Thursday, April 16, 2009

Filamu ya Nyerere kuonyeshwa DStv

Filamu ya Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere, inatarajiwa kuonyeshwa Jumapili ijayo katika chanel ya M-net kupitia DStv. Akizungumza na waandishi wa habari jana, mtayarishaji wa sinema hiyo kutoka Kampuni ya utengenezaji sinema, Savannah, Imruh Bakari alisema filamu hiyo ni ya dakika 51.

Alisema filamu ya Mwalimu Nyerere ni moja kati ya filamu sita zitakazoonyeshwa katika chanel hiyo zinazowazungumzia viongozi wengine mahiri wa Afrika. Bakari alisema sinema hiyo imetumia miaka miwili kuitengeneza na imeshirikisha wadau mbalimbali wa ndani na nje ya nchi.

Naye mwongozaji wa filamu hiyo, Lekoko Ole Levilal, alisema katika utengenezaji wake walikumbana na changamoto mbalimbali. Alisema changamoto kubwa mojawapo ni ugumu wa kutengeneza filamu kuhusiana na maisha ya mtu ambaye amefariki dunia. Filamu hiyo ilizinduliwa rasmi juzi, ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya Tamasha la Kimataifa la Mwalimu Julius Nyerere, linaloendelea Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.

No comments: