Thursday, April 9, 2009

Mrejesho wa GDSS: Mrejesho wa Utafiti wa 'Hatuna Chaguo'

Katika mfululizo wa semina za GDSS wiki hii ya tarehe 08/04/2009 mada ilikuwa ni "Mitizamo na Uzoefu wa Wanawake wa Kitanzania, Wahudumu wa Afya na Wakunga wa Jadi" Lengo la semina ni kuangalia na kujadili mrejesho wa utafiti uliofanywa na Utu Mwanamke, Care TZ, Chama cha wakunga wa jadi Tanzania(TAMA)na GRAFCA, katika wilaya tatu za Tunduru, Mpwapwa, na Kwimba. Utafiti huu uliobeba jina la 'Hatuna Chaguo'(We have no Choice), ulilenga kuelewa vikwazo vikuu ambavyo wanawake wanakumbana navyo katika upatikanaji na utumiaji wa huduma za kujifungua, na vikwazo ambavyo watoa huduma wanakumbana navyo katika utoaji wa huduma bora za kujifungua.

Mtoa mada dada Festa Andrew kutoka Utu Mwanamke, alitoa mrejesho wa utafiti huo na kutoa nafasi kwa washiriki kujadili ripoti ya tafiti hiyo. Tafiti imeonyesha wanawake waliohojiwa wanapenda kujifungulia katika vituo vya afya, isipokuwa hali ya umasikini waliyonayo na ubora hafifu wa huduma hizi katika vituo vya serikali inawapelekea wajifungulie nyumbani ama kwa wakunga wa jadi. Vikwazo vingine ambavyo vinavyochangia wanawake kutokwenda kujifungulia katika vituo vya afya ni pamoja na; Umbali kufikia katika vituo vya huduma- kwa mfano, Tunduru kituo cha karibu ni kilomita 32; Mpwapwa ni kilomita 58-, Ukosefu wa usafiri wakati wa uchungu, gharama zilizo rasmi na zisizo rasmi. Shuhuda zinaonyesha kwamba sera ya serikali ya kutoa huduma za uzazi bila malipo haijatosheleza au haitekelezwi kikamilifu.

Utafiti pia ulitoa Mapendekezo kwa ajili ya koboresha Upatikanaji, Utumiaji, na Utoaji wa Huduma za kujifungua ni pamoja na:

• Kueneza, kutekeleza, na kusimamia kitaifa sera ya serikali inayowaondolea wanawake malipo kwa ajili ya huduma ya uzazi.
• Kupanua huduma kabambe za dharura za uzazi –ikiwemo upasuaji- kwa hospitali zote za wilaya na asilimia 50 ya vituo vya afya ifikapo 2015. Kipaumbele zaidi kwa maeneo ya pembezoni.
• Kuanzishwa kwa mfumo imara wa afya ili kuhakikisha uwajibikaji katika utoaji wa huduma bora za afya.
• Kusambaza kitaifa ‘Mkataba wa huduma kwa Mteja’ ili watumiaji huduma wajue haki zao.
• Kuanzishwa utaratibu imara wa wazi wa kushughukia malalamiko, utakaoshughulikia maoni ya watumiaji wa huduma na watoa huduma.
• Kuajiri na kusambaza watumishi wa afya wenye ujuzi ili kupanua magawanyo wa wakunga wenye ujuzi kwenye maeneo ya pembezoni.
• Kuhakikisha maji, usafi, huduma za utupaji taka, na umeme wa kuaminika vinapatikana katika vituo vyote vya afya.
• Kuwa na usambazaji mfufulizo kwa madawa muhimu kwa ajili ya kujifungulia.

Katika kuhitimisha mtoa mada aliwapa nafasi washiriki waweze kuchangia juu ya utafiti na kuangalia jinsi ya kupeleka taarifa hizi kwa wananchi na kuandaa na mpango wa pamoja katika kufanikisha mapendekezo haya yanafanyiwa kazi na serikali.

Washiriki waliona vifo hivi vinavyotokana na uzazi (wanawake 24 wanakufa kwa siku, 8000 kwa mwaka) bado ni changamaoto kubwa ambayo wanaharakati wanaweza kuwahoji wanasiasa katika kipindi hiki cha kuelekea uchaguzi wa serikali za mtaa na uchaguzi mkuu mwakani, je wamefanya nini ama wamejipanga vipi kuhakikishga vifo hivi vinapungua?

Pia ni muhimu kwa wanaharakati kuandaa mkakati maalumu wa 'kuichallange' serikali ili iboreshe sekta ya afya, ukiangalia kwa makini guideline za bajeti kwa mwaka huu 2009/10 inaonyesha wazi kwamba bado sekta ya afya haijapewa kipaumbele sana na serikali yetu(Afya, Maji, na elimu imepewa 29.2% ya bajeti yote), ingawa serikali yetu ilisaini makubaliano ya Abuja juu ya afya ya mwaka 2001. Je serikali inatekeleza mkataba huu wa Abuja na mikataba mingine inayoitaka kuongeza bajeti ya sekta ya afya?

Wanaharakati walibainisha ukosefu wa rasilimali ni changamoto mojawapo ambayo inakwamisha kupeleka elimu kama hii kwa wananchi walio wengi maeneo ya vijijini ambao ndio wenye matatizo makubwa ya kupata huduma hizi za uzazi na afya kwa ujumla.

Pia washiriki walipendekeza iandaliwe mijadala ya kitaifa ambayo itajadili hali hii ya vifo vinavyotokana na uzazi kote nchini, ikianzia katika ngazi ya serikali za mitaa na kata, kupitia katika kamati za afya za mitaa, vijiji na kata.

Jamii inapaswa kuelimishwa kwamba vifo hivi vinavyotokana na uzazi havitokani na mipango ya Mungu na wala si hali ya kawaida, bali ni hali ambayo inawezwa kuzuilika kabisa ikiwa wanajamii watasimama pamoja na kuifanyia kazi kuitokomeza.

Kwa utashi imara wa kisiasa na mikakati ya kutoa maamuzi katika ngazi zote, vifo vitokanavyo na uzazi nchini Tanzania vinaweza kupunguzwa kwa haraka. Kama mwananchi unashiriki vipi katika kufanikisha vifo hivi vya uzazi vinatokemea?

No comments: