Thursday, April 23, 2009

Elimu kwa Vijana na Watu Wazima Tanzania: Je, Imepewa Kipaumbele?

Katika mfululizo wa semina za GDSS, jumatano ya tarehe 22/04/2009 mada ilikuwa ni “Elimu kwa Vijana na Watu Wazima Tanzania; Je, Imepewa Kipaumbele? Watoa mada walikuwa ni Profesa mshiriki kutoka UDSM dada E.P Bhalalusesa na Anthony Itelema afisa elimu kutoka wizara ya Elimu kitengo cha elimu kwa watu wazima, na mwezeshaji alikuwa ni dada Shekilango.

Dada Bhalalusesa alieleza maana ya kuelimika kama ilivyotafsiriwa na UNESCO; ni uwezo wa mtu kusoma na kuandika katika maisha yake ya kila siku. Mtu wazima ni mtu yeyote anayekubali majukumu katika jamii na anayejitegemea na vijana walitafsiriwa kuanzia umri wa miaka 14-35.
Aprili 2000, wawakilishi kutoka nchi 164 walikutana Dakar senegal na kukubalina juu ya Azimio la elimu kwa wote duniani (World Declaration on Education For All- EFA), miaka saba baadae(2007), kuna zaidi ya watu wazima milioni 774 wasiojua kusoma wala kuandika duniani, wanawake wakiwa 64% ya watu wote wasiojua kusoma. Nchini Tanzania EWW ilikuwa na msukumo sana baada ya uhuru mpaka mwanzoni mwa miaka ya 1980 ilipoanza kushuka kutokana na sera mpya za SAPs. Juhudi za serikali za kutaka kufikia usawa kupitia elimu ziliisha na nguvu kuelekezwa katika shughuli za kiuchumi, hivyo EWW haikuwa tena ajenda kuu katika maendeleo ya nchi. Vituo vingi vya EWW vilifungwa kutokana na utoro, pia serikali iliacha kutoa fedha kwa ajili ya EWW. Kwa sasa idadi ya watu wasiojua kusoma nchini Tanzania inakadiriwa kufikia 69.4% ya wananchi wote.

Mwaka 2000+ juhudi za kutokomeza ujinga kwa watu wazima zikaanza upya, serikali kupitia wizara ya elimu ikandaa na kutekeleza sera na mipango kadhaa yenye lengo la kuurithi mpango wa EWW. Mipango kama MKUKUTA, MEMKWA, MUKEJA, ilibuniwa na kutekelezwa ili kuhakikisha dira ya taifa ya mwaka 2025 yenye lengo la kuwa na jamii iliyoelemika ikifikiwa. Lakini pamoja na juhudi hizi bado kuna changamoto nyingi ambazo serikali inakutana nazo ambazo ni pamoja na; tafsiri mbaya ya dhana ya elimu ya watu wazima, ukosefu wa sera na mipango thabiti ya kuinua EWW, upungufu wa rasilimali, kukosekana kwa utashi wa kisiasa, na wananchi kukosa utashi wa kushiriki katika mipango hii.

Pia washiriki waliainisha changamoto zingine katika sekta ya elimu nchini ambazo ni; kukosekana kwa sera ya wazi ya EWW, umasikini unasababisha wananchi wengi kushindwa kushiriki katika maswala ya elimu, kukosekana kwa uzalendo kwa wananchi na viongozi kunakosababisha jamii ikose upendo, serikali haijatoa kipaumbele kwa mpango wa EWW, hivyo mpango huu hauna malengo, mipango na rasilimali za kutosha kuutekeleza.

Nini kifanyike?
Katika nini kifanyike, washiriki walipendekeza maoni yafuatayo;

• Wananchi wawashinikize viongozi wao wanaoomba kura wawaeleze mipango yao ya kuboresha EWW kabla ya kuwapigia kura, na wanasiasa waahidi kutekeleza ahadi hizo.
• Serikali iianzishe vituo vya EWW kuanzia ngazi ya Kata na kutoa ruzuku ya kutosha kwa vituo hivi ili viweze kutoa huduma.
• CBOs zishirikiane na serikali katika kuboresha EWW nchini kote.
• Wizara ipitishe mpango wa kuwatumia walimu waliopo kufundisha katika vituo vya EWW kama overtime, hii inaweza kupunguza upungufu wa walimu wa EWW.
• Turudishe moyo wa zamani wa uzalendo ambao ulitusaidia kulitumikia taifa letu, tofauti na sasa ambapo viongozi wengi wapo kwa ajili ya maslahi binafsi.
• Tutafute falasfa ya kutungoza katika swala la elimu. Enzi za mwalimu, falsafsa yetu ya Elimu ya Kujitegemea ilisaidia sana kujenga jamii ambayo iliweka mbele maslahi ya taifa na hivyo elimu ilipewa kipaumbele katika mapambano dhidi ya ujinga.
• Serikali iwe na sera thabiti ya EWW, tofauti na sasa ambapo kuna mipango kadhaa ambayo inatumiwa kama dira ya kufikia malengo ya EWW kwa wote.

Kama Mwananchi wa kawaida unafanya nini kuhakikisha Elimu ya Watu Wazima Inaboreshwa Nchini Tanzania?

No comments: