Sunday, April 19, 2009

Mrejesho wa GDSS: Kampeni ya Utafiti wa Ugonjwa wa Fistula – Manyoni Singida.

Jumatano ya tarehe 15/04/2009 katika mfululizo wa semina za jinsia na maendeleo mada
ilikuwa ni Muendelezo wa Kampeni dhidi ya Fistula, ambapo ulitolewa Mrejesho wa Utafiti wa ugonjwa wa Fistula uliofanywa na Utu Mwanamke katika kata kumi na moja (11) za wilaya ya Manyoni mkoani Singida. Waongoza mada walikuwa ni Anna Sangai (TGNP) na Modestus Kamonga (Daktari Mwanafunzi -Muhimbili University).

Kampeni hii ilifanywa na timu ya watu kumi na moja, na wilaya ya Manyoni ilichaguliwa kwa sababu ni eneo ambalo limeathirika sana na ugonjwa huu. Wagonjwa 19 walipatiwa huduma na 11 kati yao waliletwa Dar es salaam kwa matibabu zaidi. Katika kampeni hii wananchi walifundishwa kuhusu Ukweli kuhusu Fistula, chanzo chake, madhara, jinsi ya kujikinga na fistula, na tiba zake.

Vyanzo ambavyo vinasababisha mwanamke apate fistula ni pamoja na; mtoto kuwa mkubwa kuliko viungo vya uzazi; mtoto kukaa vibaya tumboni; kupata ujauzito katika umri mdogo (wataalamu wanashauri kuanzia miaka 18); kupata ujazito katika kipindi kifupi (mama anashauriwa apumzike angalau miaka mitatu kabla ya kujifungua tena); sababu zinazosababishwa na wataalamu wa afya katika kuokoa maisha ya mama wakati wa kujifungua; mila potufu za ukeketaji na kujifungulia nyumbani kwa kuamini ni ujasiri; na matatizo ya ujauzito wa mara ya kwanza na kukosa msaada wakati wa kujifungua.

Fistula inaweza kuzuilika kama mama atapata huduma za mwanzo za kliniki hivyo ataweza kufahamu ni lini atajifungua, uweze na hali ya mtoto tumboni, kupata ushauri mbalimbali kutoka kwa wataalamu na pia mama akijiepusha na vihatarishi vilivyotajwa. Hospitali zinazotibu fistula ni pamoja na; Kituo teule CCBRT, Muhimbili, Bugando, Kambi Maalumu Dodoma, na KCMC-Moshi.

Hamasa ya kampeni.
Katika kampeni hii ya fistula mashirika kadhaa yalishirikiana kufanikisha zoezi hili, mshirika hayo ni; TGNP -Utetezi na Ushawishi, Utu mwanamke kutoa taarifa na takwimu mbalimbali, hospitali ya CCBRT kutoa bure huduma kwa wagonjwa waliopatikana, na habari zilisambazwa na kituo cha TBC 1.

Yaliyojiri katika kampeni.
Mambo matatu yaliyojiri ni; Tatizo la mfumo dume limechangia kwa kiasi kikubwa ugonjwa huu kuendelea kuwepo, kwa mfano baadhi ya wanaume wameshindwa kuwapeleka wake zao kliniki hivyo kukosa taarifa muhimu za maendeleo ya afya za wake zao; mila potofu ambazo zinalelewa na mfumo dume kwa mfano ukeketaji; wanawake kukosa sauti na maamuzi juu ya afya ya uzazi na kupelekea kuzaa bila mpangilio pamoja na kukosa huduma muhimu wakati wa kipindi cha ujauzito. Ukatili na ukali wa baadhi ya wahudumu wa afya ni chanzo kimojawapo cha fistula kilichotajwa katika utafiti huu (kwa mfano wahudumu wengine kutowahudumia wajawazito mpaka wapewe chochote kitu). Umbali wa vituo vya afya na makazi ya wanakijiji huchangia kwa kiasi kikubwa akinamama kupata fistula (kwa mfano katika baadhi ya vijiji vituo vya afya vya karibu vipo umbali wa kilomita 50, na mara nyingi vituo hivi havina madawa muhimu wala wataalamu wa kutosha, pia barabara hazipitiki na vituo hivi havina magari ya wagonjwa).

Nini Kifanyike?
* Kuwapa nguvu wanawake ili wajitambue na kuweza kupambana na mfumo dume ambao umechangia kuwakandamiza na kusababisha wakose fursa ya kupata huduma bora za afya ya uzazi kwa wakati muafaka na hatimaye kupelekea kupatwa na magonjwa kama fistula.
* Kutoa elimu zaidi kwa akina mama li waweze kutumia vituo vya afya vilivyopo karibu na maeneo yao na kujiepusha na mila potofu zinawagandamiza.
* Kupinga mila na desturi zote potofu ambazo zinazuia akinamama kujifungilia katika vituo vya afya na badala yake kushawishi wajifungilie
* Kuhimiza serikali kuandaa vifaa na wataalamu wa kutosha wa maswala ya afya ya uzazi kwani ni jukumu la serikali kuandaa vitu hivyo na vitasaidia kupunguza wanawake kupata fistula na vifo vya uzazi.
* Kuandaa ajenda ya kitaifa ili kuuelimisha na kuhamasisha umma juu ya ugonjwa huu wa fistula na umuhimu wa kuutokomeza ugonjwa kwani inawezekana.
* Ushirikishwaji wa wanaume katika huduma ya afya ya mama na mtoto ni muhimu uwe wa pande mbili badala ya kuachiwa akina mama peke yao, hivyo kuweka msukumo kwa akina baba kwenda kliniki na wake zao ili kuweza kuwa na taarifa za afya za wake zao.


Kama Mwanaharakati unafanya nini kuhakikisha Fistula inatokemezwa nchini Tanzania? Je, Unashiriki vipi katika kukomesha Fistula?

Kwa maelezo zaidi tembelea; www.womensdignity.org

No comments: