Thursday, July 12, 2012

‘Katiba mpya itoe miaka 10 tu kwa wabunge, wawakilishi’

Na Masoud Sanani, Zanzibar
BAADHI ya wakazi wa Zanzibar wametaka Katiba Mpya iweke kipindi cha ubunge na uwakilishi kiwe miaka 10 kama ilivyo kwa Rais ili kuimarisha demokrasia nchini.Wakitoa maoni kwenye Mkutano wa kusaka maoni ulioandaliwa na Tume ya Katiba mjini hapa walisema  lazima wabunge wawe na miaka 10 kama ilivyo kwa Rais badala ya kutaka wawe wabunge milele.

Abdallah Khamis Abdallah (54) na Bakar Mwinyi Mussa (63) wa Mitakawani walitaka wabunge wa wajumbe wa Baraza la Wawakilishi wawe na muda maalumu wa uongozi wa miaka 10 kama ilivyo kwa Urais.
Abdallah pia alitaka Rais, Makamu wa Rais na Waziri Mkuu na vyeo vingine vya juu wakistaafu wawe kama wananchi wa kawaida wasienziwe kama ilivyo sasa kwani ni gharama kubwa kwa uchumi wa Taifa.

“Rais ana pensheni kubwa na marupurupu mengi kwa hiyo alipwe akawe kama mwananchi wa kawaida asiendelee kutunzwa ma Serikali,” alitoa maoni yake kwa Tume inayochukua maoni juu ya kuandikwa kwa Katiba Mpya.Alitaka pia rasilimali za Taifa ziwe za Muungano na zimilikiwe na dola.


Katika hatua nyingine wakazi wengi waliotoa maoni yao juu ya kuandikwa Katiba Mpya nchini walitaka mfumo wa sasa uendelee, lakini Rais wa Zanzibar awe Makamu wa Rais wa Muungano.

Wakitoa maoni yao katika maeneo ya Mgeni Haji, Mitakawani na Uzini, Wilaya ya Kati, Mkoa wa Kusini Unguja jana walipendekeza mfumo wa Serikali ya Muungano na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar uendelee.

Lakini wananchi hao walitaka Rais wa Zanzibar awe Makamu wa Rais wa Muungano badala ya kuwa waziri katika Muungano kama ilivyo sasa.Pia wananchi hao walitaka kero zote za Muungano ziondolewe ili Muungano uimarike na misaada kutoka nje igawiwe kwa pande zote mbili za Muungano yaani Bara na Zanzibar.

Awali mkazi Zanzibar, alishauri Katiba Mpya iwe na kipengere kitakachowatoa Ikulu Marais wanaomaliza muda wao na kutaka kugombea awamu nyingine ili wanapogombea wawe wanatoka nyumbani kwao badala ya kutoka Ikulu.

Akitoa maoni yake mbele ya Tume ya Katiba iliyopo Mkoa wa Kusini Unguja, Hassan Pandu Ibada (40) mkazi wa Mpapa, Wilaya ya Kati alieleza kuwa Rais anapaswa kutoka Ikulu wakati wa uchaguzi.
Alitaka Katiba Mpya itoe nafasi ya kuwapo kwa Rais wa muda ambaye baada ya uchaguzi atamkabidhi madaraka aliyeshinda katika uchaguzi mkuu.

“Rais akiwa wa Muungano au wa Zanzibar asitoke Ikulu na kwenda kwenye viwanja vya kampeni kuwania urais, aondoke Ikulu ili awe sawa na wagombea wengine,” alieleza mwananchi huyo .

No comments: