Tuesday, February 23, 2010

Naibu Waziri asafishwa kashfa ya vyeti feki

TUME ya Vyuo Vikuu (TCU) imemsafisha Naibu Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika, Dk David Mathayo kwa kuvitambua vyeti vyake vya shahada ya kwanza ya mifugo, shahada ya uzamili ya kilimo na sayansi pamoja na udaktari wa falsafa.

Dk Mathayo amesema, uamuzi huo ni ahueni kwa kwa kuwa jila lake lilichafuliwa sasa limesafishwa.

Kiongozi huyo wa Serikali amesema, uvumi kwamba anatumia vyeti feki ulikuwa ni uzushi wa kumuonea.

Kwa mujibu wa barua ya tume hiyo iliyosainiwa na Katibu Mtendaji wa TCU, Profesa Mayunga Nkunya, na kutumwa kwa Dk Mathayo, vyeti hivyo vimethibitishwa na kutambuliwa rasmi na tume hiyo kuwa ni sahihi. Dk Mathayo aliwasilisha vyeti hivyo TCU Februari 12 mwaka huu,

“Kwa kutumia mamlaka tuliyopewa kupitia vifungu vya Sheria ya Tume ya Vyuo Vikuu, tunathibitisha kutambua vyeti vyako vya elimu, kuanzia shahada, Shahada ya uzamili na udaktari wa falsafa kuwa vimetolewa na vyuo pamoja na taasisi za elimu zinazotambuliwa,” amesema Profesa Nkunya katika barua hiyo.

Tuna nakala ya barua hiyo ya kumsafisha Dk Mathayo huyo, nakala imepelekwa kwa Spika wa Bunge la Tanzania, Samuel Sitta, Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, na Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Profesa Jumanne Maghembe.

“Mimi kwa sasa sina la kusema zaidi ya kumshukuru Mungu na nimefurahi kwa kweli, masuala mengine nitayazungumza siku nyingine ila leo nimepata ahueni,” amesema Dk Mathayo.

Profesa Nkunya hakupatikana ili athibitishe taarifa kuhusu barua hiyo,wasaidizi wake wa karibu wamedai kuwa amesafiri. Ofisa Uhusiano wa TCU, Edward Mkaku, hakutaka kuzungumzia suala hilo.

Katika mkutano wa 18 wa Bunge uliomalizika hivi karibuni mjini Dodoma, Spika Sitta alitangaza bungeni kuwa vyeti vya Dk Mathayo vimethibitishwa kuwa ni sahihi na vinatambulika.

Dk Mathayo pamoja na mawaziri wengine sita walituhumiwa kughushi sifa za taaluma na kuzitumia kujipatia nyadhifa mbalimbali za kisiasa.

Taarifa za uhakikiwa vyeti vya mawaziri kadhaa wanaotuhumiwa kuwa na vyeti vya kughushi hazijatolewa.

Mawaziri hao ni Waziri wa Viwanda, Biashara na Masoko, Dk Mary Nagu, Naibu Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Dk John Nchimbi, na Naibu Waziri wa Kazi, Ajira na Maendeleo ya Vijana Dk Makongoro Mahanga.

Wengine ni Waziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki,Dk. Diodurus Kamala,Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam ambaye pia ni Mbunge wa Issmani, William Lukuvi,Mbunge wa Lupa(CCM),Victor Mwambalaswa,na Mbunge wa Busega (CCM)Dk. Raphael Chegeni.

1 comment:

Anonymous said...

Wizi mtupu!!