Friday, April 3, 2009

Mrejesho wa GDSS: Je, Bajeti Mpya Itawanufaisha Wanawake? Uchambuzi wa Muongozo wa Bajeti 2009-12 Kwa Mtizamo wa Ukombozi wa Wanawake Kimapinduzi.

Mfululizo wa semina za GDSS, jumatano ya tarehe 1/04/2009, mada ilikuwa ni Uchambuzi wa Muungozo wa bajeti kwa mwaka wa fedha 09/12 uliotolewa na serikali kwa mtizamo wa Ukombozi wa wanawake kimapinduzi. Mada hii iliwakilishwa na Glory Shechambo na Marjorie Mbilinyi (TGNP)

Mada ililenga kuchambua mambo makuu mawili; kwanza, Mgawanyo wa fedha kulingana na vipaumbele vya Serikali na Mtarajio ya wananchi walio wengi; pili, Nafasi ya wananchi katika utayarishaji wa bajeti.
Katika uchambuzi mambo makuu yaliyoangaliwa ni pamoja na; Kukua na Kuyumba kwa Uchumi wa nchi, Maendeleo ya sekta kulingana na Malengo Matatu ya MKUKUTA- Kupunguza umasikini wa kipato, Ustawi wa jamii, na Utawala bora, nk. Mambo yaliyojitokeza katika uchambuzi;-
• Uchumi wa Nchi unaonekana umekuwa kwa 7% kwa mwaka 2001-07
• Mfumuko wa Bei umekua kwa 3%-10% kwa mwaka 2007-08
• Matumizi ya serikali yamezidi kutoka tilioni 7.2 (08/09) hadi tlioni 8.1 (09/10)
• Kushuka kwa thamani ya shilingi kwa 13.2%

Vipaumbele vya serikali kwa mwaka huu wa fedha ni; Miundombinu-barabara na mawasiliano-, ajira, Kilimo cha Umwagiliaji, Madini na Nishati. Na vipaumbele vya wanaharakati ni Maji, Afya, Elimu, Ukatili wa Kijinsia na HIV. Mgawanyo wa Fedha kulingana na malengo matatu ya MKUKUTA kwa mwaka wa fedha 09/10 ni kama ifuatavyo; Kupunguza Umasikini 51.2% pungufu kwa 2.9%,Ustawi wa Jamii 29.2% pungufu kwa 4.9%, na Utawala Bora 19.5%.

Muongozo huu wa bajeti umeacha maswali kadhaa bila kujibiwa; Mfano; Kwa nini bado kuna upungufu wa chakula nchini? Ni ajira gani zilizoongezeka? Na njia zilizotumika kuongeza ajira hizo? Katika elimu hakielezwi ni kiasi gani cha fedha kilichotengwa katika kuendeleza elimu? Kulipa madai ya walimu? Kununua vitabu? na kujenga nyumba za walimu? Katika afya, hakielezwi kiasi kilichotengwa kulipia wauguzi wa afya? Kuongeza watumishi? Kupunguza vifo vya akina mama na watoto?

Mambo kama Maji, Rushwa na Ufisadi, Kuuguza wagonjwa wa UKIMWI, Usalama wa Walemavu-albino-, asilimia ya wanawake katika ngazi za maamuzi na Uimarishaji wa ushirikishaji wa jamii katika Utayarishaji wa bajeti hayakuchambuliwa katika muungozo huu wa bajeti.

Changamato Zilizopo.
1. Swala la Uwazi katika maandalizi ya bajeti, raia wa kawaida wameshindwa kushiriki katika maandalizi ya bajeti. Pia Muungozo wa Bajeti umeandaliwa kwa Lugha ya Kiingereza na Kuchelewa kusambazwa, vitu ambavyo vimepelekea wananchi wengi wa kawaida kushindwa kushiriki katika uandalizi huo. Wananchi wanaweza kushiriki katika mchakato wa bajeti katika Nyanja mbili; kuandaa budget na kufuatilia matumizi ya bajeti.

2. Ongezeko la bei (Inflation) limetumika kama kigezo kikuu cha kuendelea kuomba misaada na kushuka kwa thamani ya shilingi. Utegemezi kwa nchi wahisani kwa mwaka wa huu 09/10 ni 34.5%, kitu amabacho kinatishia uhuru wetu wa maamuzi, misaada hii huambatana na masharti mengi.

3. Maswala kama mgawo wa umeme, mishahara ya wabunge, udhibiti wa maliasili, Ufisadi, mapato ya madini na swala la wachimbaji wadogo hayajagusiwa sana katika muungozo huu wa bajeti

4. Serikali imeendelea kushindwa kuandaa mazingira ya kuwawezesha wananchi wa kawaida kuwekeza na kuzalisha, badala yake imekuwa ikiendelea kuwanyanyasa kwa mfano kuwasumbua wafanyabiashara wadogo.

Nini Kifanyike?
Wanaharakatia waliweza kukubaliana Mambo Makuu Matatu;
1. Tunahitaji kuwa na Muungozo Mbadala wa Bajeti, ambao utakuwa wazi na kutoa fursa kwa wananchi kushiriki katika maandalizi ya bajeti, na kohoji na kusimamia matumizi ya fedha hizo.
2. Wananchi watumie fursa ya Uchaguzi iliyopo mwaka huu wa 2009 na 2010 kuchagua viongozi wa serikali wa mitaa, wabunge, na Rais kuchagua viongozi amabo wataweza kuwajibika kwa maslahi ya wengi.
3. Wanaharakati wafuatilie Maazimio wanayofikia mara kwa mara katika vikao na semina mbalimbali.

Ukiwa kama mwanaharakati unashiriki vipi katika kuandaa bajeti mbadala inayowajali wanawake?

No comments: