Tuesday, July 24, 2012

Asilimia 30 ya watoto hufanyiwa ukatili nchini

Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto, Sofia Simba amesema ripoti ya utafiti wa ukatili dhidi ya watoto nchini, imeonyesha takribani wanawake watatu kati ya 10 na mwanaume mmoja kati ya saba, walifanyiwa vitendo vya ukatili wa kijinsia na watu wazima walipokuwa watoto chini ya umri wa miaka 18.

Alisema matokeo ya utafiti huo yatasaidia kuweka mikakati madhubuti ya kuzuia na kukabiliana na tatizo hilo.

Aidha, Simba, alisema matokeo hayo yatasaidia katika kuanzisha taratibu za kuboresha huduma kwa waathirika wa ukatili na kuandaa miongozo na kanuni za utekelezaji wa Sheria ya Mtoto Namba 21 ya mwaka 2009.

“Katika mwaka huu wa fedha wizara itasambaza kanuni na miongozo hiyo katika halmashauri zote nchini, ili wananchi waweze kuzielewa na kuzizingatia…pia itatayarisha mwongozo wa kukusanya takwimu za watoto wanaonyanyaswa,” alisema.

Simba alieleza hayo bungeni jana alipokuwa akiwasilisha makadirio ya mapato na matumizi ya wizara yake kwa mwaka wa fedha 2012/13.

Wizara hiyo imeomba bajeti ya Sh. bilioni 15.6 ambapo kati ya hizo Sh. bilioni 12.1 ni matumizi ya kawaida.

Wakati huo huo, Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni imemshambulia Waziri Simba, kwa kumhadaa, kumdanganya na kumteleza Nasra Mohamed ambaye alifariki dunia baada kufanyiwa unyama na mumewe.

Mbunge wa Viti Maalum (Chadema), Conjesta Rwamlaza, alitoa kauli hiyo alipokuwa akisoma maoni ya kambi hiyo kuhusu makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara ya Maendeleo ya jamii, Jinsia na Watoto kwa mwaka 2012/13.

“Waziri Simba ambaye pia ni Mwenyekiti wa Umoja wa Wanawake wa CCM Taifa alieleze Bunge hili ni kwanini alimhadaa, kumdanganya na kumtelekeza Nasra Mohamed bila msaada wowote wakati aliahidi kwa kinywa chake mwenyewe kuwa angemsaidia?” alisema na kuongeza:

“Kambi ya Upinzani inataka kujua Waziri anawasaidiaje watoto walioachwa na marehemu na pia hatua gani zitachukuliwa dhidi ya aliyetenda ukatili huu?”

Alisema wanasikitishwa kuona kwamba Serikali haiko mstari wa mbele katika kupigania haki kwa wanawake wanaonyanyaswa.

Rwamlaza alisema tukio hilo lilitokea Februari 19  mwaka huu, katika Wilaya ya Bunda Mkoani Mara, ambako Nasra Mohamed, alifanyiwa unyama na mumewe Elisha Mkumbati ambaye alimgonga kwa makusudi na gari na baadaye kumburuza na gari hilo jambo lililomsababishia maumivu makali na hatimaye umauti.

 
CHANZO: NIPASHE

No comments: