Friday, February 4, 2011

Umeme balaa jipya

-Bado miezi miwili kuwa giza totoro
-Sasa kudura za Mungu tu ndio mwokozi

HALI ya uzalishaji umeme nchini ni mbaya. Kiwango cha maji kwa ajili ya kuzalisha umeme kwas asa kina ukomo wa miezi miwili tu kama mvua za kutosha hazitanyesha, Raia Mwema imetafiti na kuthibitishiwa na uongozi wa shirika la umeme nchini, TANESCO,na Waziri wa Nishati na Madini, William Ngeleja.

Kwa mujibu wa uchunguzi wa gazeti hili, sekta ya uzalishaji umeme nchini inakabiliwa na matatizo makubwa matatu. La kwanza ni uhaba wa maji katika mabwawa ya kuzalisha umeme, hususan bwawa muhimu la Mtera, mkoani Iringa.

Tatizo la pili ni uhaba wa gesi asilia ambayo imekuwa ikitumika na kituo cha kuzalisha umeme cha Songas kilichopo Ubungo, ikibainika kuwa upatikanaji wa gesi hiyo si wa kutosheleza mahitaji. La tatu ni uhaba wa mafuta ya kuzalisha umeme, hasa katika mtambo wa IPTL, chanzo kikiwa ni ukosefu wa fedha.

Hali ya umeme nchini Uchunguzi wa gazeti hili kwa miezi kadhaa sasa umebaini kuwa hali ni Mbaya mno, na hilo linathibitishwa na mgao wa umeme unaoendelea nchini hivi sasa.

Sababu ya mgao huo uliodumu kwa zaidi ya miezi miwili ni mbili. Taarifa za kiuchunguzi zinafichua kuwa, sababu ya kwanza ni matatizo katika mitambo ya gesi asilia iliyopo katika kisiwa cha Songosongo.

Gesi asilia huzalishwa Songosongo na hupelekwa kwa mabomba hadi kituo cha Songas, Ubungo, na kusambazwa kwenye vituo vinavyonunua gesi hiyo ili kuzalisha umeme.

Vile vile licha ya mitambo ya gesi kuwa mibovu na matengenezo yakeyakitajwa kuendelea vizuri, Raia Mwema imebaini kuwa kiasi cha gesi inayopatikana kwa ajili ya uzalishaji huo kinazidi kupungua.

Sababu ya pili ni uhaba wa maji kwenye mabwawa ya kuzalisha umeme. Vituo vya Kihansi (megawati 180), New-Pangani Falls (megawati 68), Hale (megawati 21) na Nyumba ya Mungu (megawati 8), vinazalisha chini ya uwezo.

Hali ya kuzalisha chini ya uwezo inatokana na maji yanayoingia kwenye mitambo hiyo kuwa kidogo na kwa kuwa vituo hivyo havina mabwawa makubwa yanayohifadhi maji mengi. Kati ya vituo hivyo, ni Nyumba ya Mungu pekee yenye hifadhi ya maji.

Matokeo ya hali hiyo ya uzalishaji umeme kushuka ni kwamba TANESCO inawajibika kugawa umeme kwa sehemu na kwa awamu, maarufu kama “mgawo wa umeme”.

Mahitaji ya umeme ni makubwa kuliko uzalishaji. Mahitaji ya juu ya umeme hivi sasa nchini katika gridi ya taifa ni megawati 840 wakati mitambo ya kufua umeme (ya maji, gesi na mafuta kwa pamoja) inazalisha takriban megawati 670.

Kwa hiyo kuna upungufu wa kati ya megawati 170 na megawati 200, kulingana na mahitaji ya umeme ya kila siku.

Tutarajie nini siku zijazo?

Hakuna matarajio nje ya uwezo wa Mwenyezi Mungu kuihurumia nchi kwa kushusha mvua nyingi katika kipindi cha miezi michache ijayo ili ijaze mabwawa.

Ikiwa mvua za kutosha hazitanyesha ili kuongeza maji kwenye mabwawa, tutarajie kwamba hali ya umeme itakuwa mbaya zaidi.

Taarifa zilizopo zinathibitisha kuwa kwa kiasi kikubwa nchi inategemea umeme wa maji. Bwawa la Mtera ndilo linalohifadhi maji mengi yanayotegemewa kuzalisha umeme kwenye kituo cha Mtera kinachozalisha megawati 80.

Maji hayo ya Mtera pia huelekea bwawa dogo la Kidatu na kutumika kuzalisha umeme kituo cha Kidatu chenye uwezo wa megawati 200.

Raia Mwema imebaini kuwa maji kwenye bwawa la Mtera yamepungua na wakati huo huo yanayoingia bwawani hapo (inflows) ni kidogo.

Umebaki umeme wa miezi miwili

Kwa mujibu wa uchunguzi wetu, hadi Januari 28, mwaka huu, bwawa la Mtera lilikuwa lina mita 691.73 za ujazo tu kutoka usawa wa bahari.

Maana yake ni kwamba kuna mita 1.73 tu zilizobaki kabla ya kina cha chini cha bwawa hilo kufikiwa, ambacho ni mita 698.50, kutoka usawa wa bahari.

Kwa mujibu wa watalaamu wa TANESCO, mita 1.73 ya ujazo ziliyobaki za maji, zinatosheleza kuzalisha umeme kwa miezi miwili tu, ikiwa mvua haitanyesha na kuongeza maji kwenye bwawa hilo.

Kwa maana hiyo, watalaamu wa TANESCO wanaeleza kuwa kinachosubiriwa ni neema ya Mungu kuleta mvua.

“...ama tutarajie baada ya miezi miwili uwezekano wa kituo au bwawa la Mtera kufungwa maji yakiisha. Mtera ikifungwa, lazima Kidatu nayo itafungwa kwa sababu wote hutumia maji ya mto Ruaha.

“Matokeo ya kufungwa vituo hivi ni kuongezeka kwa “mgawo” kwa sababu vituo vya gesi na mafuta yaani Songas (megawati 189), Ubungo Gas Plant (102Mw); IPTL (100Mw) na Tegeta (45Mw) havina uwezo wa kutosheleza mahitaji ya nchi.

“Vituo vya nguvu ya maji (Kidatu, Kihansi, Mtera, New Pangani Falls,Hale na Nyumba ya Mungu) vina uwezo (installed capacity) ya Mw561 pamoja na vituo vya gesi, mafuta na dizeli-uwezo wa taifa ni Mw 1047 tu,” anasema mhandisi wa TANESCO, ambaye hakuwa tayari kuandikwa jina lake gazetini.

IPTL na ukosefu wa fedha

Kituo cha IPTL kwa wakati huu kinasuasua kwenye uzalishaji kwa sababu ya ukosefu wa mafuta ya kuzalisha umeme.

Wiki kadhaa, mitambo ya kituo hicho iliwashwa ili kupunguza ukali wa “mgawo” unaeondelea lakini kilizalisha megawati 20 tu badala ya megawati 100, kutokana na upungufu wa mafuta.

Vituo vya gesi (Songas, Ubungo na Tegeta) navyo vinazalisha chini ya uwezo wake kutokana na upungufu wa gesi kutoka Songosongo.

Upungufu wa gesi unaweza kuathiri hata miradi mingine mipya. Kwa mfano, mipango ya kuwa na kituo cha Kinyerezi, ifikapo mwaka 2013, haitafikiwa ikiwa bomba la Songosongo halitapanuliwa.

“Leo hii Serikali ikiruhusu Dowans kununuliwa na umeme wake ikauziwa TANESCO, Dowans haitafikia kiwango chake cha juu cha megawati 100 kutokana na uhaba wa gesi.

“Hili ni tatizo ambalo Wizara ya Nishati na Madini inapaswa kulichukua kwa uzito unaostahili na mitambo ya Songosongo inahitajiwa kupanuliwa na bomba lililopo kukarabatiwa ili gesi ya kutosha ifikishwe Dar es Salaam kwa mahitaji ya wateja wa viwandani na hasa vituo vya umeme,” anasema mtaalamu ndani ya TANESCO, akisisitiza kutoandikwa jina lake gazetini kwa kuwa si msemaji wa shirika hilo.

Tatizo kubwa zaidi

Mbali na matatizo hayo, tatizo kubwa zaidi ni kutokuwa na umeme wa zaida(reserve margin au spinning reserve) kwenye mifumo ya kuzalisha umeme.

Ndiyo sababu kukitokea hitilafu kidogo kwenye mifumo ya kuzalisha umeme, hakuna suluhisho mbadala zaidi ya kutangaza “mgawo”.

Kwa mfano, mtambo wa megawati 50 ukiharibika Kidatu au Songas, lazima “mgawo » wa umeme utatangazwa.

Umeme si kipaumbele cha serikali?

Tangu utawala wa Rais Ali Hassan Mwinyi, Benjamin Mkapa na sasa JakayaKikwete, hakujawa na uwekezaji wa kutosha katika sekta ya umeme na pia, miradi ya ubabaishaji imekuwa ikiibuliwa mara kwa mara, kama vile Richmond.

Wataalamu ndani ya TANESCO wanaeleza kuwa katika Awamu ya Kwanza, ikiongozwa na Mwalimu Julius Nyerere, serikali ilikuwa makini katika nishati. Wanaeleza kuwa wakati huo, mitambo ya ziada ya kuzalisha umeme ilikuwapo na baadhi yaka ilipokuwa ikipata hitilafu, mitambo ya ziada ilikuwa tarari kuanza kazi na hapakuwahi kuwa na “mgawo”.

Utaratibu huo ndio unatajwa kutumika katika nchi zinazotambua kuwaumeme ni suala nyeti. Kwa mara ya kwanza nchini, mgawo wa umeme ulianza mwaka 1992 wakati wa utawala wa Mwinyi, ukaendelea wakati wa Mkapa na kushamiri wakati huu wa Kikwete.

Tafiti zinabainisha kuwa wakati Tanzania inahangaika na umeme wa kuvizia kutoka mitambo ya megawati 100 kama Dowans, nchini Afrika Kusini, watu binafsi wamekuwa na mitambo ya kuzalisha umeme wa megawati 100 ndani ya uzio wa nyumba zao.

Kauli ya bosi TANESCO

Raia Mwema iliwasiliana na Mkurugenzi Mkuu wa TANESCO, William Mhando, ambaye alikiri kuwa hali ya uzalishaji umeme ni mbaya na kiwango cha
maji kilichobaki kinaweza kuzalisha umeme wa miezi miwili pekee, kama mvua hazitanyesha.

“Ni kweli, kiwango cha maji si cha kuridhisha. Kwa sasa ni mita za ujazo 691.95. tunategemea mwezi Machi mvua zinyeshe pamoja na mwanzoni mwa Aprili,” anasema Mhando.

Kiwango hicho kimetofautiana kidogo na kile kilichotokana na uchunguzi wetu ambacho ni 691.73, kilichopatikana Januari 28, mwaka huu.

“Ni kweli hizo mita za ujazo 691 zinaweza kuzalisha umeme kwa miezi hiyo miwili tu,” anasema.

Kuhusu upungufu wa gesi ya Songosongo, Mhando anasema: “Kiwango cha upatikanaji gesi kutoka Songosongo inayosafirishwa kwa mabomba hadiDar es Salaam ni kweli kilipungua.

“Upungufu huo ulitokana na ukarabati uliokuwa ukifanyika huko na matengenezo yalichukua mwezi mzima, lakini tangu Januari 25 hali imerudi ya kawaida.

Alisema kampuni ya Pan African Energy inayozalisha gesi hiyo na kuisafirisha, imelihakikishia TANESCO kiwango cha gesi kitakuwa kikipatikana katika hali ya kawaida.

Kuhusu kiwango cha gesi kushindwa kukidhi mahitaji kama vituo zaidi vya kuzalisha umeme kwa gesi vitaanzishwa alisema : “Ni kweli kiwango cha sasa hakitatosheleza kama itaanzishwa mitambo mipya tofauti na ya sasa.

Vipi kuhusu mradi wa Kiwira?

Kuhusu mradi wa Kiwira, Mhando anasema serikali inakusudia kuukabidhi mradi huo kwa TANESCO itakayoshirikiana na TAMICO ili kuzalisha umeme.

Alisema mradi huo utaendeshwa kwa fedha za mkopo, akijibainisha kuwa kwa sasa hali ya kifedha ndani ya TANESCO si ya hasara kama ilivyokuwa awali.

“Awali, mwaka 2006 tulikuwa na hasara ya takriban Sh bilioni 168, lakini sasa hasara imepungua hadi Sh bilioni tano na inazidikupungua...tunaweza kuvunja rekodi sasa na kwa hiyo tunaweza kukopeshena na wadau wengine, ikiwamo Benki ya Dunia,” alisema Mhando.

Kauli ya Waziri Ngeleja

Raia Mwema iliwasiliana na Waziri wa Nishati na Madini, William Ngeleja, ambaye naye alikiri kuwa hali ya umeme si nzuri na kwamba Mtera inaweza kuzalisha umeme wa miezi miwili tu.

“Ni kweli kiwango cha maji Mtera kinaweza kuzalisha umeme wa miezi miwili tu ijayo kama mvua haitanyesha,” alisema Ngeleja.

Kuhusu kusafirishwa kwa kiwango cha kutosha cha gesi kutoka Songosongo, alisema upanuzi wa miundombinu utafanyika kama ambavyo kampuni ya Pan African Energy ilivyoahidi.

“Kuhusu suala la gesi ya Songosongo, kuna kitu kinaitwa ‘re-rating’ ambacho ni kama upanuzi wa miundombinu ya kusafirisha gesi inayofanywa na kampuni ya Pan-African Energy.

“Bwawa la Mtera hali si nzuri lakini kuna dalili za mvua na naambiwa maji yameanza kuingia kidogo kutokana na mvua zilizonyesha kidogo. Unajua, bwawa hili linajazwa na maji kutoka mikoa ya Singida, Dodoma na Iringa.

“Kiwira, uzalishaji utaanza baada ya miezi 20, na Kinyerezi katika miaka miwili na nusu kuanzia sasa na Artmus itakayozalisha Mw300.

Akizungumzia hali ya IPTL kukosa fedha kwa ajili ya ununuzi wa mafuta ya kuendesha mitambo hiyo na hivyo kupunguza mgawo nchini alisema mitambo hiyo itaanza uzalishaji wakati wowote baada ya mafuta kupatikana.

Mamlaka ya Hali ya Hewa

Kaimu Mkurugenzi wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA), Dk. Emmanuel Mpeta, aliieleza Raia Mwema kuwa, kunyesha kwa mvua mwezi Machi, mwaka huu kutategemea na mwenendo wa hali ya hewa.

“Hatutarajii mvua mwezi huu, pengine hadi Machi ambapo mifumo ya mvua inakuwa imesogea kutoka kusini,” alisema.

Ofisa mmoja wa TANESCO ameliambia Raia Mwema kwamba mvua zinazotarajiwa kunyesha kati ya Machi na Mei, hunyesha katika baadhi ya maeneo ya nchi na kwamba hata zikiwa za kutosha zinaweza zisisaidie sana mabwawa ya kuzalisha umeme kwa kuwa huwa zinawahi kukatika katika maeneo hayo.

Anasema kawaida Januari huwa kina cha maji kinapanda, lakini mwaka huu kimeshuka katika mabwawa ya Mtera na Kihansi. Taarifa zinaeleza kwamba hali itakuwa mbaya zaidi katikati ya mwaka huu.

Chanzo: www.raiamwema.co.tz

No comments: