Monday, July 9, 2012

Dk Ulimboka apata ahaueni

Na Geofrey Nyang'oro
AFYA ya Mwenyekiti wa Jumuiya ya Madaktari, Dk Steven Ulimboka imeanza kuimarika ingawa bado amelazwa katika Chumba cha Wanaohitaji Uangalizi Maalumu (ICU).

Dk Ulimboka alipelekwa Afrika Kusini  Juni 30, mwaka huu baada ya jopo la madaktari lililokuwa likimtibu, likiongozwa na Profesa Joseph Kahamba kutoa taarifa za kubadilika ghafla kwa afya yake na kupendekeza apelekwa nje ya nchi kwa ajili ya vipimo na matibabu zaidi.

Jana, Katibu wa Jumuiya ya Madaktari, Dk Edwin Chitage alisema taarifa walizokuwa nazo zinasema: “Afya mwenyekiti wetu imeanza kuimarikia, lakini bado yupo katika chumba cha wagonjwa mahututi kwani alikuwa naumwa sana.”

Katika hatua nyingine, Dk Chitage alisema madaktari na wananchi wa kawaida wanaendelea kutoa mchango wa awamu ya pili unaolenga kukusanya Dola za Marekani 30,000 kwa ajili ya kulipia gharama za matibabu za Dk Ulimboka.

“Sijapata kiwango sahihi kilichokusanywa hadi sasa, lakini michango inaendelea vizuri. Madaktari na wananchi wanaendelea kukusanya na tunawashukuru,” alisema Dk Chitage.

Madaktari na ndugu wa Dk Ulimboka kwa pamoja, walikataa ofa iliyokuwa itolewe na Serikali ya kulipia gharama za matibabu za mgonjwa huyo wakiishutumu kuhusika na tukio la kutekwa, kupigwa na kutupwa katika Msitu wa Pande kwa mwenyekiti huyo wa jumuiya ya madaktari.
Madaktari pia wamepinga tume ya polisi iliyoundwa na Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Kamishna Msaidizi wa Polisi, Suleman Kova wakitaka kuundwa kwa tume huru kuchunguza tukio hilo.

Hilo ni miongoni mwa madai matano ya madaktari yaliyomo katika tamko la pamoja baina yao na viongozi wa dini na wanaharakati.

Madai mengine ni pamoja na Serikali kurejea katika meza ya majadiliano na madaktari, kufuta kesi iliyofungua mahakamani dhidi ya madaktari hao, kuwarejesha kazini waliofukuzwa na Rais Jakaya Kikwete kukutana na viongozi hao kujadili chanzo cha mgogoro huo.

No comments: