Friday, February 26, 2010

Aliyemshushua Mkapa sasa kutuzwa

-Ni Clare Short aliyeshupalia Tanzania kutoinunua

NYOTA ya Waziri wa zamani wa Uingereza wa ushirikiano wa kimaendeleo, Clare Short, aliyekuwa mstari wa mbele kupinga ununuzi wa rada ya Tanzania kiasi cha kutofautiana na Rais wa Awamu ya Tatu, Benjamin Mkapa inazidi kung’ara nchini na Raia Mwema imebaini kuwapo kwa maandalizi ya kumpatia tuzo mahsusi kama sehemu ya kutambua juhudi zake hizo ambazo zimebainika kuwa na maslahi kwa Watanzania.

Kama tuzo hiyo itatolewa, basi, itakuwa ya kwanza kutolewa kwa Waziri kutoka Ulaya. Claire Short alifikia hatua ya kutishia kujiuzulu wadhifa wake katika Bunge la nchini kwake ili kuonyesha msimamo wa kutetea wananchi wa nchi masikini kama Tanzania.

Mama huyo ndiye Waziri aliyeanzisha mzozo wa kupinga ununuzi wa rada hiyo katika Bunge la Uingereza, nchi ambayo ni mfadhili wa maendeleo ya Tanzania, na hasa bajeti ya Taifa ambayo zaidi ya asilimia 30 hutegemea wafadhili.

Hoja zilizokuwa zikitumiwa na Short katika kupinga ununuzi huo ni pamoja na rada hiyo kuuzwa bei ghali tofauti na thamani halisi lakini pia ubora wake kuwa ulikuwa ni wa kutia shaka. Rada hiyo ilinunuliwa kutoka Kampuni ya utengenezaji na uuzaji vifaa vya kijeshi ya Serikali ya Uingereza ya BAE Systems.

Uchunguzi wa Raia Mwema kwa wiki kadhaa sasa umebaini kuwa maandalizi ya utoaji tuzo hiyo yanafanywa na Kituo cha Msaada wa Sheria na Haki za Binadamu Tanzania (LHRC), cha jijini Dar es Salaam kwa kushirikisha wadau wengine kadhaa wakiwamo wasomi mashuhuri nchini.

Hata hivyo, alipoulizwa kuhusu kuwapo kwa maandalizi hayo, Mkurugenzi wa LHRC Francis Kiwanga hakuwa tayari kuthibitisha wala kukanusha lakini akiweka bayana msimamo wa kituo hicho kwamba hakiridhishwi na kusuasua kwa Serikali katika kuwachukulia hatua wahusika wa kashfa hiyo ya rada, ambayo kwa maneno yake ni kuwa “chenji iliyorejeshwa ni ushahidi wa kutosha” kuwashughulikia wahusika.

“Kuhusu kutoa tuzo kwa Clare Short siwezi kuzungumzia hilo kwa sasa lakini nikwambie tu kwamba tumekuwa na mtandao rasmi wa kushughulikia masuala kama hayo ya rushwa. Sasa hilo la rada ni sehemu ya hayo, ni suala mahsusi ambalo linafanyiwa kazi ya uchambuzi wa kina ili baadaye tuamue kwa pamoja tunafanya nini…kama suala la tuzo litajitokeza sawa au mengine,” alisema Kiwanga.

Lakini Raia Mwema limebaini, mapema wiki hii, kwamba mazungumzo ya NGOs kadhaa kuhusu suala la kumtuza Claire Short yameshaanza na yanatarajiwa kuhitimishwa karibuni.

Katika hatua nyingine Kiwanga alisema; “unajua kwenye hii nchi kuna tatizo la impunity yaani watuhumiwa waliofanya hata makosa ya wazi ya ufisadi wanalindwa na system licha ya kuwapo kwa ushahidi wa wazi.”

Lakini alipoulizwa kama anaweza kuwa na mifano ya kuthibitisha hilo hakusita kutaja kashfa za Richmond, akihoji kuwa kwa nini Mramba (Basil, waziri wa zamani wa fedha) afikishwe mahakamani kwa kuitia hasara nchi lakini wengine katika Richmond na rada waachwe.

Soma Zaidi

Thursday, February 25, 2010

Pinda hafikirii kumrithi Kikwete

WAZIRI Mkuu, Mizengo Pinda, amesema hana mawazo ya kuwania urais kwa kuwa ni kazi kubwa, ngumu, na yenye lawama.

Waziri Mkuu ametoa msimamo huo jana mjini Tabora, baada ya mshairi Ramadhan Katwila ‘ Mv Liemba’, kusoma shairi akimwomba Mungu kumjaalia awe Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania baada ya Rais Jakaya Kikwete kumaliza ngwe yake mwaka 2015.

Pinda amesema hana hamu ya kuwa Rais, kwa sababu ni kazi ngumu tofauti na watu wanavyofikiri.

“Baba wa Taifa (Mwalimu Nyerere) alisema Ikulu si mahali pa kukimbilia, msifikiri kauli ile ni ya uongo.“Urais ni kazi ngumu. Hata hii kazi ya uwaziri mkuu ni ngumu sana, sema kwa vile tu ni lazima mzigo mzito akabidhiwe ‘Mnyamwezi’.

“Ni kazi ambayo kila mtu anakutupia lawama hata ambazo hustahili. Utasikia mwingine anasema kwanza liangalie lilivyo, kila siku utaandamwa na magazeti na kila mara utajikuta kwenye ‘The Komedi’,” alisema Waziri Mkuu.

Hata hivyo, alisema atakuwa tayari kumuunga mkono mtu yeyote atakayejitokeza kuwania urais baada ya kipindi cha Rais Kikwete kumalizika.

Awali Mwenyekiti mstaafu wa CCM wa Mkoa wa Tabora, Juma Nkumba, alimwomba Mungu ampe rehema Rais Kikwete aweze kumteua tena Pinda kuwa Waziri Mkuu mara baada ya kushinda uchaguzi mkuu ujao.

Jana Waziri Mkuu alikagua bwawa na lambo la Imalamihayo ambalo linatumika kama kuogesha mifugo ya wafugaji wa eneo hilo.

Akihutubia wafugaji hao, Pinda aliwataka wapunguze idadi ya mifugo ili kufuga kisasa na kuongeza tija na faida.

Alisema wilaya ya Tabora ina ng’ombe 54,000 ambao ni wengi kulingana na eneo hilo na hivyo kuathiri malisho ya mifugo hao hatua ambayo inawafanya kukosa afya inayotakiwa.

Baadaye Waziri Mkuu alifungua sekondari ya Nkumba ambayo ni kwa ajili ya wakazi wa kata ya Uyui na ambayo inakabiliwa na uchache wa walimu, ukosefu wa maabara, umeme na maji.

Katika hatua nyingine, Mbunge wa Tabora Mjini, Siraju Kaboyonga, aliwachangia wafugaji wa Imalamihayo Sh 100,000 na kutangaza kujenga kisima cha maji shuleni Nkumba, hatua ambayo wananchi katika jimbo hilo walisema angeifanya mapema bila kusubiri ujio wa Waziri Mkuu.

Wednesday, February 24, 2010

Mwanakijiji amshitua Pinda

WAZIRI Mkuu, Mizengo Pinda ameshtushwa na swali lililomtaka kutoa maelezo ya kwa nini Serikali inahofu kukubaliana na uamuzi wa Mahakama Kuu ya Tanzania iliyobariki mgombea binafsi.

Swali hilo liliulizwa jana na mkazi wa kijiji cha Ibushi, Joseph Mazwazwa, mara baada ya Pinda kukagua bwawa linalotumika kwa shughuli mbalimbali za binadamu, wanyama na kilimo.

“Mheshimiwa Waziri Mkuu ni kwa nini Serikali inahofia kuwapo kwa mgombea binafsi katika uchaguzi mkuu ingawa Mahakama Kuu ilishabariki kuwapo kwa mfumo huo katika uchaguzi?,” aliuliza.

Waziri Mkuu alimjibu kwa kusema, ni kweli Mahakama Kuu ilibariki mgombea binafsi baada ya kesi ya suala hilo kuwasilishwa mahakamani hapo.

Alisema hata hivyo suala hilo linaleta utatanishi kutokana na tafsiri ya kikatiba, kwa kuwa Katiba inasema mgombea katika nafasi za kisiasa, kama diwani, Mbunge na Rais, ni lazima atokane na chama cha siasa kilichosajiliwa.

Alisema, hatua hiyo ndiyo inayoleta utata kwa Serikali kukubaliana na uamuzi wa Mahakama Kuu wa kuruhusu kuwapo kwa mgombea binafsi.

“Ni sababu hizi hasa ndizo ambazo zimetufanya kupinga uamuzi huu wa Mahakama. Hata hivyo wenzetu bado wanataka mfumo huu uwepo na ndiyo maana wamekata rufaa katika chombo cha juu ambacho ni Mahakama ya Rufaa ili mfumo huu uruhusiwe.

“Hata hivyo kesi hii kwa ngazi ya Mahakama ya Rufaa bado haijatolewa uamuzi, kwa hiyo ni vigumu kueleza. Mahakama ya Rufaa ikibariki uamuzi huu basi hatutakuwa na la kufanya itabidi tukubaliane na matokeo katika suala hili,” alisema Waziri Mkuu.

Kesi ya kutaka Mahakama kukubaliana na kuwapo kwa mfumo wa mgombea binafsi, ilifunguliwa katika Mahakama Kuu na Mwenyekiti wa Chama cha Democratic (DP), Mchungaji Christopher Mtikila na Mahakama hiyo iliamuru mfumo huo kuanza kutumika, lakini Serikali ilikataa kutekeleza amri hiyo ya Mahakama.

Hata hivyo katika siku za karibuni wanaharakati wamekuwa wakishinikiza Serikali ikubali mfumo huo kwani tayari kuna uamuzi wa Mahakama wa kuuruhusu, hata kama Mahakama ya Rufaa itakuwa bado haijatoa uamuzi kwa suala hilo.

Tuesday, February 23, 2010

Kikwete apewa nafasi kubwa kushinda uchaguzi 2010

RAIS Jakaya Kikwete amepewa nafasi kubwa ya kushinda Urais katika uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika mwaka huu kwa kuwa wananchi wanampa nafasi kubwa ya kuwashinda wapinzani wake watakaojitokeza kuwania kwenda Ikulu.

Utafiti uliofanywa na kampuni ya Synovate umebainisha kuwa, utendaji wa Kikwete unawaridhisha wananchi kwa asilimia 75.

Wananchi pia wamesema, chama cha siasa ambacho kipo karibu zaidi na wananchi ni Chama Cha Mapinduzi(CCM).

Kwa mujibu wa wananchi hao, CCM ipo karibu na wananchi kwa asilimia 70, Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kwa asilimia 17, Chama Cha Wananchi(CUF) kwa asilimia 9, NCCR Mageuzi kwa asilimia 2,Tanzania Labour(TLP) na UDP asilimia 1.

Kwa mujibu wa taarifa ya utafiti ya kura ya maoni ya robo ya mwisho Oktoba- Desemba mwaka jana iliyofanywa na kampuni hiyo, lengo lilikuwa ni kupata kura ya maoni ya watanzania katika mambo ya kijamii, kisiasa na kiuchumi katika vipindi tofauti ndani ya mwaka.

Meneja wa Utafiti wa Vyombo vya Habari na Umma wa kampuni hiyo, Abdallah Gunda, amewaeleza waandishi wa habari kuwa, kampuni hiyo ambayo zamani ilijulikana kwa jina la Steadman Group ilikusanya maoni kwa kuwahoji watu 2000.

Amesema, watu hao waligawanywa sawasawa na uwiano wa idadi ya wananchi wa Tanzania na ilikusanya mahojiano ya uso kwa uso katika maeneo tofauti yaliyochaguliwa.

Kwa mujibu wa taarifa hiyo,watu hao walipoulizwa ni Rais yupi wangependa awe kwa mwaka 2010, walimchagua Kikwete kwa asilimia 75.

Kikwete alifuatiwa na Freeman Mbowe kwa asilimia 10, Profesa Ibrahim Lipumba alipata kura kwa asilimia 9, John Cheyo, Salim Ahmed Salim na Zitto Kabwe ambao walipata asilimia 1.

Mbunge aliyefanya vema kwa kipindi hicho cha mwisho wa mwaka 2009 ni Zitto Kabwe kwa asilimia 31, Anne Kilango Malecela asilimia 13, Dr. Wilbroad Slaa asilimia 7, Dr. Harrison Mwakyembe asilimia 6, John Magufuli asilimia 3, Lawrence Masha asilimia 2.

Wabunge wengine ni Mizengo Pinda, Mohamed Dewji, Lucas Selelii, Samuel Sitta, John Cheyo, John Nchimbi, Halima Mdee, Jenista Mhagama, Philemon Ndesamburo, Hamad Rashid Mohamed, David Mathayo, Mark Mwandosya na Hamis Kagasheki ambao wote wamepata kura za maoni kwa asilimia 1.

Kwa mujibu wa ripoti hiyo,zaidi ya robo tatu ya watanzania wanaamini kwamba Tanzania ni nchi yenye demokrasia, asilimia 57 kati yao wanaamini kwamba yapo matatizo madogo madogo.

Asilimia 21 ya waliohojiwa wamesema, Tanzania ipo demokrasia kamili, demokrasia yenye matatizo makubwa asilimia 15 wakati asilimia 3 ya wananchi walidai kwamba nchi haina demokrasia.

Wananchi walipoulizwa endapo uchaguzi ungeitishwa kesho ni wangapi wangepiga kura asilimia 94 walidai wangepiga kura, na asilimia 5 walisema wasingepiga kura.

Asilimia 69 walidai wamechoshwa na siasa, asilimia 9 walisema hawajajiandikisha, asilimia 7 ya wananchi walisema wagombea hawawasaidii.

Gunda amesema, katika utafiti huo walipita mikoa ya Mwanza, Shinyanga, Mbeya,Kagera, Dar es Salaam, Kigoma, Zanzibar, Tanga, Morogoro, Tabora, Iringa, Dodoma, Kilimanjaro, Arusha, Mtwara, Mara, Singida, Rukwa, Manyara, Ruvuma, Pwani, Lindi na Pemba.

Aidha alisema kuwa waliwahoji wanaume kwa asilimia 54 na wanawake asilimia 46,waliwagawa katika matabaka manne kuanzia umri wa mika 18-27 asilimia 39 walihojiwa, 28-37 asilimia 32, 38-47 asilimia 16 na miaka 48 na kuendelea walihojiwa asilimia 14.

Pia alisema kuwa watu 100 walishiriki kufanya mahojiano na kwamba,walikuwa wamepatiwa mafunzo.

Naibu Waziri asafishwa kashfa ya vyeti feki

TUME ya Vyuo Vikuu (TCU) imemsafisha Naibu Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika, Dk David Mathayo kwa kuvitambua vyeti vyake vya shahada ya kwanza ya mifugo, shahada ya uzamili ya kilimo na sayansi pamoja na udaktari wa falsafa.

Dk Mathayo amesema, uamuzi huo ni ahueni kwa kwa kuwa jila lake lilichafuliwa sasa limesafishwa.

Kiongozi huyo wa Serikali amesema, uvumi kwamba anatumia vyeti feki ulikuwa ni uzushi wa kumuonea.

Kwa mujibu wa barua ya tume hiyo iliyosainiwa na Katibu Mtendaji wa TCU, Profesa Mayunga Nkunya, na kutumwa kwa Dk Mathayo, vyeti hivyo vimethibitishwa na kutambuliwa rasmi na tume hiyo kuwa ni sahihi. Dk Mathayo aliwasilisha vyeti hivyo TCU Februari 12 mwaka huu,

“Kwa kutumia mamlaka tuliyopewa kupitia vifungu vya Sheria ya Tume ya Vyuo Vikuu, tunathibitisha kutambua vyeti vyako vya elimu, kuanzia shahada, Shahada ya uzamili na udaktari wa falsafa kuwa vimetolewa na vyuo pamoja na taasisi za elimu zinazotambuliwa,” amesema Profesa Nkunya katika barua hiyo.

Tuna nakala ya barua hiyo ya kumsafisha Dk Mathayo huyo, nakala imepelekwa kwa Spika wa Bunge la Tanzania, Samuel Sitta, Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, na Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Profesa Jumanne Maghembe.

“Mimi kwa sasa sina la kusema zaidi ya kumshukuru Mungu na nimefurahi kwa kweli, masuala mengine nitayazungumza siku nyingine ila leo nimepata ahueni,” amesema Dk Mathayo.

Profesa Nkunya hakupatikana ili athibitishe taarifa kuhusu barua hiyo,wasaidizi wake wa karibu wamedai kuwa amesafiri. Ofisa Uhusiano wa TCU, Edward Mkaku, hakutaka kuzungumzia suala hilo.

Katika mkutano wa 18 wa Bunge uliomalizika hivi karibuni mjini Dodoma, Spika Sitta alitangaza bungeni kuwa vyeti vya Dk Mathayo vimethibitishwa kuwa ni sahihi na vinatambulika.

Dk Mathayo pamoja na mawaziri wengine sita walituhumiwa kughushi sifa za taaluma na kuzitumia kujipatia nyadhifa mbalimbali za kisiasa.

Taarifa za uhakikiwa vyeti vya mawaziri kadhaa wanaotuhumiwa kuwa na vyeti vya kughushi hazijatolewa.

Mawaziri hao ni Waziri wa Viwanda, Biashara na Masoko, Dk Mary Nagu, Naibu Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Dk John Nchimbi, na Naibu Waziri wa Kazi, Ajira na Maendeleo ya Vijana Dk Makongoro Mahanga.

Wengine ni Waziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki,Dk. Diodurus Kamala,Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam ambaye pia ni Mbunge wa Issmani, William Lukuvi,Mbunge wa Lupa(CCM),Victor Mwambalaswa,na Mbunge wa Busega (CCM)Dk. Raphael Chegeni.

Monday, February 22, 2010

‘Chokochoko dhidi ya Bunge ni uchochezi’

MABALOZI wa amani waliounda umoja ujulikanao kama Amani Forum wamewakosoa wanaharakati wanaoandaa maandamano dhidi ya Bunge kwa kusema kitendo hicho ni choko choko zinazoashiria uvunjifu wa amani unaofanywa na watu wenye maslahi binafsi.


Mwenyekiti wa Chama cha Tanzania Labour (TLP), Augustine Mrema ambaye ni mmoja wa wajumbe pamoja na Katibu wa Umoja huo, Risasi Mwaulanga wameliambia gazeti hili kwamba kesho watahutubia mkutano wa hadhara katika viwanja vya Mwembe Yanga, Temeke, waliouandaa ambao pamoja na masuala mengine, wamesema wataufafanulia umma madhara ya tamko la wanaharakati hao dhidi ya bunge.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti na gazeti hili, mabalozi wa Amani Forum ambayo Mwenyekiti wake ni Mbunge wa Afrika Mashariki, Dk Walid Kabourou, Mrema na Mwaulanga walisema tamko hilo la wanaharakati ni miongoni mwa viashiria ambavyo vimeanza kuonekana yakiwemo maneno ya chini chini ya kuvunja amani ya nchi.

Katibu wa Amani Forum, Mwaulanga alisema katika mkutano wa hadhara wa kesho ambao ni wa kwanza kufanyika tangu umoja huo uzinduliwe rasmi mwezi uliopita, mabalozi hao wamesema watahakikisha wanaueleza umma pia athari za maneno ya chini chini ambayo yamekuwa yakijitokeza kuhusu masuala ya dini.

Mwaulanga alisema wanaharakati na vyama vya siasa, vimekuwa vikitoa mfano wa Marekani katika harakati zao lakini vikishindwa kubaini kwamba wao hufanya mambo kwa maslahi ya nchi na maendeleo.

Alisema katika kuhakikisha kuwa umma unaelewa ukweli wa mambo juu ya suala zima la kulinda amani, Amani Forum mwezi ujao itafanya mikutano mingine miwili Dar es Salaam katika maeneo ya Manzese na Buguruni kabla ya kuhamia kwenye mikoa aliyoitaja kwamba ni yenye utata.

Aliitaja mikoa hiyo kuwa ni Mara, Arusha, Mwanza, Mbeya na ya Kusini. “Uamuzi wa wanaharakati hauna chochote zaidi ya kujenga hisia za chuki na wananchi kutoiamini serikali na bunge lao,” alisema Mwaulanga na kusisitiza kwamba badala ya kuandamana, wangekwenda kujipanga wachaguliwe wabunge wanaoendana na matakwa wanayohitaji na si kuandaa maandamano nchi nzima.

Mwaulanga ambaye maoni yake yaliungwa mkono na Mwenyekiti wa TLP, Mrema, alisema kupitia wanaharakati, wanaweza kujipitisha watu wengine wenye malengo maalumu ya kiuchumi au kisiasa wakapitisha maazimio kwa wananchi yanayoweza kuiingiza nchi kwenye mgogoro.

Katibu huyo wa mabalozi wa amani ambaye alisema mkutano wa kesho utazungumzia pia mauaji mkoani Mara, alisema wanaharakati walipaswa waandamane kupinga ukatili kama uliojitokeza hivi karibuni wa watu 17 wa ukoo mmoja kuuawa katika Kijiji cha Buhare, Mara na si kujielekeza kwenye mambo ya kisiasa.

“Umeona hizi taasisi zisizo za kiserikali, zimetangaza maandamano yasiyoisha nchi nzima. Sasa yale maandamano ingawa yanaweza kudaiwa ni dhidi ya bunge, si wangeyafanyia Dodoma bunge linapokuwa pale.

Lakini unaposema ni maandamano nchi nzima, ni dalili kwamba yanapinga serikali nzima,” alisema Mrema. Mrema alisema, “ukishasema maandamano ni nchi nzima, ni dhahiri polisi itakataa. Wakishakataa si dalili ya mgogoro umeanza.

Soma zaidi

Mizengo Pinda ambeba Rostam Aziz


WAZIRI Mkuu Mizengo Kayanza Peter Pinda amewashauri wananchi wa Jimbo la Igunga mkoani Tabora wasimkatae Mbunge wao Rostam Aziz wakati wa uchaguzi mkuu ujao kwa kusikia maneno yanayosemwa bungeni, badala yake wazingatie kile alichowafanyia.

Wakati Pinda anampigia debe Mbunge huyo jana kwenye mkutano wa hadhara katika uwanja wa Kumbukumbu ya Sokoine, baadhi ya wananchi wa jimbo hilo walimwomba Waziri Mkuu amshinikize Mbunge wao abaki jimboni humo, kwa madai kuwa haonekani.

Wananchi hao walitoa ombi hilo ili waweze kupata fursa ya kumweleza kero zao na awaeleze yanayosemwa bungeni kuhusu yeye (Rostam).

Mmoja wa wananchi aliyejitambulisha kwa jina la Moka Changalawe alimweleza Pinda kuwa kukosekana kwa Mbunge jimboni kwa muda mrefu kumesababisha baadhi ya viongozi kuwanyanyasa wananchi kwa kuwabambikia kesi za uongo, zikiwemo kutishia kuua.

Hata hivyo, Pinda katika hotuba yake, alisema kama kuna manyanyaso na ubabe kwenye halmashauri hiyo, ni vitendo vya kuchochea rushwa na serikali imejipanga kuondoa tatizo hilo.

Hata hivyo hakujibu ombi la wananchi hao la kumwomba Mbunge huyo kubaki jimboni humo. Pinda juzi mara baada ya kuwasili mjini hapa alizungumza na watendaji wa halmashauri ya wilaya ya Igunga na kuwaomba wasimkatae Mbunge huyo.

“Tunaelekea katika uchaguzi mkuu ujao baadaye mwaka huu. Naomba mtakapokuwa mnachagua viongozi wenu mzingatie wamewafanyia nini iwe ni katika nafasi ya udiwani au ubunge.

“Iwapo mnataka kumchagua tena Rostam zingatieni amewafanyia nini katika ubunge wake. Msisikilize kile kinachosemwa bungeni juu yake. Bunge lina mambo yake, mimi kama Waziri Mkuu nafahamu mambo ya pale bungeni,” alisema Waziri Mkuu.

Alisema iwapo wananchi wa Igunga wanaridhishwa na namna Mbunge wao anavyowatatulia matatizo yao ya kimsingi wana hiari ya kumchagua tena kuendelea kuwa Mbunge bila kusikiliza nini kinasemwa juu yake.

Ingawa Waziri Mkuu hakufafanua zaidi ni maneno gani ya bungeni ambayo yamekuwa yakisemwa juu ya mbunge huyo, Rostam ni miongoni mwa wabunge ambao wamekuwa wakihusishwa na kampuni ya Richmond iliyoingia mkataba tata na Shirika la Umeme (Tanesco).

Wakati wa kuhitimisha mjadala bungeni juu ya suala la Richmond katika mkutano wa 18 wa Bunge ulioahirishwa hivi karibuni mjini Dodoma, Spika Samuel Sitta alisema suala hilo limekwisha isipokuwa amebakiwa na kazi ya kumsihi Rostam aachane na mawazo ya kutaka liundwe jopo la majaji kuichunguza ripoti ya kamati teule iliyochunguza na kuwasilisha bungeni taarifa ya Richmond.

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu alionya tabia ya viongozi kujenga uhasama baina yao kwamba hatua hiyo inawafanya kutumia muda mwingi katika kugombana badala ya kuwatumikia Watanzania masikini.

Alisema serikali haitavumilia kuona viongozi wanatumia muda mwingi katika ugomvi wakati Watanzania wanakabiliwa na matatizo mbalimbali ukiwewo umasikini.

“ Kama kweli tunataka kuwahudumia wananchi masikini hawa ni lazima tuwe na ushirikiano sisi viongozi kwanza. Idadi yetu sisi Watanzania ni kama milioni 40 hivi au na zaidi kidogo. Hata hivyo asilimia 80 ni wakulima na asilimia 20 ndio sisi viongozi.

“Iwapo sisi asilimia 20 tutajali zaidi maslahi yetu na kuwasahau hawa masikini ipo siku hawa watu watatupiga marungu,” alisema Waziri Mkuu.

Alisema viongozi wa serikali wanawajibika kutumia fedha wanazozipata katika kuwasaidia masikini wanaowaongoza badala ya kujilimbikizia fedha huku wakizungukwa na watu masikini jambo ambalo ni hatari.

Friday, February 19, 2010

CCM: Ruksa kumvaa Kikwete


-Wanaotaka urais fomu Julai Mosi
-Za ubunge Julai 23
-Mgombea urais Z'bar kutajwa Julai 16

VIGOGO wa Chama cha Mapinduzi (CCM) wenye ubavu wa kumvaa Mwenyekiti wa chama hicho, Rais Jakaya Kikwete katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka huu, wataanza kujulikana Julai Mosi, mwaka huu, takriban siku 23 kabla ya kuvunjwa rasmi kwa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, imeelezwa wiki hii mjini Dodoma.

Wagombea hao wa urais watatakiwa kuchukua fomu na kuzirejesha siku saba baadaye, yaani Julai 8 mwaka huu na majina yao yatafikishwa kwenye Mkutano Mkuu wa CCM, Julai 18, mjini Dodoma, kwa ajili ya uteuzi, ikiwa ni siku mbili baadaye, baada ya mgombea urais wa Zanzibar kuteuliwa na Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC).

Mteule wa kugombea urais Zanzibar tofauti na urais wa Jamhuri, hutangazwa na NEC ambayo safari hii katika kumpata Rais wa saba wa Zanzibar, itafanya kazi hiyo Julai 16, 2010.

Katika nafasi za kugombea urais wa Muungano ni Mbunge wa Maswa pekee, John Shibuda ndiye aliyetangaza nia ya kutaka nafasi hiyo na kwa upande wa urais wa Zanzibar, viongozi kadhaa wanatajwa akiwamo Makamu wa Rais, Dk. Ali Mohammed Shein, Waziri Kiongozi Shamshi Vuai Nahodha na Naibu Waziri wa Afrika Mashariki, Mohamed Aboud Mohamed.

Wengine wanaotajwa kuwania kuongoza Visiwani ni Naibu Waziri Kiongozi, Juma Shamuhuna, Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Dk. Hussein Mwinyi, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-Muungano, Muhammed Seif Khatibu na aliyekuwa Waziri Kiongozi, Dk. Gharib Bilali.

Kwa upande wa Bunge, litavunjwa rasmi Julai 23, mwaka huu takriban miezi mitano ijayo, mapema zaidi kuliko ilivyokuwa ikifanyika awali.

Wakati Bunge hilo likivunjwa Julai 23, wabunge wa CCM wenye kutaka kutetea nafasi zao watapaswa kuchukua fomu kwenye chama chao siku tatu baada ya Bunge kuvunjwa, yaani Julai 26 na kulazimika kurejesha fomu hizo siku mbili baadaye, yaani Julai 28.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa saa nane usiku wa kuamkia Jumanne, wiki hii, mjini Dodoma na Katibu wa NEC- Itikadi na Uenezi, Kapteni mstaafu John Chiligati, siku hizo za uchukuaji na urejeshaji fomu kwa wanaotaka kuwania ubunge kwa tiketi ya CCM zinawahusu pia wagombea wa ujumbe wa Baraza la Wawakilishi Zanzibar.

Akizungumzia kuhusu madiwani, Chiligati aliwaambia waandishi wa habari kuwa wagombea watachukua fomu Julai 10 na kuzirudisha Julai 14 na kwamba kuanzia Julai 31 hadi Agosti 7, ni siku za wagombea ubunge, uwakilishi-Zanzibar na udiwani kufanya kampeni kwenye matawi ya chama hicho.

“Watapiga kura za maoni katika matawi yote nchini Agosti 8, kwa wagombea wote wa ubunge, uwakilishi na udiwani.

Akifafanua kuhusu kura za maoni, alisema NEC imehimiza kila wanachama wa CCM kujiorodhesha kwenye daftari la wanachama katika tawi lake na mwisho wa kujiorodhesha ni Julai 30, mwaka huu na baada ya hapo upokeaji wanachama wapya utasitishwa hadi mchakato wa kura za maoni uhitimishwe.

“Watakaopiga kura za maoni ni wale tu watakaokuwa wamejiandikisha kwenye daftari katika tawi,” alisema Chiligati na kuongeza kuwa wagombea wote wa ubunge bila kujali nyadhifa zao za sasa watatembezwa wakati wa kuomba ridhaa kwa wanachama kwa kutumia magari ya chama yatakayokodiwa na watakula chakula kilichoandaliwa na chama.

“Hatutaki mtu ashindwe kugombea au kufanya kampeni za kuomba kura za maoni kwa kuwa hana gari kama mwingine, hana pikipiki au baiskeli. Wote watatumia usafiri wa chama, chakula cha chama na watazunguka pamoja, katika kila tawi ambako kila mmoja atajieleza,” alisema Chiligati.

Katika hatua nyingine, NEC imekata mzizi wa fitina na hasa malumbano yaliyoanzia katika Umoja wa Wanawake (UWT) wa chama hicho wa kutaka Wabunge wa Viti Maalumu waliokaa kwa mihula zaidi ya miwili kuachia nafasi hizo ama wakagombee kwenye majimbo au wajiengue kabisa kwenye ubunge.

Katika uamuzi wake wa sasa, NEC imekubali Viti Maalumu iwe na ukomo wa mihula miwili lakini utaratibu huo utaanza rasmi kutumika mwaka 2015, ili wahusika wa sasa wajiandae, ikiwa ni kinyume na alivyotarajia Mwenyekiti wa UWT, Sophia Simba, aliyekuwa akipigania utaratibu huo uanze, katika uchaguzi wa mwaka huu.

Thursday, February 18, 2010

Mkapa: Kuna mtu kanizomea?

RAIS mstaafu wa Serikali ya Awamu ya Tatu, Benjamin Mkapa, amesema, hakuna Mtanzania anayeweza kudiriki kumzomea kwa kuwa rekodi ya utendaji wake kitaifa na kimataifa inaendelea kumlinda.

Mkapa amelakiwa kwa kishindo katika ziara ya siku moja wilayani Kilolo mkoani Iringa.

“Mmeona mapokezi yangu, kuna mtu yeyote amenizomea? Sijifichi na wala sikimbii kuzomewa, mimi niko ‘busy’ sana na shughuli za kimataifa baada ya kumaliza utumishi wangu serikalini,” amesema Mkapa.

Ameyasema hayo jana alipozungumza na wadau wanaonufaika na taasisi yake ya Benjamin William Mkapa HIV/AIDS Foundation wilayani hapa.

Alizungumza wakati wa majadiliano kuhusu hali ya Ukimwi nchini yaliyofanyika katika Ukumbi wa Hospitali Teule ya Wilaya hiyo iliyopo Ilula.

Mkapa amesema, baada ya kumaliza urais wake amekuwa akijihusisha na shughuli mbalimbali za kimataifa zinazomfanya awe safarini muda mwingi akishughulikia uhusiano na ushirikiano baina ya Tanzania na nchi nyingine; mambo yanayohusu kumbukumbu ya Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere na kuimarisha taasisi yake ili ishiriki vizuri zaidi katika mapambano ya Ukimwi unaotishia ustawi wa watu na taifa.

Amesema, wanaoishi na Virusi Vinavyosababisha Ukimwi (VVU) ni sehemu ya mapambano ya Ukimwi na hivyo wasiwe na hofu,wajiamini na waape kuishi maisha kama wengine.

Mkapa amesema, nchi inayoendelea ambayo nguvu kazi yake inapungua siku hadi siku kutokana na janga hilo, itakuwa ndoto kwake kupiga hatua za maendeleo.

“Ili tupambane vizuri na janga hili ni lazima tuwe tayari sasa kama nchi kubeba sehemu ya mzigo wa mapambano unaobebwa na wafadhili mbalimbali duniani kwasababu itafika siku watachoka,” amesema Mkapa.

Wednesday, February 17, 2010

TAMKO LA FemAct NA MASHIRIKA MENGINE YA KIRAIA KUHUSU KUTORIDHISHWA NA KIWANGO CHA UTENDAJI WA BUNGE LA TANZANIA KATIKA MKUTANO WAKE WA 18

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
LEO, FEBRUARI 17, 2010


Sisi Muungano wa Asasi za Kiraia zinazotetea Usawa wa jinsia, haki za binadamu, maendeleo na ukombozi wa wanawake kimapinduzi (FemAct) pamoja na asasi zingine za kiraia tumekuwa tukifanya kazi kwa karibu na wabunge na Bunge la Tanzania kwa muda mrefu sasa. Tunatambua jitihada za muda mrefu za baadhi ya Wabunge pamoja na Bunge kwa ujumla katika kutetea haki na maslahi ya wananchi wa Tanzania. Tulifika hatua ya kuanza kuamini kwamba ukombozi wa Mtanzania unaweza kuletwa kupitia Bungeni.

Katika mkutano wa 18, Bunge lilikuwa litekeleze majukumu kadhaa ikiwa ni pamoja na kupata taarifa ya serikali kuhusu utekelezaji wa maazimio 23 ya Bunge ya kashfa ya manunuzi ya kitapeli ya mitambo ya kufua umeme wa dharura ya Richmond LLC, mkataba mbovu wa ubinafsishaji wa Mgodi wa makaa ya mawe Kiwira, ukodishaji wa bandari kwa kampuni ya TICTS na mkataba mbovu wa ukodishaji reli ya kati (TRL). Mengine ni Bunge kupokea na kujadili taarifa ya kamati ya Bunge kuhusu uchafuzi wa mazingira na ukiuakaji wa haki za Binadamu mgodi wa North Mara na ukiukwaji wa haki za binadamu eneo la Loliondo wilaya ya Ngorongoro.

Mkutano huo wa 18 wa Bunge ulimalizika Ijumaa tarehe 12 Februari 2010. Tofauti na matarajio ya wananchi, Bunge limemaliza kikao chake bila ya kuchukua hatua madhubuti juu ya kashfa za Richmond, Kiwira, TICTS, TRL, Loliondo na North Mara. Jambo hili limetushtua na kutusikitisha sana. Tulitarajia Bunge kutimiza wajibu wa mamlaka na kazi za Bunge kama inavyoelezwa katika Katiba Ibara ya 63 (2 ), inasema;

“Sehemu ya pili ya bunge itakuwa ndicho chombo kikuu cha Jamhuri ya Muungano ambacho kitakuwa na madaraka kwa niaba ya mwananchi, kuisimamia na kuishauri serikali ya jamhuri ya muungano na vyombo vyake vyote katika utekelezaji wa majukumu yake kwa mujibu wa katiba hii ”.

Sisi wananchi tunaona kuwa Bunge limeshindwa kutekeleza wajibu wake wa kikatiba wa kuisimamia serikali, kutokana na mfumo mbaya wa madaraka na uwajibikaji kati ya serikali na bunge ambao unaruhusu maslahi ya chama tawala chukua hatamu kuliko maslahi ya wananchi wengi na taifa kwa ujumla. Wananchi wengi kupitia taasisi mbalimbali wameshatoa hoja kuhusu umuhimu wa kubadilisha huu mfumo huu mbaya wa utawala na utamaduni wa kisiasa unaolimbikiza madaraka kwa watawala na kuvuruga mgawanyo wa madaraka na uwajibikaji. Mapendekezo kadhaa yalikwishatolewa kiwa ni pamoja na kutenga baraza la mawaziri lisitokane na wabunge. Mfumo huu umedhoofisha demokrasia shirikishi ambayo ingewezesha wananchi na makundi yao kuwa na uwezo wa kuliwajibisha bunge,wabunge na madiwani. Aidha mfumo huu unalimbikiza madaraka katika serikali kuu na kudhoofisha uwezo wa madaraka kwenye serikali za mitaa ambako ndiko kwenye wananchi walio wengi.

Katika muktadha wa mfumo unaolimbikiza madaraka kwa walio wachache na kuvuruga uwajibikaji, ni vigumu kwa bunge kuiwajibisha serikali kama inavyotegemewa na wananchi walio wengi. Ndio maana bunge limefunika kisiasa kashfa za Richmond, Kiwira, TRL, na TICTS ingawakashfa hizi zimelisababishia taifa letu hasara kubwa ya mabilioni ya fedha na madhara makubwa kwa wananchi ikiwa ni pamoja na kuwafanya wawe maskini na fukara zaidi.

Mabilioni ya fedha ya wananchi zilizopotea zingeweza kutumika kuboresha hali za wananchi. Kwa mfano;

oFedha zilizopotea katika kashfa ya Richmond ni shilingi bilioni 173 Kiasi hicho kingeweza kujenga nyumba 19,211 za walimu wa shule za msingi nchi nzima kwa gharama ya shilingi milioni tisa(9) kwa kila nyumba. Mpango wa Pili wa Maendeleo ya Elimu ya Msingi (MMEM II 2007-2011) ulipanga kutumia sh bilioni 153 kwa ujenzi wa nyumba za walimu. Kwa hiyo fedha zilizopotea katika kashfa ya Richmond zingetosha na kubaki kujenga nyumba zote za walimu wa shule ya msingi kulingana na mahitaji yaliyopangwa na MMEM II ili kuboresha elimu ya msingi katika shule za umma nchini. Mpaka sasa serikali imeweza kutoa asilimia tatu (3%) tu ya fedha za ujenzi wa nyumba za walimu kiasi ambacho hakizidi shilingi bilioni tano.

oKiasi cha fedha kilichopotea katika kashfa ya Richmond, kingeweza kuwapatia chakula cha mchana wanafunzi 5,242,424 kwa Mwaka mzima kwa kasma ya shilingi 33,000 kwa Mwaka kama ilivyokadiriwa na mpango wa chakula duniani. Taifa lingeweza kuepusha mimba za utotoni mashuleni ambazo baadhi zinachangiwa na ukosefu wa chakula kwa wanafunzi mashuleni.

oKiasi hicho kingeweza kujenga zahahati zaidi ya 1,700 kwa gharama ya shilingi millioni 100 kwa kila moja na kuboresha huduma ya afya kwa wananchi vijijini na kwa makundi ya watoto, wazee na watu wenye ulemavu na kuepusha vifo vya wanawake katika uzazi ambao kwa sasa takribani wanawake ishirini na nne hupoteza maisha kila siku kutokana na sababu za uzazi.

Ni dhahiri kuwa mfumo wa utawala uliopo haukidhi haja ya kusimamia rasilimali za nchi yetu na kuwajibisha watawala kwa wananchi. Hivyo tunatoa wito kwa wananchi kutambua kuwa Tanzania sasa inahitaji mapinduzi makubwa na ya haraka katika mfumo wa uwajibikaji na uongozi na, muundo wa sera za utawala, siasa na uchumi. Uchaguzi Mkuu wa 2010 ni fursa pekee kwa wananchi kufanya mapinduzi yanayotarajiwa; kuchagua watu waadilifu na wanaoweka mbele maslahi ya taifa na wananchi. Wabunge wetu wa sasa wameshindwa kutetea na kulinda haki na maslahi ya taifa na wananchi.

Ni kutokana na haya tunayoyabaini, FemAct na Mitandao mingine tunapendekeza na kudai yafuatayo:

1)Bunge lijisafishe na kuanza kuangalia na kuweka maslahi ya taifa kuliko maslahi ya vyama na wabunge binafsi kutokana na kuogopa kutopitishwa na vyama vyao kugombea nafasi za ubunge majimboni.

2)Serikali iharakishe kuweka mazingira ya kuruhusu wagombea binafsi katika nafasi mbali mbali za uongozi wa kisiasa katika ngazi zote za utawala;
3)Mwaka huu wa uchaguzi mkuu, kila mpiga kura awe makini na kuchagua wagombea waadilifu na wasio wabinafsi ili kupata bunge litakalokuwa na uwezo wa kusimamia serikali na kutunga sheria kwa kuzingatia maslahi ya taifa

4)Wananchi kutambua kuwa wao ndio wana wajibu wa kuchagua wabunge wenye uwezo wa kuisimamia serikali ili iweze kuwachukulia hatua kali viongozi na watumishi wote wa umma ambao wanafanya ufisadi unaosababisha taifa kupoteza mabilioni ya fedha. Hivyo ni vema wananchi wakati wa uchaguzi wakaepuka kudanganyika kwa rushwa na hongo kama fulana,kanga, kofia, na vyakula, kwani kumpa mtu kura yako kwa rushwa ni kuweka rehani maendeleo yako na taifa.

5)Wasomi na matajiri wazalendo wajitolee kuchangia mawazo na maono mapya pamoja na rasilimali za kuwezesha mapinduzi na ukombozi wa wananchi dhidi ya ujinga, maradhi, umaskini na unyonge; na

6)Vyombo vya habari na makundi ya vuguvugu la mapinduzi ya jamii, kwa pamoja, waongoze mapinduzi mapya nchini Tanzania ili kuwe na uwajibikaji utakaoweza kubadilisha maisha ya wananchi kijamii na kiuchumi.

Aidha, sisi kwa pamoja kama Asasi za Kiraia tumeamua kuchukua hatua zifuatazo;
(a)Kuandaa maandamano makubwa ya kitaifa kuonyesha kutoridhishwa na utendaji usioridhisha wa Bunge la sasa na kudai mfumo mbadala wa demokrasia shirikishi ambao una uwezo zaidi katika kutetea maslahi ya wananchi
(b)Kutoa elimu ya uraia kwa wananchi ili waweze kutambua mamlaka walioyo nayo katika kuwachagua na kuwafanya wabunge na viongozi kujali maslahi ya taifa na wananchi.
Mungu ibariki Tanzania

Imetolewa na kusainiwa na

1. FEMINIST ACTIVIST COALITION (FemAct)
2. CHAMA CHA WALEMAVU TANZANIA (CHAWATA)
3. TANZANIA NETWORK OF LEGAL AID PROVIDERS (TANLAP)
4. SAHRINGON TANAZANIA CHAPTER
5. MEDIA COUNCIL OF TANZANIA (MCT)
6. MTANDAO WA WAFUGAJI
7. TANZANIA COALITION ON DEBT AND DEVELOPMENT (TCDD)

17 Februari 2010

Kambi za Lowassa, Sitta zadaiwa kuipasua CCM

Makamu Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Bara, Pius Msekwa amesema, semi zenye maudhui ya upatanishi zilitumiwa na Kamati ya Rais mstaafu, Ali Hassan Mwinyi kuzipatanisha kambi mbili za wabunge wa CCM zilizosigana ndani ya Bunge kwa muda mrefu.

Amezitaja kambi hizo kuwa ni ile iliyokuwa ikiongozwa na Spika wa Bunge, Samuel Sitta na ya Waziri Mkuu aliyejiuzulu, Edward Lowassa.

Msekwa amewaeleza waandishi wa habari mjini Dodoma kuwa,Kamati ya Mwinyi imefanya kazi nzuri ya kutafuta kiini cha mpasuko miongoni mwa wabunge wa CCM ndani ya Bunge kama ilivyotumwa na Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) ya chama hicho.

Amesema,Kamati ya Mwinyi ilikutana na wabunge wa CCM kwa siku nne mfululizo kuanzia Novemba mosi hadi Novemba nne, mwaka jana mjini Dodoma na kuzungumza nao ili kudadisi kiini cha mpasuko baina yao bungeni.

Kutokana na maelezo ya wabunge hao wa CCM, Kamati ya Mwinyi ilibaini kuwa kulikuwa na makundi, la Lowassa na la Sitta, chanzo kikiwa ni hofu kutoka kila upande kuwa mwenzake ana mpango wa kumng’oa.

“Kutokana na maelezo yao, ilionekana kuwa uhasama hasa ulianza baada ya ripoti ya Richmond kuwasilishwa bungeni ambapo yaliibuka makundi hayo mawili yaliyoanza kushambuliana, kundi moja likiitwa la mafisadi na lingine likijiita la upambanaji dhidi ya ufisadi,” amesema Msekwa.

Msekwa amesema,kutokana na malumbano hayo, kila kundi liliingiwa na hofu kuhusu kundi lingine kuendesha mikakati ya chini chini ya kuwaondoa wenzao madarakani.

“Hawa wanaodai kupambana na ufisadi walianza kulalamika kuwa kundi la mafisadi lilikuwa linawatumia watu ili kuwang’oa katika ubunge kwa kumwaga mabilioni ya fedha kwa watu hao na kundi la pili lilikuwa likilalamika kwa kubatizwa jina la mafisadi, jina ambalo kimsingi linamaanisha rushwa, jambo ambalo ni kosa kisheria,” alisema.

Msekwa amesema,baada ya kubaini hilo, Kamati ilizungumza na kila kundi kwa nyakati tofauti kujadili namna nzuri ya kuondoa tofauti baina yao.

“Kimsingi hali sasa ni shwari, lakini bado ipo kazi ambayo imebakia na tumeiomba NEC ituongeze muda ili tuifanye, nayo ni ya kukutanisha makundi hayo na vinara wao (Sitta na Lowassa) ili wote watoe madukuduku yao mbele ya wenzao na kuhitimisha uhasama. Kazi hii tutaifanya karibuni na tutaleta taarifa katika kikao cha NEC mwezi ujao,” alisema Msekwa.

Amesema,Kamati ilibaini kuwa malumbano hayo yalipamba moto zaidi kutokana na Kamati ya Wabunge wa CCM kutofanya vikao kama kanuni zinavyoelekeza na hivyo wabunge kuligeuza Bunge kuwa sehemu ya kushambuliana badala ya kutumia vikao vya Kamati ya Wabunge wa CCM.

Alisema Kamati ilipochunguza kama kulikuwa na uendeshaji mbovu wa shughuli za Bunge chini ya Spika Sitta na kuwa chanzo cha malumbano hayo, Kamati hiyo ikiwajumuisha watalaamu wa zamani wa uspika (Msekwa-Spika Bunge la Tanzania na Abdulrahman Kinana – Spika Bunge la Afrika Mashariki), ilibaini kuwa Sitta alikuwa akiendesha Bunge kwa kuzingatia kanuni na sheria za Bunge bila kupotosha hata kidogo.

“Hata hivyo wao wenyewe (Wabunge wa CCM) walionesha wasiwasi kuhusu baadhi ya kanuni za Bunge kuwa inawezekana zikachangia malumbano hayo, lakini tuliwaambia kwa kutumia vikao vyao vya Bunge, wanaweza kuziangalia kanuni hizo kuona kama wanaweza kuzirekebisha kwa namna watakavyo bila kuingiliwa,” amesema.

Hata hivyo, alisema ishara iliyoonekana katika kikao cha Bunge kilichopita ambapo wabunge na Sitta walifunga rasmi mjadala wa Richmond ndani ya Bunge bila kushinikizwa, inaonesha kuwa Kamati hiyo imeanza kupata mafanikio makubwa ya kujenga umoja na mshikamano baina ya wanaCCM hao.

Alisema Kamati hiyo pia iliridhishwa na namna wajumbe wa Baraza la Wawakilishi Zanzibar walivyokuwa wakijadili masuala yanayowasilishwa katika Baraza hilo ili kujadiliwa.

Tuesday, February 16, 2010

Vichaa,wafu watumika kuiba bilioni 6.8

MKUU wa Mkoa wa Rukwa, Daniel ole Njoolay, yupo tayari kujiuzulu endapo mamlaka za uteuzi zitamtaka awajibike kutokana na kashfa ya ufisadi wa fedha za ruzuku ya pembejeo za kilimo inayowakabili viongozi mkoani humo.

Njoolay amewaeleza waandishi wa habari kuwa, yupo tayari kujiuzulu ikiwa hana budi kufanya hivyo.

Ametoa msimamo huo baada ya kupokea taarifa ya tume aliyoiunda kuchunguza kashfa ya matumizi mabaya fedha za ruzuku ya pembejeo za kilimo kupitia mfumo wa vocha.

Inadaiwa kuwa,viongozi mkoani humo wametumia visivyo Sh bilioni 6.8,za ruzuku.

“Uongozi wa Mkoa wa Rukwa unaiomba radhi sana serikali kwa kashfa hii iliyotokea mkoani na tutakuwa tayari kuwajibika kisiasa kama hapana budi,” imesema sehemu ya taarifa ya Njoolay aliyoitoa kwa waandishi wa habari.

Taarifa ya tume hiyo ya watu tisa iliyofanya uchunguzi kwa takribani mwezi mmoja, imebainisha kuwa waliohusika na ufisadi huo ni watendaji 43 wa vijiji, mawakala 23, watumishi wanne wa kilimo ambao wote watafikishwa kwenye vyombo vya sheria.

Kwa mujibu wa Njoolay,wenye nyadhifa za kisiasa waliobainika kuhusika na kashfa hiyo wakiwemo madiwani na wakuu wa wilaya watafikishwa kwenye vyama vyao vya kisiasa ili washughulikiwe huko.

Taarifa ya Njoolay imeeleza kuwa, uchunguzi wa tume umebaini mambo mengine kadhaa ikiwa ni pamoja na mkoa, wilaya na vijiji kutokuwa makini kusimamia na kufuatilia kwa karibu usambazaji wa ruzuku ya pembejeo ya kilimo kwa wakulima.

Kwa mujibu wa taarifa hiyo,'wajanja' walitumia mwanya huo wa Serikali kutofuatilia kwa makini kuiibia Serikali mabilioni hayo ya fedha.

Kazi ya kufanya hesabu haijakamilika,lakini kiasi kilichokuwa kimechukuliwa benki ni Sh bilioni 6.8 na kilichobaki ni Sh bilioni 1.6 tu.

Kati ya hizo kiasi kilichotumika vizuri, asilimia 25 zimetumika Sumbawanga, asilimia 30 Nkasi na asilimia 80 80 wilayani Mpanda.

Waliohusika kuiba fedha hizo za Serikali walitumia mbinu kadhaa ikiwa ni pamoja na kughushi sahihi za wakulima, kuandikisha wakulima hewa, wafu, watoto,na vichaa.

Mbinu zingine ni pamoja na kuwahonga wakulima fedha kidogo kati ya Sh 2,000 na 7,000 ili watie saini vocha bila kupata mbolea na pia kuwapatia wakulima idadi ndogo ya mbolea kuliko kiasi halisi walichosainishwa.

Kamati ya Ulinzi na Usalama ya mkoa imeagiza hatua kadhaa zichukuliwe zikiwemo za kuipongeza Wilaya ya Mpanda kwa kusimamia kwa ufanisi suala hili na hatua za kinidhamu zichukuliwe dhidi ya watumishi wa Serikali waliolegalega kufuatilia kwa ukaribu zoezi hili.

Hatua nyingine ni pamoja na mawakala wote na watendaji walioibia Serikali wafikishwe kwenye vyombo vya sheria na tume iendelee na uchunguzi kuwabaini wengine, kuna uwezekano idadi ya watuhumiwa ikaongezeka.

Tume ya kuchunguza uozo huo uliokuwa ukipigiwa kelele na wakulima wengi waliolalamika kukosa pembejeo za kilimo msimu huu, iliundwa Januari 11, mwaka huu na mkuu wa mkoa huyo.

Waziri ndani ya sakata la Muro

-Achunguzwa kwa mahusiano na waliotimuliwa Bagamoyo
WAZIRI Mwandamizi katika serikali ya Rais Jakaya Kikwete, anahusishwa na sakata lililomsibu Mtangazaji wa Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC), Jerry Muro, na sasa uchunguzi dhidi yake unaendelea, Raia Mwema limefahamishwa.

Habari za ndani ya Serikali zimeeleza kwamba vyombo vya dola vimeshitushwa na taarifa za kuhusika kwa waziri huyo ambaye taarifa zake zimekutwa kwa Muro na wenzake wawili Edmud Kapama na Deogratias Mgasa.

Kwa mujibu wa habari hizo, vyombo vya dola vilipowapekua na kuwahoji Muro na wenzake vilipata ushahidi wa waziri huyo kuwa na ‘mahusiano’ na watendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Bagamoyo, waliotimuliwa na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda.

Waliotimuliwa madarakani na Pinda ni Mkurugenzi Mtendaji Rhoda Nsemwa; Mweka Hazina, Michael Karol Wage; Ofisa Kilimo, Mifugo na Ushirika, Naftal Rhemtullah; Ofisa Mipango, Aloyce Gabriel na Mkaguzi wa Ndani, Abdul Mwinyi.

“Jerry Muro na wenzake walikutwa na ushahidi unaoonyesha kwamba waziri (anamtaja jina) alikuwa akinufaika na fedha za ubadhirifu kutoka Halmashauri ya Wilaya ya Bagamoyo. Walikuwa na ushahidi wa gari ambalo Waziri huyo amenunuliwa na liko Morogoro katika sehemu ya biashara zake,” kinaeleza chanzo cha habari serikalini.

Raia Mwema limefahamishwa kwamba vyombo vya dola kwa pamoja sasa vinachunguza jinsi waziri huyo (jina tunalo) alivyonufaika na fedha kutoka halmashauri hiyo ya Bagamoyo na sababu za mmoja wa watumishi hao kutoa fedha kwa waziri huyo.

“Unajua wanaangalia mahusiano kati ya Waziri huyo na mmoja wa watumishi waliofukuzwa kazi na Waziri Mkuu, maana lazima Serikali ijiridhishe walitoa fedha kwake kwa maslahi gani na kama wana mahusiano ya binafsi, kibiashara ama ya kikazi kabla ya kuchukua maamuzi na pia kina Muro na wenzake walizipataje hizo taarifa na walikuwa wanazitumia kwa malengo gani,” anaeleza Ofisa Mwandamizi serikalini.

Mbele ya Hakimu Gabriel Mirumbe wa mahakama ya Hakimu Mkazi ya Kisutu, Jerry Muro na wenzake wawili walishtakiwa kwa pamoja, wiki iliyopita, kwa kuomba rushwa ya shilingi milioni 10 toka kwa Mweka Hazina wa Wilaya ya Bagamoyo, Wage, aliyefukuzwa kazi hivi karibuni na Waziri Mkuu kwa ubadhirifu.

Mwendesha Mashtaka wa Serikali, Boniface Stanslaus akiwa na Mwendesha Mashtaka wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), Benny Lincoln wamedai mahakamani hapo kwamba mshitakiwa wa kwanza na wa pili pia wanakabiliwa na shitaka la kujipachika wadhifa ambao si wao.

Inasemekana January 29, 2010 katika hoteli ya Sea Cliff washtakiwa walijitambulisha mbele ya Wage kuwa wao ni maafisa wa TAKUKURU wakati si kweli.

Mapema mwaka huu, Waziri Mkuu, Pinda, aliwavua madaraka viongozi watendaji hao wakuu wa Halmashauri ya Wilaya ya Bagamoyo, kwa kutowajibika ipasavyo na kutozingatia kanuni za fedha na ameteua wapya.

Pinda alitangaza uamuzi huo mjini Bagamoyo mwanzoni mwa mwaka huu kwenye mkutano na viongozi na watendaji wa Halmashauri hiyo, akiwa Waziri mwenye dhamana ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa.

Aliwavua madaraka watendaji wakuu hao kwa kutumia kanuni ya 37 ya Kanuni za Utumishi wa Umma za Mwaka 2003 na kusema hatua nyingine za kinidhamu zitafuatia kadri itakavyoonekana inastahili.

Baada ya kuwavua madaraka watendaji hao, aliwateua Samuel Saiyanga kuwa Mkurugenzi Mtendaji mpya wa Halmashauri hiyo, akitokea Halmashauri ya Wilaya ya Kigoma na Fidelis Nenetwa kuwa Mweka Hazina, akitokea Halmashauri ya Manispaa ya Shinyanga.

Wengine walioteuliwa ni Fidelica Myovelo, kuwa Ofisa Kilimo, Mifugo na Ushirika akitokea Halmashauri ya Wilaya ya Iringa; Felista Masamba kuwa Mkaguzi wa Ndani akitokea Halmashauri ya Wilaya ya Lindi na Prudence Mtiganzi kuwa Mhandisi wa Maji akitokea Halmashauri ya Wilaya ya Kilombero.

Alisema uamuzi wa kuwapumzisha watendaji hao unatokana na mapendekezo ya ripoti ya uchunguzi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali, Septemba na Oktoba mwaka jana.

Uchunguzi wa Mdhibiti ulitokana na tuhuma za ukiukwaji wa kanuni za fedha, uzembe wa kufuatilia utekelezaji wa miradi na ubadhirifu katika Halmashauri hiyo.

Ripoti hiyo ilibainisha ukiukwaji mkubwa wa kanuni za fedha, uzembe na kushindwa kuwajibika na matokeo yake kuzorota kwa miradi ya maendeleo katika wilaya hiyo.

Waziri Mkuu alisema pamoja na kuwa hatua hizo zimechukuliwa kwa Bagamoyo, halmashauri zingine nchini zikae chonjo na zitashughulikiwa kwa kuwa nazo zina matatizo yanayofanana na ya Bagamoyo.

Thursday, February 11, 2010

Nguza Viking na mwanae papii wafungwa maisha.wawili waachiwa huru


Mahakama ya Rufaa Tanzania mapema leo imewaachia huru watoto wawili wa Mwanamuziki nyota wa muziki wa dansi hapa nchini Nguza Viking (Nguza Mbangu wa pili kulia na Francis Nguza wa mwisho kulia) huku yeye mwenyewe pamoja na mtoto wake Papii Kocha wakifungwa maisha.Baadhi ya Watu wamesema kuwa kutokana na kutolewa kwa hukumu hiyo mpaka sasa njia inayoweza kuwaokoa ni kwa Mh. Rais kutoa msamaha kwa makosa waliyoyafanya ya kubaka . Rufaa hiyo ilikuwa ikisikilizwa na Jaji Masati wa mahakama kuu ambapo hukumu hiyo imesomwa na Neema Chusi Naibu msajili wa mahakama ya Rufaa hukumu.Aidha hali ya Mahakamani hapo kwa ndugu na jamaa zao walishikwa na butwaa kwa kile kilichotokea huku wengi wao wakilia kwa uchungu.

Nguza Viking na mwanae papii wafungwa maisha.wawili waachiwa huru

Mahakama ya Rufaa Tanzania mapema leo imewaachia huru watoto wawili wa Mwanamuziki nyota wa muziki wa dansi hapa nchini Nguza Viking (Nguza Mbangu wa pili kulia na Francis Nguza wa mwisho kulia) huku yeye mwenyewe pamoja na mtoto wake Papii Kocha wakifungwa maisha.Baadhi ya Watu wamesema kuwa kutokana na kutolewa kwa hukumu hiyo mpaka sasa njia inayoweza kuwaokoa ni kwa Mh. Rais kutoa msamaha kwa makosa waliyoyafanya ya kubaka . Rufaa hiyo ilikuwa ikisikilizwa na Jaji Masati wa mahakama kuu ambapo hukumu hiyo imesomwa na Neema Chusi Naibu msajili wa mahakama ya Rufaa hukumu.Aidha hali ya Mahakamani hapo kwa ndugu na jamaa zao walishikwa na butwaa kwa kile kilichotokea huku wengi wao wakilia kwa uchungu.

Sakata la Richmond lazikwa Dodoma

KAMATI ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini imejivua suala la utata wa mkataba baina ya Tanesco na kampuni ya Richmond Development Company LLC, baada ya kueleza kuridhishwa na utekelezaji wa Serikali wa maazimio ya Bunge kuhusu sakata hilo huku ikielekeza kwamba masuala yaliyobaki, badala ya kubaki kama maazimio ya Bunge, yapelekwe kwenye kamati za kisekta zinazohusika.

Kamati hiyo kupitia kwa Mwenyekiti wake, Mbunge wa Bumbuli, William Shelukindo (CCM), imeliomba Bunge azimio lililotaka Mkurugenzi wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) na maofisa wa taasisi hiyo walioshiriki katika uchunguzi wa kuandaa taarifa ya Richmond wawajibishwe, kwa sasa liachwe kwenye mamlaka ya juu ya nchi.

Katika taarifa ya Kamati hiyo kuhusu utekelezaji wa maazimio hayo, hususan kuhusu watumishi hao wa Takukuru, Shelukindo alisema kamati imeona kuwa haitakuwa haki kutolea maelezo au majibu kwa Serikali kuhusu azimio hilo, kwa sababu Mkurugenzi Mkuu wa Takukuru anawachunguza wabunge.

“Kwa mantiki hii, kamati inaona Bunge likubali kwamba suala hili liachwe kwenye Mamlaka ya Juu ya Nchi,” alisema Shelukindo na kusisitiza kwamba hata kwenye kamati, azimio hilo Namba 9 halikujadiliwa. Kikatiba, Mkurugenzi Mkuu wa Takukuru huteuliwa na Rais.

Wakati katika maazimio mengi kamati ilieleza kuridhishwa na hatua zilizochukuliwa na Serikali, kwenye maazimio namba 5,7,9 na 14 yaliyotaka Serikali kuwawajibisha watumishi wote wa umma waliohusika katika suala hilo la Richmond, imeshauri Bunge likubaliane na maelezo yaliyotolewa na Serikali juu ya hatua ya Waziri Mkuu na mawaziri wawili waliowahi kuongoza Wizara ya Nishati na Madini kuwajibika kwa kujiuzulu.

“Kamati imezingatia maoni yaliyotolewa katika ripoti hii. Tofauti na ripoti iliyowasilishwa Agosti 2009, kwa kuwa haikutoa maelezo yoyote juu ya suala hili. Kwa kuwa Serikali sasa imejiridhisha kwenye kifungu 36(d)..., kamati inashauri Bunge likubaliane na maelezo hayo kwa kuzingatia msingi huo wa uwajibikaji,” alisema Shelukindo.

Alinukuu kifungu hicho cha 36(d) kwa kusema: “hatua ya kujiuzulu kwa aliyekuwa Waziri Mkuu pamoja na mawaziri wawili waliowahi kuongoza Wizara ya Nishati na Madini kwa kutekeleza dhana nzima ya uwajibikaji katika suala hili linalohusu zabuni kati ya Tanesco na Richmond”.

Aliyekuwa Waziri Mkuu wa wakati huo, Edward Lowassa, alipoulizwa na waandishi wa habari kuhusu taarifa hiyo ya kamati alisema baada ya kutoka katika ukumbi wa Bunge jana mchana kabla ya suala hilo kuhitimishwa jioni, hakuwa na maoni zaidi ya kusema anawaachia wabunge wachangie.

Hata hivyo, taarifa ya Serikali ya utekelezaji wa maazimio namba 8 na 14 yaliyoitaka Serikali kuwawajibisha viongozi wenye dhamana ya kisiasa waliokuwa mawaziri hao wa Nishati na Madini ambao ni Dk Ibrahim Msabaha na Nazir Karamagi, inaonesha suala la mawaziri hao halijaisha.

Taarifa hiyo inasema kwa sasa vyombo vya Dola vimekamilisha uchunguzi wa ndani ya nchi, lakini uchunguzi wa nje kwa kushirikiana na vyombo vya Dola vya kimataifa unaendelea na Serikali imehimiza vyombo hivyo vihitimishe suala hilo.

Katika maoni ya Kamati juu ya utekelezaji huo, Shelukindo aliliambia Bunge kwamba wamezingatia maelezo hayo ya Serikali kwa kupendekeza kuwa hatua hiyo iendelee chini ya usimamizi wa Serikali yenyewe, na utakapokuwa tayari, taarifa itolewe kwenye Kamati ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama.

Maazimio mengine ambayo kamati imeridhishwa nayo, ni namba moja na mbili yaliyoielekeza Serikali kufanya mapitio upya ya Sheria ya Ununuzi ya Umma ya mwaka 2004 kwa malengo ya kuiboresha na kuipa Mamlaka ya Udhibiti wa Ununuzi wa Umma (PPRA). Maazimio hayo pia yaliitaka Mamlaka hiyo isiwajibike kwa Wizara ya Fedha.

Serikali katika ufafanuzi wake, ilisema muswada husika utawasilishwa bungeni katika mkutano wa Aprili mwaka huu, hali ambayo kamati pamoja na kuridhishwa na hatua hiyo, imeshauri Serikali iendelee kushughulikia suala hilo na kuwasilisha taarifa kwenye Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Fedha na Uchumi.

Kuhusu Azimio namba 3 ambayo pamoja na mambo mengine, ilitaka mikataba ya madini ipitiwe upya, kamati ilipongeza Serikali kwa hatua iliyofikiwa katika kurekebisha mkataba wa Songas na kuhimiza utaratibu huo ufanyike kwenye mikataba mingine iliyobaki.

Eneo lingine ambalo Serikali imeikonga kamati, ni kwenye azimio namba 11 lililotaka kudhibiti utaratibu wa viongozi waandamizi wenye dhamana ya kisiasa kuendelea na biashara zao binafsi wakiwa madarakani.

Serikali katika maelezo kuhusu utekelezaji wake, imesema kipo kikundikazi kilichoundwa kushughulikia azimio hili kwa kuandaa waraka wenye Mapendekezo ya Kurekebisha Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma (Sura 398) ulio katika ngazi ya kujadiliwa na Kamati ya Makatibu Wakuu (IMTC).

Hata hivyo, kamati ilieleza kukubaliana na maelezo hayo ya Serikali lakini kwa kushauri iwasilishe Muswada wa Marekebisho ya Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma ya mwaka 1995 ili ufanyiwe marekebisho na kupelekwa kwenye Kamati ya Bunge ya Katiba, Sheria na Utawala, kabla ya Bunge hili kumaliza muda wake.

Katika Azimio namba 10, kamati ilimpongeza Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) kwa kuchunguza kwa umakini na kugundua kuwa malipo ya usafirishaji wa mitambo yalifanyika mara mbili; yaani kwa kutumia ndege na meli. Lakini ilishauri Serikali iendelee kufuatilia suala hilo, ili fedha hizo zirejeshwe serikalini.

Kuhusu azimio la kutaka wamiliki wa Richmond wafunguliwe kesi ya jinai, kamati ilieleza kuzingatia hatua zilizofikiwa na Serikali kwa kumfikisha mwakilishi wake, Naeem Gire mahakamani. Hata hivyo ilisisitiza wamiliki wafikishwe mahakamani na Serikali itoe taarifa kwa Kamati ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama.

Miongoni mwa wabunge waliochangia, ni wa Viti Maalumu, Stella Manyanya (CCM) ambaye licha ya kuwa mjumbe wa kamati hiyo, vile vile alihusika katika kamati maalumu iliyoundwa kuchunguza sakata hilo la Richmond.

Manyanya alisema watu wanaweza kujiuliza kwamba kwenye maazimio mbona Bunge linakubaliana na kuyapitisha; lakini alifafanua kwamba, “Bunge lilikuwa halibishani wala kushindana, bali lilichukua wajibu kutekeleza majukumu yake.

“Kwa upande wa Serikali, maazimio mengi yametekelezwa. Hilo ndo suala la msingi. Lakini sivyo tu, vilevle yale ambayo yanahitaji uchunguzi wa kina, ndiyo maana tumesema badala ya kubaki kwenye Bunge kama maazimio, yarudi kwenye sekta zinazohusika.”

Taarifa ya Serikali iliyopitiwa na kamati hiyo na kuiwasilisha jana bungeni, ilitanguliwa na taarifa mbili zilizowasilishwa bungeni na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda Agosti 28, mwaka juzi, nyingine Februari 11, mwaka jana na taarifa moja iliyokabidhiwa na kujadiliwa na kamati, ambazo zililitaarifu Bunge kuwa utekelezaji wa maazimio 10 kati ya 23 yaliyotolewa na Bunge ambayo katika uwasilishwaji wake uliofanyika Februari mwaka jana, utekelezaji wake ulikuwa haujakamilika.

Wakati huo huo, taarifa kuhusu namna Serikali ilivyoshughulikia suala la mgodi wa makaa ya mawe wa Kiwira, Kamati hiyo ya Nishati na Madini kupitia kwa Makamu Mwenyekiti wake, Dk Harrison Mwakyembe, iliipongeza Serikali kwa hatua ilizochukua kwa kusema hiyo ni ishara tosha ya Serikali kujali wananchi wake.

Hata hivyo, pamoja na kueleza kuridhishwa, kamati iliainisha baadhi ya maeneo yanayohitaji kutekelezwa ikiwa ni pamoja na kuikumbusha Serikali kufuatilia uchunguzi uliofanywa na Takukuru wa Sh milioni 50 zilizotolewa kutoka Consolidated Holdings Corporation kwenye mfuko wa mafao ya wafanyakazi wa mgodi huo.

Iliitaka Serikali ikamilishe haraka makabidhiano ya mgodi huo kutoka kampuni ya TANPOWER ili wafanyakazi ambao wanaendelea na shughuli za kutunza mgodi huo, sasa wafahamu wanaripoti kwa nani pindi watakapohitaji huduma.

Kwa upande mwingine, Kamati ilishangazwa na kitendo cha viongozi waandamizi wa Tanpower kulipwa malimbikizo ya mshahara hadi Sh milioni 80 kwa mwezi, wakati wafanyakazi wa kati walilipwa Sh milioni nane na ngazi ya chini Sh milioni 1.5.

Uamuzi wa rufaa ya babu Seya na wanawe kutolewa leo



Babu Seya, Papii Kocha, Nguza Mbangu na Francis Nguza wakisikiliza kesi yao mwaka jana.
Mahakama ya Rufaa Tanzania baadaye leo inatarajiwa kusoma uamuzi kuhusu rufaa ya mwanamuziki huyo maarufu na hao wanawe watatu...

Wednesday, February 10, 2010

Halmashauri kupatiwa fedha za kununulia dawa

WIZARA ya Afya na Ustawi wa Jamii imekubali wazo la kupeleka fedha katika Halmashauri kwa ajili ya kununulia dawa.

Naibu Waziri wa Wizara hiyo, Dk Aisha Kigoda amesema, Serikali inafanya tathmini ili kupata namna ya kudhibiti matumizi ya fedha hizo.

Mbunge wa Karatu, Dk Wilbroad Slaa ametoa wazo hilo bungeni wakati anauliza swali la nyongeza na kuiuliza Serikali kama haiwezi kupeleka katika Halmashauri asilimia 20 ya fedha za kununulia dawa ili zinunue popote kwa ajili ya wananchi badala ya kusubiri dawa kutoka Bohari ya Dawa(MSD).

Dk Kigoda amewaeleza wabunge kuwa, MSD imekasimu madaraka zaidi kwa bohari za kanda ili kuimarisha mfumo wa usambazaji wa dawa, vifaa tiba, na vitendanishi.

Wawekezaji kunyang'anywa viwanda

WAWEKEZAJI wanaokiuka mikataba ya ununuzi wa viwanda watanyang’anywa, Serikali imelieleza Bunge.

Waziri wa Viwanda, Biashara na Masoko, Mary Nagu, amewaeleza wabunge kuwa, wawekezaji hao watanyang’anywa viwanda hivyo, watapewa wanaoweza kuwekeza kwa manufaa ya taifa.

Waziri Nagu ametoa msimamo huo wakati anajibu swali la Mbunge wa Viti Maalum, Magdalena Sakaya, aliyedai kuwa, wawekezaji wengi wanakiuka mikataba ya ununuzi wa viwanda.

Kwa mujibu wa Nagu, Baraza la Mawaziri litaamua hatua za kuchukua endapo mwekezaji hatatekeleza mkataba wa mauzo.

Friday, February 5, 2010

BREKING NYUUUUUUZZZZZ: JERRY MURO NA WENGINE WAWILI WATINGA KIZIMBANI LEO

Mtangazaji wa TBC Jerry Muro na watu wengine wawili, Edmund Kapama na Deogratius Ngassa, wamepanda kizimbani mchana huu wakikabiliwa na mashataka kadhaa likiwemo la kula njama kutaka kupokea rushwa.

Mbele ya Hakimu Gabriel Mirumbe, Jerry Muro na washtakiwa hao wawili walishtakiwa kwa pamoja kwa kuomba rushwa ya shilingi milioni 10 toka kwa mweka hazina wa wilaya ya Bagamoyo aliefukuzwa kazi hivi karibuni na Waziri Mkuu kwa ubadhirifu Bw. Michael Wage.
Mwendesha Mashtaka wa Serikali Boniface Stancilaus akiwa na Mwendesha Mashtaka toka TAKUKURU Benny Lincolin wamedai mahakamani hapo kwamba mshtakiwa wa kwanza na wa pili pia wanakabiliwa na shtaka la kujipachika wadhifa ambao sio wao.
Inasemekana January 29, 2010 katika hoteli ya Sea Cliff washtakiwa walijitambulisha mbele ya Wage kuwa wao ni maafisa wa Takukuru wakati sio kweli.

Upande wa mashtaka uliiomba mahakama usitoe dhamana hasa kwa washtakiwa wa kwanza na wa pili kwa madai kwamba waliwahi kufungwa huko nyuma na kuwa kwao nje kutaharibu upelelezi ambao haujakamilika na bado unaendelea.

Hakimu alipowataka kutoa uthibitisho kwamba washtakiwa hao waliwahi kufungwa huko nyuma upande wa mashtaka ulishindwa kuthibitisha hivyo dhamana ikawa wazi kwa m ashartia ya kila mmoja kuwa na wadhamini wawili wataosaini bondi ya milioni 5 kila mmoja, ama kwenda rumande hadi Februari 12, mwaka huu kesi itaposomwam tena.

Jerry Muro na Edmund Kapama
walitimiza masharti ya dhamana na kuachiwa.
Ngassa atapelekwa rumande.

Pinda aagiza ‘Muro achunguzwe haraka, kwa kina’

WAZIRI Mkuu Mizengo Pinda ameagiza uchunguzi kuhusu sakata la mwandishi wa habari, Jerry Muro, anayetuhumiwa kwa rushwa na kukutwa na pingu, ufanyike kwa kina na haraka ili ukweli ubainike, badala ya suala hilo kuendelea kuibua hisia mbaya miongoni mwa wananchi.

Pinda alisema jana bungeni kwamba binafsi hapendi suala hilo liendelee kwa muda mrefu, kwa kuwa linaweza kuanza kuleta hisia zisizo nzuri kwa wananchi.

Aliliambia Bunge kwamba amezungumza na Waziri wa Mambo ya Ndani, Mkuu wa Jeshi la Polisi na amehakikishiwa kwamba suala hilo halitachukua muda mrefu kumalizika.

Waziri Mkuu alitoa ufafanuzi huo bungeni baada ya Kiongozi wa Upinzani Bungeni, Hamad Rashid Mohamed, kulifikisha jana katika chombo hicho cha kutunga sheria wakati wa kipindi cha maswali ya papo kwa hapo.

“Kwa kauli nilizozipata tayari, nimezungumza na Waziri wa Mambo ya Ndani, nimezungumza na Inspekta Jenerali wa Polisi, nimehakikishiwa kwamba jambo hili wataliharakisha sana, vile vile kwa sababu linaweza kuleta hisia zisizo nzuri sana kwa wananchi, na tutajitahidi tuweze kulimaliza haraka,” alisema Pinda.

Pinda alisema mkanganyiko uliojitokeza ndani ya suala hilo ni namna ambavyo polisi walivyoanza kulishughulikia, hususan kuanzia kwenye vyombo vya habari na wakati huo huo Muro mwenyewe kutumia vyombo hivyo pia.

“Tatizo ninalolipata Mheshimiwa Hamad ni pengine namna jambo hili lilivyoanza kushughulikiwa, sababu tumekimbilia kwenye vyombo vya habari sisi tunaochunguza na yeye kama mtuhumiwa ametafuta vyombo vya habari na kuvitumia, kwa hiyo sasa ujumbe tunaowapa wananchi kwa ujumla unaweza ukatuchanganya sana,” alisema Pinda.

Alisema kutokana na mazingira hayo, ndiyo maana inabidi uchunguzi ufanyike na uwe wa kina, ili kubaini ukweli wa yale wanayomtuhumu ni kiasi gani na kiasi gani si kweli.

Katika swali lake la msingi Hamad ambaye pia ni Mbunge wa Wawi (CUF) alitaka kufahamu iwapo misukosuko anayopata Muro ambaye ni mwandishi wa kituo cha Televisheni ya Shirika la Habari Tanzania (TBC1), kama ni sehemu ya misukosuko wanayopata waandishi wa habari wanaofuatilia mambo mazito duniani hasa barani Afrika.

Hamad alisema kwa muda mrefu waandishi wengi wa habari wanaofuatilia mambo mazito ya nchi, hupata misukosuko sehemu mbalimbali duniani hasa katika Bara la Afrika.

Naibu Spika wa Bunge, Anne Makinda kabla ya kumpa nafasi Waziri Mkuu kujibu swali hilo la kwanza kuulizwa katika mfululizo wa maswali yaliyokuwa yamepangwa, alimwambia Hamad, “Bahati yako, halijaenda mahakamani.”

Pia Waziri Mkuu katika kujibu alianza kusema, “hili suala lingekwenda mahakamani jibu lingekuwa rahisi kweli.”

Katika majibu yake, alisema, “Labda niseme kwanza kwamba, binadamu alivyoumbwa ni kiumbe mwenye upungufu, hata kama angekuwa ana sifa nyingine zote, lakini tukubali tu kwamba atakuwa na upungufu.

Waziri Mkuu anao, Hamad anao, kwa hiyo na waandishi wa habari vile vile wanao upungufu wao kama binadamu.” Alisema ndiyo sababu zikawekwa sheria, kanuni.

“Sasa yaliyompata Jerry, kama binadamu na kama mtumishi mwingine yeyote, ni jambo ambalo linawezekana kabisa, yale anayotuhumiwa yanawezekana yakawapo, vile vile yasiwepo,” alisema Pinda.

Alisema kutokana na suala hilo kukimbiziwa kwanza kwenye vyombo vya habari na kujenga picha tofauti kwa wananchi, ndiyo maana upo umuhimu wa kufanya uchunguzi wa kina.

“Kwa hiyo mimi rai yangu ni kuwa uchunguzi fanyeni kama mnavyofanya uchunguzi mwingine wowote, utakapofikia mwisho itajulikana kama ni kesi ya kwenda mahakamani au hapana,” alisema Pinda.

Wakati huo huo, kwenye swali la nyongeza, Mbunge huyo wa Wawi alitaka kufahamu ni namna gani Waziri Mkuu anaweza kutumia nafasi yake kuhakikisha suala hilo linakwenda na kumalizika haraka kuepuka linavyoandikwa.

Thursday, February 4, 2010

Msekwa alia na Spika Sitta

WAKATI Halmashauri Kuu (NEC) ya Chama Cha Mapinduzi ikitarajiwa kupokea, Jumatano ijayo, taarifa ya Kamati ya Rais mstaafu, Ali Hassan Mwinyi inayotafuta njia ya kumaliza msuguano ndani ya chama hicho, mmoja wa wajumbe wa kamati hiyo ambaye pia ni Makamu Mwenyekiti wa chama hicho, Pius Msekwa, ameelezwa kutaka Spika wa Bunge Samuel Sitta achukuliwe hatua, Raia Mwema limefahamishwa.

Habari za ndani ya CCM zimeeleza kwamba Msekwa, ambaye alipoteza nafasi yake ya Uspika baada ya kushindwa na Sitta, amekuwa akionyesha waziwazi kutaka hatua zichukuliwe dhidi ya Sitta na wabunge wanaomuunga mkono katika vita dhidi ya ufisadi.

Hata hivyo, Msekwa amekuwa akipata pingamizi kutoka kwa wajumbe wenzake, akiwamo Mzee Mwinyi, na Spika wa kwanza wa Baraza la Kutunga Sheria la Jumuiya ya Afrika Mashariki, Abdurahaman Kinana.

Wakati Kinana ameelezwa kuwa na msimamo mkali zaidi akitaka pande zote husika zichukuliwe hatua kulingana na uzito wa tuhuma, kwa watuhumiwa wa ufisadi kushughulikiwa kukisafisha chama na Sitta na wenzake kukemewa, Mzee Mwinyi amekuwa akielezwa kutumia busara zaidi kutoa maoni yake.

“Msekwa alisema wazi kwamba matatizo ya sasa yasingekuwapo kama Sitta angechukuliwa hatua na vikao vya CCM vilivyoandaliwa mahususi kumshughulikia, lakini Mzee Mwinyi akamwambia chama hicho tawala hakiendeshwi kwa jazba,” anasema mtoa habari wetu ndani ya CCM.

Soma zaidi

UFAFANUZI WA SPIKA KUHUSU TAARIFA POTOFU ZILIZOTOLEWA NA BAADHI YA VYOMBO VYA HABARI KUHUSU SERIKALI KUUONDOA MUSWADA WA BARAZA LA USALAMA LA TAIFA WA

Waheshimiwa Wabunge, napenda kutoa ufafanuzi kuhusu utaratibu unaotumika kuamua ni Muswada upi uende Kamati gani, na huu utaratibu siyo kwamba ni hiari ya mtu isipokuwa unatawaliwa na Sheria na Kanuni za Bunge. Kwahiyo napenda kutoa ufafanuzi kuhusiana na mwenendo wa kupeleka Miswada katika Kamati kwa mujibu wa Kanuni zilizotungwa na Bunge kama ifuatavyo;

Muswada wa Sheria hupelekwa kwenye Kamati na Spika kama isemavyo Kanuni ya 84(1) “Spika atapeleka Muswada wa Sheria kwenye kamati inayohusika na Kamati itaanza kuujadili muswada huo mapema iwezekanavyo’’

Kwa mujibu wa Kanuni za Bunge toleo la 2007, Kanuni ya 114(14) inasema; Kamati inayohusika ni ile iliyopelekewa Muswada kwanza kama isemavyo Kanuni hiyo nanukuu;

“Kamati yoyote ambayo Spika atapeleka kwake kwanza Muswada au jambo lingine lolote, itahesabiwa kuwa ndiyo Kamati inayohusika kushughulikia Muswada huo au jambo hilo’’

Kwa mujibu wa Kanuni hizi uamuzi wowote wa Spika kupeleka Muswada kwenye Kamati yoyote ni halali kwa kuwa amepewa mamlaka ya kufanya hivyo.

Hata hivyo, kwa kuzingatia matakwa ya Nyongeza ya Nane Kifungu cha 9(1)b ya Kanuni za Bunge Toleo la 2007, moja ya Majukumu ya Kamati za Kudumu za Sekta ni kushughulikia Miswada ya Sheria na Mikataba inayopendekezwa kuridhiwa na Bunge iliyo chini ya Wizara inayozisimamia, kwa hiyo tunazo Kamati za Kisekta ambazo zinaweza kupewa Miswada ya Sekta zake, kwa hiyo Kamati ya Katiba, Sheria na Utawala ndiyo inayosimamia Ofisi ya Rais – Utawala Bora kama ilivyotajwa kwenye Nyongeza ya Nane, Kifungu cha 8(2)(a) kisemacho:
“Kamati ya Katiba, Sheria na Utawala itasimamia shughuli za Wizara zifuatazo:
(a) Ofisi ya Rais;
(i) Utawala Bora
(ii) Menejimenti ya Utumishi wa Umma.” na
Kwa mujibu wa Kanuni za Bunge, kwenye Nyongeza ya Nane, Kifungu cha 8(4) Kamati ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama inasimamia shughuli za Wizara zifuatazo:-
Wizara ya Mambo ya Nchi za Nje na Ushirikiano wa Kimataifa;
Wizara ya Ushirikiano wa Afrika Mashariki;
Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa na
Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi.

Hivyo waheshimiwa wabunge kwa mujibu wa Kanuni, Nyongeza ya Nane, Kifungu cha 8(2)(a) na 9(1)(b) hakukuwa na kosa wala tatizo lolote kwa maamuzi ya kupeleka muswada huo katika Kamati ya Katiba, Sheria na Utawala kwa sababu sekta ama Wizara hii iko chini ya Kamati hii.
Waheshimiwa Wabunge, Kamati inayopelekewa Muswada inaweza kuwaruhusu Wabunge ambao si wajumbe wa Kamati au watu ambao si Wabunge kuhudhuria na kushiriki katika shughuli za Kamati kama ilivyo Kanuni ya 114(8) isemayo:
‘’Bila kuathiri masharti yaliyotangulia ya Kanuni hii, kila Kamati itajiwekea utaratibu wake, na Kamati inaweza kuwaruhusu wabunge ambao si wajumbe wa Kamati au watu ambao si wabunge kuhudhuria na kushiriki shughuli za Kamati lakini hawatakuwa na haki ya kupiga kura’’.
Kwa hiyo tarehe 3/11/2009 Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba, Sheria na Utawala ilifanya kikao cha pamoja na Kamati ya Kudumu ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama kujadili kwa pamoja muswada huo Dodoma Hotel.
Kamati ilikwenda mbali zaidi kwa kuwaita pia wadau mbali mbali waje kujadili muswada huo na tarehe 15 Oktoba, 2009 Kamati ilialika wadau na waliofika walikuwa ni taasisi zisizo za kiserikali za NOLA (National Organization for Legal Assistance) na Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (Legal and Human Rights Centre).

Hata hivyo, tangu tarehe 30 Januari, 2010 baadhi ya Vyombo vya Habari vimekuwa vikitoa taarifa potofu kuhusiana na kuondolewa na Serikali kwa Muswada wa Baraza la Usalama wa Taifa kwa kutumia kifungu 87(1) cha Kanuni za Bunge baada ya michango ya baadhi ya Wabunge kuonyesha kutokukubaliana na baadhi ya vifungu katika Muswada huo.
Habari hizo za upotoshaji zimekaziwa jana tarehe 2 Februari, 2010 katika gazeti lingine la Mtanzania Toleo namba 512 lililobeba habari yenye ujumbe usemao “Sitta aikoroga Serikali’’ likiwa na dondoo zifuatazo:
Apeleka Muswada kwenye Kamati siyo
Siri yavuja, Ofisi yake ilionywa ikakataa
Malecela, Ngwilizi, Lubeleje washangaa
Na gazeti lingine la Tazama Tanzania, toleo namba 378 nalo la tarehe 2 Februari, 2010 lililobeba habari yenye kichwa cha habari kinachosomeka `Spika Sitta achangia kumkwaza Waziri Sophia Simba’.
Waheshimiwa Wabunge, kama nilivyosema ni vizuri magazeti yakatumia kanuni zetu. Kuondolewa kwa Muswada uliowasilishwa na Mheshimiwa Waziri, Sophia Simba, ni utaratibu tu, na wala siyo mara ya kwanza kwa Muswada kuondolewa kama itafikia mahali Serikali ikaridhika na kuona kwamba inafaa kuchukua hatua kama hiyo, jambo ambalo ni utaratibu wa kawaida ambao hufanyika ndani ya Bunge, na kwa maoni yangu ni utaratibu mzuri kwa sababu Serikali inaonesha umakini na usikivu wa kile ambacho Wananchi wake wanajadili kupitia Wawakilishi wao ambao ni Waheshimiwa Wabunge.
Kwa mantiki hiyo pale itakapoonekana kwamba, maoni yale hayafai, Kanuni zinamruhusu Waziri husika kuuondoa Muswada huo ili kuufanyia marekebisho kwa lengo la kuuboresha zaidi, kwa hiyo si kosa na wala si ishara ya Wizara husika kushindwa kufanyakazi.

Kwa maoni yangu ni vyema vyombo vya habari vikazingatia Kanuni za Bunge pindi vinapokuwa vinaripoti juu ya maamuzi yanayofanywa na Bunge kuhusiana na masuala mbalimbali ili kuweza kuwatendea haki Watanzania na pia kuepusha migongano baina ya Mihimili ya Dola.

Ufafanuzi huu umetolewa jana tarehe 03 Februari 2010.

Wednesday, February 3, 2010

Miswada muhimu yasogezwa mbele

MISWADA miwili ya Uchaguzi ambayo imekuwa ikisubiriwa kwa hamu kuwasilishwa jana bungeni, sasa itawasilishwa rasmi Jumatatu ijayo, huku Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Sera, Uratibu na Bunge, Philip Marmo akisema imesogezwa mbele ili kuiboresha zaidi.

Akizungumza na HabariLeo juzi mjini hapa, Marmo alisema miswada hiyo ambayo ni wa Gharama ya Uchaguzi na wa Marekebisho ya Sheria za Uchaguzi yote ya mwaka 2009, imekuwa ikivutia hisia za watu wengi hivyo kuonekana bora kushirikisha wadau zaidi ili iweze kueleweka.

“Tunachofanya ni kuhakikisha tunawaelewesha wabunge na wananchi kuwa miswada hii si ya kuwaadhibu bali kuhakikisha kuwa makosa yanayofanyika katika uchaguzi yanadhibitiwa,” alisema Marmo.

Alisema sheria iliyopo ya uchaguzi imekuwa na makosa mengi hasa katika upande wa rushwa, hivyo sheria ya sasa inajaribu kufafanua zaidi kipi halali na kipi si halali kwa kuzingatia maoni ya wadau.

Alisema katika mkutano uliofanyika hivi karibuni chini ya Waziri Mkuu Mizengo Pinda, kila mbunge aliyezungumza hakupinga moja kwa moja muswada huo, bali alitaka ufanyiwe maboresho zaidi hasa katika kipengele cha taratibu za kuwa wazi wakati wa uchaguzi, mwenendo usiofaa katika kampeni na kumchangia mtu fedha nyingi kupita kiasi.

Alisema lengo la sheria hiyo ni kuwa wazi kwa matumizi ya fedha wakati wa kampeni, hali ambayo haikudhibitiwa katika sheria ya uchaguzi iliyopo ambayo inatakiwa kufanyiwa marekebisho.

wali akiahirisha Bunge katika Kikao cha Sita cha Mkutano wa 18 unaoendelea mjini hapa, Mwenyekiti wa Bunge, Zubeir Ali Maulid, alitangaza mabadiliko ya ratiba ikionesha kuwa miswada hiyo miwili ingewasilishwa mmoja jana na mwingine kesho na kila mmoja ukijadiliwa kwa siku mbili.

Kwa mujibu wa ratiba ya sasa muswada wa gharama za uchaguzi utawasilishwa siku ya Jumatatu na muswada wa Marekebisho ya Sheria utawasilishwa Jumatano.

Ratiba hiyo inaonesha badala ya muswada wa gharama kutakuwa na Azimio la Bunge la Kuridhia Mkataba wa Kimataifa kuhusu Kahawa wa mwaka 2007 na Azimio la Bunge kuridhia Mkataba wa Kimataifa kuhusu Hakimiliki za Wagunduzi wa aina mpya za Mimea na Azimio la Bunge la kuridhia Itifaki ya Jinsia na Maendeleo ya Jumuiya ya Nchi za Kusini mwa Afrika (SADC).

Polisi: Muro alishirikiana na watuhumiwa sugu


POLISI Dar es Salaam imesema mtangazaji wa TBC, Jerry Muro ameshirikiana na watuhumiwa sugu wa utapeli kumdai rushwa ya Sh milioni 10 aliyekuwa Mhazini wa Halmashauri ya Wilaya ya Bagamoyo, Michael Wage.

Kamanda wa Polisi wa Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Suleiman Kova, jana aliwaonesha waandishi wa habari watuhumiwa hao ambao wanadaiwa pia kuwa na kesi mbalimbali za utapeli na kujifanya kuwa ni maofisa Usalama wa Taifa.

Watuhumiwa hao Edmund Kapama (52) mkazi wa Mwananyamala amebainika kwamba mwaka jana alipandishwa kizimbani katika Mahakama ya Wilaya ya Ilala, akikabiliwa na tuhuma za udanganyifu akijifanya ofisa usalama wa Taifa aliyetumwa kuchunguza mwenendo mbaya wa kazi wa Naibu Waziri wa Kazi, Ajira na Maendeleo ya Vijana na kutaka apewe rushwa.

Mwingine aliyehusishwa na Jerry ni Deogratias Mgasa (35), mkazi wa Mbezi Beach ambaye pia alikamatwa mwaka jana akidaiwa kuwa kiongozi wa mtandao wa matapeli nchini akituhumiwa kutapeli Sh bilioni 4 kutoka kwa watu zaidi ya 40.

Mtuhumiwa huyo akiwa na wenzake, inadaiwa alijifanya mtumishi wa taasisi nyeti, ikiwamo ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa nchini (Takukuru), Usalama wa Taifa na Jeshi la Polisi na wote wanadaiwa kuibia wafanyabiashara, watumishi wa sekta mbalimbali na taasisi za fedha.

“Katika kuendelea na upelelezi wa kesi ya Michael anayedaiwa kupata vitisho na kutakiwa atoe Sh milioni 10 na watuhumiwa watatu, polisi waliwatia mbaroni watuhumiwa wengine wawili baada ya kupata taarifa kutoka kwa raia wema,” alisema Kamanda.

Alisema watuhumiwa hao walikamatwa juzi katika mgahawa maarufu wa PR Camp, Kinondoni na kabla ya kukamatwa polisi wapelelezi walipata kumbukumbu za watuhumiwa hao wakidaiwa kushirikiana na Muro kupitia picha zilizoonekana kwenye CCTV.

“Katika tukio hili watuhumiwa watatu walionekana wakiwa katika meza ya mazungumzo na mlalamikaji. Pia kumbukumbu zingine zinaendelea kufuatiliwa kwa kutumia mtindo huu wa vifaa vya teknolojia ya kisasa, ili kuondoa ubishi au utata kwa lengo la kupata ufanisi na uwazi,” alisema.

Aidha, alisema walipata kumbukumbu za hoteli walizokaa kati ya Januari 28 na 29 mwaka huu na walifanya upelelezi na kukutana na wahusika wa hoteli na wahudumu na kukubali kuwatambua, ingawa hawakutambua walichokuwa wakijadili na kwamba yataelezwa zaidi mahakamani.

Pia Kova alisema watu hao walifanyiwa gwaride la utambulisho na mlalamikaji aliwatambua. Hata hivyo, alisema kwamba watuhumiwa hao wawili watafikishwa mahakamani wakati wowote huku Muro akisubiri jalada lake lifikishwe kwa wakili wa Serikali Kanda ili kujiridhisha.

Alipoulizwa iweje watuhumiwa wote wafunguliwe jalada moja halafu mmoja atengwe na wengine wapandishwe kizimbani, Kova alijibu kwamba Polisi ina mamlaka ya kuamua mshitakiwa afikishwe mahakamani kwa wakati gani endapo yuko nje kwa dhamana.

“Mtuhumiwa anapokuwa nje ni uamuzi wa Polisi kumpeleka mahakamani kwa wakati wowote, labda kama angekuwa yuko mahabusu ndipo kungekuwa na muda maalumu wa kumpeleka mahakamani.

Muro ni mwaminifu na tunaamini hawezi kutoroka maana ni mwajiriwa ila hawa ni matapeli nikiwaachia hapa siwapati tena,” alisema.

Akizungumzia utata uliopo na tetesi kwamba tuhuma hizo za Muro zimepikwa, alisema yeye hawezi kujidhalilisha kwa kesi kama hiyo, isipokuwa anatimiza wajibu wake kama polisi na asingeweza kukwepa jukumu hilo, maana limepitia mikononi mwake.

“Katika kesi hii hakuna mipango yoyote na sidhani kama kuna kitu cha tofauti zaidi ya tuhuma zilizopo na kama kipo cha tofauti, mimi sikijui … hapa natimiza wajibu wangu na siwezi kubambika kesi kama hii na kamwe siwezi kujidhalilisha kwa kupanga kakesi kama haka,” alisema Kamanda.

Kuhusu risiti ya pingu ambayo Muro alitakiwa kuiwasilisha alisema kuwa hadi jana mchana alikuwa bado hajaiwasilisha.

Muro, ambaye mwaka jana alipata tuzo ya mwandishi bora, alikamatwa na Polisi Januari 31 mwaka huu mchana, katika hoteli ya City Garden katikati ya Jiji akidaiwa kutaka kupokea rushwa ya Sh milioni 10 ingawa hakukutwa na udhibiti.

Hata hivyo baadaye polisi walimfikisha katika kituo kikuu na kumhoji kwa saa kadhaa na hatimaye kumwachia huru akisubiri jalada lifikishwe kwa Mwanasheria wa Serikali.

Tuesday, February 2, 2010

Walioidhinisha fedha EPA wadaiwa kutokuwa na kosa

ALIYEKUWA Mkurugenzi Msaidizi katika Idara ya Madeni ya Nje katika Benki Kuu Tanzania (BoT), Emmanuel Boaz, ameiambia Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, kwamba maofisa wa BoT, Iman Mwakosya, Ester Komu na Sophia Larika, wanaokabiliwa na mashitaka ya kujipatia fedha kwa njia ya udanganyifu kwenye Akaunti ya Madeni ya Nje (EPA), kupitia kampuni ya Mibale Farm hawakufanya kosa.

Boaz alipohojiwa na mawakili wa washitakiwa hao ambao wanashitakiwa pamoja na Farijala Hussein, Rajab Maranda na Ajey Somani, alidai kuwa kwa uelewa wake, kama ambavyo yeye alikuwa akitenda kazi zake na washitakiwa hao, walifanya hivyo pia hajui kama walikuwa na nia ovu katika kuidhinisha malipo ya zaidi ya Sh bilioni 3.8.

Akihojiwa jana na wakili Majura Magafu, alikubaliana naye kwamba waliopitia jalada la maombi ya kuhamishiwa deni kwenda Kampuni ya Mibale kutoka Kampuni ya India ya Lakshmi Textile Mills, walikuwa 10 akiwamo yeye na kuwa hajui sababu ya maofisa hao kushitakiwa na wengine kuachwa.

Aliendelea kudai, kuwa malipo ya Mibale Farm hayakuwa na shaka kwani yalikuwa halali na pia hakukuwa na shaka dhidi ya ofisa yeyote wa BoT kuhusu malipo hayo.

Mbele ya jopo la mahakimu watatu wakiongozwa na Samwel Kalua, shahidi huyo alidai kwamba yeye na watendaji wote waliokuwa wakishughulikia malipo ya kampuni hiyo, walifuata maelekezo ya aliyekuwa na kauli ya mwisho katika malipo hayo, Gavana wa BoT, Daudi Balali (marehemu).

Katika mashitaka hayo, Mibale Farm inadaiwa kuhamishiwa deni la BoT na Lakshmi Textile Mills. Hussein, Maranda, Somani na Kiza Selemani ambaye hayumo katika kesi hiyo, walisaini hati za makubaliano hayo ya kuhamisha deni ambayo inadaiwa kuwa ni ya kughushi.

Ilidaiwa kuwa Oktoba 26, 2005, BoT iliingiza fedha hizo kwenye akaunti iliyofunguliwa na watuhumiwa hao ikiwa na namba 6005274 ya Mibale Farm katika Benki ya Barclays na benki hiyo kutia shaka kwa kuwa fedha hizo ziliingizwa kwa jina la Mibale Farm na si Nibale Farm na hivyo ilitaka kufahamu uhalali wake.

Monday, February 1, 2010

Mtangazaji anayefichua tuhuma za rushwa mbaroni


JESHI la Polisi katika Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, linamshikilia mtangazaji wa Shirika la Habari Tanzania (TBC), Jerry Muro, kwa tuhuma za kudai fedha kwa njia ya vitisho kwa aliyekuwa Mhasibu wa Halmashauri ya Wilaya ya Bagamoyo, Michael Wage.

Akizungumza na gazeti hili kwa simu jana jioni, Kamanda wa Polisi wa Kanda hiyo, Suleimani Kova alisema Muro alimtishia Wage kuwa yeye ni Ofisa wa Kitengo cha Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) na kumtaka atoe fedha Sh milioni 10.

“Mpaka sasa, Polisi bado inamhoji mtuhumiwa na baada ya mahojiano hayo kukamilika, taratibu za kisheria zitachukuliwa dhidi yake na maelezo zaidi kuhusu mtangazaji huyo nitayatoa kesho (leo) wakati wa mazungumzo yangu na waandishi wa habari,” alisema Kova jana saa 12:15 joni.

Gazeti hili lilimshuhudia mtangazaji huyo akiwa katika Kituo Kikuu cha Polisi, akiwa ameshikilia bahasha kubwa tatu za khaki pamoja na kamera ya video.

Akizungumzia tukio hilo, Muro ambaye amejipatia umaarufu katika siku za karibuni kwa vipindi vyake vya uchunguzi, alikana tuhuma hizo na kueleza kushangazwa kuwekwa chini ya ulinzi kwa madai kuwa alipigiwa simu na mtu kupewa taarifa kuwa kuna kazi katika Hoteli ya City Garden, katikati ya Jiji.

“Nilipewa taarifa ya kazi City Garden, lakini baada ya kufika hapo nilishangaa nawekwa chini ya ulinzi na askari waliovaa kiraia ambao ndiyo walionifikisha kituoni hapa ingawa sielewi kosa langu, lakini nakana tuhuma hizo siyo kweli,” alisema Muro.

Naye mlalamikaji Wage alidai mtuhumiwa huyo anatumiwa na watu wengine ambapo juzi alimpandisha katika gari lake na kumfunga pingu kisha kumtaka atoe Sh milioni 10. Kwa kuthibitisha kuwa alikuwa ndani ya gari hilo, alidai kuacha miwani yake yenye mikanda myeusi.

Baada ya polisi kumhoji, Muro kama anazo pingu, alikiri kumiliki pingu pamoja na bastola ambapo baada upekuzi katika gari lake lenye namba za usajili T545 BEH aina ya Toyota Crester, polisi walikuta pingu hizo pamoja miwani iliyodaiwa kuwa ya mlalamikaji.

Hadi kufikia saa 12:15 jioni, gazeti hili lilipoondoka kituoni hapo, mtangazaji huyo alikuwa anashikiliwa na polisi kwa mahojiano.

Muro ni mtangazaji aliyejizolea umaarufu zaidi kupitia kipindi chake cha Usiku wa Habari kinachooneshwa kila siku kupitia Kituo cha TBC1. Kabla ya kuhamia TBC, alikuwa mtangazaji wa ITV.

Wabunge 'walilia' fedha za ofisi

WABUNGE wamelalamika kuwa hawajawahi kupata fedha kwa ajili ya kuendesha ofisi zao.

Waziri Mkuu, Mizengo Pinda ameahidi kuyafanyia kazi malalamiko hayo.

Leo asubuhi wabunge walipiga kelele bungeni kupinga maelezo ya Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) kuwa kuna fedha zinatolewa kwa ajili ya kuendesha ofisi za wabunge.

Mwanri amewaeleza wabunge kuwa kuna fedha zinatolewa kwa ajili ya ofisi zao ikiwa ni pamoja na kununulia samani na kugharamia mambo mengine ikiwemo chai.

“Fedha za kuendesha ofisi za wabunge zimekuwa zikitolewa kupitia ofisi za wakuu wa mikoa (Makatibu Tawala wa mikoa) na hatimaye kupelekwa kwenye ofisi za wakuu wa wilaya (Makatibu tawala wa wilaya)” amesema Mwanri wakati anajibu swali la Mbunge wa Mkinga, Mbarouk Mwandoro.

Mbunge wa Pangani, Mohamed Rished Abdallah, amesema bungeni kuwa hafahamu kama kuna fedha zinatolewa kwa ajili ya ofisi ya Mbunge.

Mbunge wa Iramba Mashariki, Mgana Msindai amesema amekuwa Mbunge kwa miaka 15 na hajawahi kupata fedha za ofisi yake.

Mbunge huyo alishauri kuwa, fedha hizo ziingizwe kwenye fungu la fedha za Mfuko wa Kuchochea Maendeleo wa Jimbo (CDCF), Waziri Mkuu Mizengo Pinda amekataa.

Waziri Mkuu amewaeleza wabunge kuwa kwa mfumo wa sasa haifahamiki fedha kiasi gani zinapelekwa kwa Mbunge yupi ili kuendesha ofisi.

Pinda amesema, Serikali itatafuta mfumo mzuri wa kuzisimamia fedha hizo hivyo wabunge wampe muda.

Mwanri amewapongeza wabunge kwa kuuliza kuhusu fedha za CDCF kwa kuwa hata yeye na Waziri Mkuu wanazihitaji kwa sababu wana majimbo.

Mwandoro alimuuliza Waziri Mkuu, ni lini Serikali kwa kushirikiana na Ofisi ya Bunge itaanza kuzitumia fedha za CDCF kwa kuwa Bunge lilishapitisha sheria hiyo, na Rais wa Tanzania ametoa kibali iwe sheria rasmi.

Mwanri amelieleza Bunge kuwa fedha za CDCF ni za maendeleo, si za kwa ajili ya kuendesha ofisi ya Mbunge.