo uleule wa jino kwa jino, wabunge wa chama tawala wameikataa katakata Bajeti mbadala iliyowasilishwa na Kambi ya Upinzani Bungeni, huku kambi hiyo ya upinzani ikiiunga mkono bajeti hiyo kwa asilimia moja.
 
Hivyo ndivyo vioja vya Bunge hili linaloendelea na vikao vyake mjini Dodoma kujadili Bajeti ya Serikali ya mwaka ujao wa fedha. Tusidanganyane, hakuna jambo la maana linalofanyika kule Dodoma hivi sasa. Kama tumewatuma wabunge waijadili Bajeti na kwa kauli moja kurekebisha pale panapohitaji kurekebishwa ili hatimaye ipitishwe bajeti endelevu yenye kutilia maanani maendeleo ya nchi na maslahi ya wananchi wote, wabunge hao wanakuwa wasaliti wakubwa  wanapofanya kinyume na matarajio ya wananchi ambao ndiyo hasa waliowapa ridhaa ya kuwawakilisha bungeni.
 
Kama moja ya habari tuliyochapisha katika toleo la gazeti hili leo inavyosema, wananchi waliohojiwa jana walisema pasipo kutafuna maneno kwamba bajeti zote mbili, yaani ya Serikali ya chama tawala na ya Kambi ya Upinzani Bungeni zinafaa kutumika kwani zote zina vipengele vingi vinavyofaa kuingizwa katika Bajeti ya pamoja. Kwa maneno mengine, wananchi wanasema inahitajika Bajeti mwafaka yenye kutilia maanani michango ya wabunge wa pande zote mbili.
 
Pamoja na wabunge wengi kufanya vituko vilivyowafadhaisha wananchi, tunayo matumaini kwamba hali hiyo inaweza kurekebishwa iwapo uongozi wa Bunge na wabunge watatimiza wajibu wao na kuweka mbele maslahi ya taifa. Bado upo muda wa kutosha kufanya hivyo kwa kujadili mambo ya msingi, ikiwa ni pamoja na kutafuta suluhisho la kukua kwa deni la taifa, mfumuko wa bei, kupambana na umaskini, kuboresha kilimo, ajira kwa vijana na utekelezaji wa Mpango wa Maendeleo wa Miaka Mitano.

No comments: