Monday, April 6, 2009

Mila potofu yakwaza maendeleo ya wanawake

Ukosefu wa elimu, mila potofu pamoja na mfumo dume vinachangia baadhi ya wanawake kushindwa kujikwamua kiuchumi kutokana na baadhi ya jamii kuamini hawawezi kuongoza mambo mbalimbali.

Hayo yalisemwa juzi jijini Dar es Salaam na Mratibu wa Mtandao wa Wanawake Barani Afrika (WiLDAF), Judith Odunga, wakati wa mafunzo ya siku mbili ya waandishi wa habari kuhusu Sera ya Maendeleo ya Wanawake na Jinsia.

Alisema ingawa sera hiyo imelenga kumkomboa mwanamke katika nyanja za siasa na uchumi lakini haijaweza kumsaidia kutokana na jamii hususan wanawake wenyewe kuwa na dhana potofu kwamba mwanamke mwenzao hawezi kuwaongoza.

“Nawasihi wanawake wenzangu wawachague wanawake wanaojitokeza kugombea uongozi katika ngazi mbalimbali, msiwakebehi pia ondoeni mfumo dume kwa kuwasomesha watoto wenu ili waweze kuwasaidia,” alisema.

Naye mwezeshaji kutoka Kituo cha Mafunzo na Maendeleo (TWIFUNDE), Yasin Ally, aliiasa jamii kuondoka na mila potofu zinazomkandamiza mwanamke na kuwasihi wanawake kujishughulisha na biashara mbalimbali zitakazowasaidia kujikwamua kiuchumi.

Imeandikwa na Veronica Mheta; Tarehe: 5th April 2009
HabariLeo

No comments: