Monday, July 30, 2012

Maganzo: Mji wenye utajiri wa almasi usio na huduma ya maji

Mmoja wa wakazi wa Kijiji cha Masagala nje kidogo ya Mji mdogo wa Maganzo akitoka kuchota maji bwawani bwawa hili lilichimbwa na mkandarasi huyo.
Binti akichota maji katika moja ya mabwawa ambayo si salama kwa matumizi anuai bwawa hili lilichibwa na mkandarasi aliyekuwa akitengeneza barabara.
Mabinti wakitoka kusaka maji kwa matumizi anuai.

Na Joachim Mushi, Kishapu

KWA mtazamo wa kawaida ni kitendo cha kawaida kwa mji wowote kuendelea kutokana na rasilimali zake zinaouzunguka mji huo. Maeneo mengi nje ya nchi na hata Tanzania yamekuwa yakipata maendeleo ya jamii na mazingira yake kutokana na rasilimali na shughuli za kijamii zinazolizunguka eneo lenyewe.

Hali hii ni tofauti na ilivyo katika Mji mdogo wa Maganzo uliopo wilayani Kishapu, Mkoa wa Shinyanga, ambao umefanikiwa kuwa na rasilimali ghali yenye thamani kubwa ulimwenguni. Mji huu una madini ya almasi yanayopatikana karibia sehemu kubwa ya eneo la Maganzo.

Kihistoria Mji wa Maganzo unachimbwa madini ya almasi tangu kitambo kidogo. Wananchi wanachimba madini hayo katika mashamba, viwanja na maeneo mengine ambayo yanaaminika kuwa na almasi. Huu ni utajiri mkubwa ambao Mji mdogo wa Maganzo umefanikiwa kuwa nao.

Baadhi ya wananchi wamefanikiwa kunufaika na utajiri huu. Nasema hivyo maana ukifika katika eneo hilo utashuhudia nyumba za thamani na za kisasa na hata magari ya kifahari ambayo baadhi ya wakazi wa eneo hilo wameyapata kutokana na almasi.

Mji huo unahuduma ya umeme, afya (japokuwa kunachangamoto kadhaa), mawasiliano (mtandao wa simu) na pia umefanikiwa kupitiwa na barabara kuu ya lami inayotoka Shinyanga mjini kuelekea Mkoa wa Mwanza. Kwa kiasi fulani mji unavutia.

Wapo wawekezaji kadhaa wa madini akiwemo Kampuni ya Williamson Diamonds ambayo licha ya kumiliki eneo kubwa la machimbo ya almasi inamiliki maeneo mengine kadhaa ya ndani ya mji huo. Wachimbaji hawa wanaendesha shughuli za uchimbaji madini eneo hilo.

Lakini pamoja na rasilimali hii ya Mji Mdogo wa Maganzo hauna huduma ya maji safi na salama ya uhakika. Mji mzima hauna maji ya bomba na badala yake hutegemea maji ya kuletwa kwa madumu kwa baiskeli kutoka mjini Mwadui ambapo ni kilometa kadhaa kutoka katika mji huo.

Wachuuzi wa maji kwa kutumia baiskeli ndio wanaotoa huduma ya maji safi na salama kwa wakazi wa Mji wa Maganzo. Wachuzi hawa zaidi ya 100 ndio wanaotegemewa kuupatia mji huu maji kibiashara. Dumu moja la maji huuzwa kati ya sh. 400 hadi 500 kulingana na umbali alipo mwananchi anayeitaji maji hayo.

Benard Lucas ni mmoja wa wachuuzi (wauzaji wa maji kwa kutumia baiskeli) Maganzo, anasema alianza kufanya biashara hiyo ya uuzaji wa maji tangu mwaka 2009 baada ya kupata mtaji. Anasema uuzaji wa maji eneo hilo unaitaji muhusika awe na baiskeli pamoja na madumu ya kubebea maji pekee.

“Sehemu ambayo huyachota maji haya sisi hatulipii...huyachota bure kazi yako ni kusafirisha kwa kutumia baiskeli na kuwatafuta wateja walipo. Dumu moja la maji tunauza kati ya shilingi 400 na 500 kulingana na umbali anapopatikana mteja,” anasema Lucas.

Anasema kwa upande wake huuza madumu 14 hadi 16 kwa siku kulingana na uchakarikaji wa siku hiyo. Mwanambelembe Machia ni muuzaji mwingine wa maji katika Mji mdogo wa Maganzo, anasema amekuwa akifanya biashara hiyo kwa muda mrefu sasa na inalipa.

“Mimi nina watu wangu maalumu ambao tumekubaliana kupeleka maji kiasi fulani kwa kila siku. Huwa napata wastani wa shilingi 5,000 kwa siku kama kukiwa na biashara mbaya lakini kiasi hiki kinanitosha kabisa kwa matumizi yangu,” anasema Machia.

Kwa upande wake Frank Simba mchuuzi wa maji eneo hilo anasema alimaliza elimu ya msingi mwishoni mwa 2011, lakini baada ya kushindwa kuendelea na masomo ya sekondari alinunuliwa baiskeli na wazazi wake na kuanza biashara hiyo ya uuzaji maji ili aweze kujitegemea.

Anasema msimu mbaya wa biashara hiyo ni kipindi cha masika ambacho wananchi hutegemea maji ya mvua ili kukwepa gharama. “Kutokana na wingi wetu kipindi hiki huwa kibaya kwa biashara maana wateja huadimika kabisa,” anasema kijana huyu anaeomba shida ya maji isitoweke Maganzo.
 
Hata hivyo Sera ya Maji ya nchi ya mwaka 2002 inaeleza kuwa madhumuni ya jumla ya sera kuhusu utoaji wa huduma ya maji vijijini ni kuboresha afya ya jamii na kusaidia kuondoa umaskini vijijini ikiwa ni pamoja na kuboresha upatikanaji wa maji safi, salama na ya kutosha.

Madhumuni mahsusi ya sera hiyo ni kuhakikisha upatikanaji wa huduma endelevu ya maji safi, salama na ya kutosha, kwa gharama iliyo ndani ya uwezo wa wananchi vijijini. Pia kuweka bayana majukumu na wajibu wa wadau mbalimbali. Lakini kama hiyo haitoshi sera pia imesisitiza kuhusu wananchi kulipia sehemu ya gharama za ujenzi wa miradi, na pia kulipia gharama zote za uendeshaji na matengenezo ya miradi yao, tofauti na dhana iliyokuwepo ya kuchangia tu sehemu ya gharama za uendeshaji na matengenezo.

Hii haipingwi kuwa maji ni hitaji la msingi na haki ya kila mtu. Na kwa kutambua kuwa upatikanaji wa maji safi na salama ni hitaji la msingi na haki ya kila mtu, utoaji wa huduma ya maji vijijini utaimarishwa. Hata hivyo haki kama hii haipo kwa wakazi wa Mji mdogo wa Maganzo ambao unautajiri mkubwa wa almasi. Wakazi wa eneo hili kutokana na shida ya maji wamekuwa wakitumia maji kutoka kwenye madimbwi kukwepa gharama za kununua maji kila kukicha, huku wakihatarisha maisha yao kiafya.

Mwenyekiti wa Serikali ya Kijiji cha Maganzo, Lwinzi Kidiga anakiri huduma ya maji ni kero kubwa kwa wakazi wa vijiji vyote vinavyo zunguka eneo hilo. Anabainisha kuwa zipo juhudi ambazo yeye na viongozi wenzake wanazifanya kuhakikisha wanakabiliana na hali hiyo.

Anasema kwa sasa tayari uongozi wa kijiji umefanya mazungumzo na mwekezaji wa madini ya almasi eneo hilo, ambaye pia ni mmiliki wa mgodi wa Williamson unaochimba almasi eneo hilo na mwekezaji huyo amekubalia kuwaletea maji wananchi kwenye moja ya tanki kubwa ambalo lipo jirani na soko kubwa eneo hilo. Anaongeza kuwa mradi huo unatarajia kuanza kati ya mwezi Julai, 2012.

Lakini huenda miaka kadhaa ijayo kero hiyo ya maji ikatoweka kwani, Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Kishapu, Lucas Said akizungumzia kero hiyo anasema kwa sasa wataalamu wanafanya utafiti katika vijiji kadhaa kuhakikisha vinapatiwa huduma ya maji pale mpango wa kuleta maji kutoka Ziwa Victoria kwa matumizi eneo hilo utakapo kamilika.

No comments: