Thursday, July 12, 2012

Nusu ya Bajeti ya Ardhi kujenga Kigamboni mpya

Na Florence Majani, Dodoma
 WIZARA ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, imetenga zaidi ya nusu ya bajeti yake kwa mwaka wa fedha, 2012/2013 kwa ajili ya kuanza utekelezaji wa mradi wa ujenzi wa mji mpya wa Kigamboni, Manispaa ya Temeke, Dar es Salaam.Fedha zilizotengwa kwa ajili ya kuendeleza mji huo ni Sh60 bilioni ambazo ni sawa na asilimia 59 ya makadirio ya matumizi ya wizara hiyo, ambayo ni Sh101.731 bilioni.

Hata hivyo, Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Profesa Anna Tibaijuka alisema Bungeni jana kuwa fedha zilizotengwa kwa ajili ya ujenzi huo ni sawa na asilimia 10 tu ya mahitaji ya kiasi cha Sh605.
“Kwa hiyo tutatumia mbinu za kisasa kutafuta pesa nyingine Sh605 bilioni nje ya Bajeti kutekeleza mradi huu bila kuchelewa zaidi. Mradi huu unahitaji kiasi hicho cha fedha kwa miaka mitatu ya kwanza,” alisema Profesa Tibaijuka alipokuwa akiwasilisha makadirio ya matumizi ya wizara yake jana na kuongeza:

“Nitasimamia mradi huu kwa kasi, ari na nguvu mpya. Ingawa pia sitakuwa nimetenda haki iwapo sitawashukuru wananchi wa Kigamboni kwa uvumilivu na ushirikiano wanaotuonyesha.”

Katika Bajeti ya wizara hiyo ya Sh101.7 bilioni, matumizi ya kawaida ni Sh30.7 bilioni na Sh71 bilioni ni za maendeleo. Katika fedha hizo za maendeleo, Sh61 bilioni ni fedha za ndani na Sh10 bilioni ni fedha za nje.

Kuhusu wananchi wanaoishi katika eneo hilo, Profesa Tibaijuka alisema hakuna mkazi yeyote wa Kigamboni atakayehamishwa kwani idadi ya wananchi waliopo ni ndogo ikilinganishwa na idadi ya makazi mapya yanayotakiwa kujengwa katika eneo hilo.
Alisema ni ushauri wake kwamba wakazi wote wa Kigamboni wachague kubaki katika mji huo kwani wawekezaji wa ndani na nje watapewa maeneo kwa ajili ya kujenga makazi ambayo yatatumika kuwahamishia wananchi watakaoamua kubaki.

“Tunashauri wote wabaki kwa kuwa sasa hivi kuna wananchi takribani 82,000 wakati tunajenga mji mpya wenye uwezo wa wakazi 400,000. Hakuna sababu ya wananchi kuhama eneo hili ila makazi yao yatapangwa upya na kuboreshwa,” alisema.

Gharama za mradi
Profesa Tibaijuka alisema ujenzi wa Mji wa Kigamboni utafanywa kwa awamu tatu, ambazo zitatekelezwa kati ya mwaka huu na 2032 na gharama zinazotarajiwa kutumika hadi utakapokamilika ni Sh11.6 trilioni.

Alisema awamu ya kwanza itakuwa kati ya mwaka 2012 na 2022, awamu ya pili kati ya 2022 na 2027 na awamu ya tatu ni kati ya 2027 na 2032.
Profesa Tibaijuka alisema miongoni mwa kazi zitakazofanywa katika mwaka huu wa fedha ni kuundwa kwa wakala mpya wa kusimamia mradi huo anayejulikana kama Kigamboni Development Agency (KDA).

Kazi nyingine ni kuidhinisha mpango na kuanza utekelezaji, kufanya uthamini wa mali zilizomo katika maeneo ya miundombinu, huduma za maji na eneo mbadala na kulipa fidia kwa mali zilizomo katika maeneo yaliyofanyiwa uthamini.

Kuhusu fidia, Waziri Tibaijuka alisema wananchi ambao hawajakiuka maagizo ya mradi kwa kufanya maendelezo haramu, wasiwe na wasiwasi kuhusu fidia kwa sababu mradi utazingatia haki na ni endelevu... “Fidia itatolewa kwa mujibu wa sheria kwa tathmini ya kiujumla ambayo itakokotolewa kutokana na viwango vya soko na kuhusishwa ili iwe sahihi.”

Alisema atafanya ziara ya mafunzo kwa wawakilishi kutoka Kigamboni kutembelea mji mpya ili uwepo uelewa wa pamoja juu ya jinsi mji huo utakavyokuwa.

Hazina ya Ardhi
Katika hatua nyingine, Profesa Tibaijuka alisema wizara yake inakamilisha uanzishaji wa Hazina ya Ardhi pamoja na Mfuko wa Fidia ya Ardhi.
Alisema vyombo hivyo vitasimamia utoaji wa ardhi kwa wawekezaji wa ndani na nje kwa misingi ya kuingia ubia wa kumiliki pamoja hisa zitakazotolewa kwa uwiano kati ya wananchi na wawekezaji husika.

Kuhusu kuweka na kutunza alama za mipaka ya Tanzania na nchi jirani, Profesa Tibaijuka alisema majadiliano ya kupima maeneo hayo yalishakamilika.
Alisema majadiliano yalishafanyika baina ya Tanzania na nchi za Comoro na Msumbiji na mkataba wa kwanza kati ya Tanzania, Msumbiji na Comoro kwenye alama za utatu baharini inayotenganisha nchi hizo ulikamilika na kutiwa saini Desemba 5, mwaka jana.

“Mkataba wa pili kati ya Tanzania, Shelisheli na Comoro ulitiwa saini Februari 17, mwaka huu. Hivyo basi, Tanzania imekamilisha upimaji wa mipaka katika Bahari ya Hindi na itatangaza eneo lake la ukanda wa kiuchumi baharini bila kipingamizi kwa nchi jirani,” alisema.

Alisema wizara yake imewasilisha andiko la kudai nyongeza ya eneo ya ukanda wa kiuchumi baharini Januari, mwaka huu na Tume ya Mipaka ya Baharini ya Umoja wa Mataifa, inapitia andiko hilo.

Profesa Tibaijuka alisema kupatikana kwa eneo hilo lenye ukubwa wa kilomita za mraba 61,000 kutaiwezesha Tanzania kuvuna rasilimali za chini ya bahari kwa manufaa ya sasa na kwa vizazi vijavyo.

Kurasini kulipwa fidia
Kuhusu mradi wa uendelezaji wa eneo la Kurasini ulioanza 2006 kwa ajili ya upanuzi wa Bandari ya Dar es Salaam, Profesa Tibaijuka alisema wizara imetenga fedha chini ya Wizara ya Viwanda na Biashara kulipa fidia kwa wananchi watakaopisha mradi huo katika eneo la Kurasini na Shimo la Udongo.

“Wizara itaendelea na malipo hayo kwani hata mwaka jana tulilipa kiasi cha Sh550 milioni kwa wakazi wa Mtaa wa Kurasini waliopo jirani na Mabwawa ya Majitaka,” alisema.

Alisema wizara yake itaendelea kutatua migogoro ya ardhi, urasimishaji wa makazi holela, mikopo ya nyumba, ujenzi wa nyumba unaofanywa na Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) na ujenzi wa nyumba za biashara na makazi.

No comments: