Friday, February 4, 2011

Migogoro ya ardhi yakwamisha elimu Kisarawe

Picha hii ni jengo (madarasa na ofisi) la shule ya Msingi Tondoroni iliyopo kata ya Kiluvya wilayani Kisarawe, picha hii ilipigwa mnamo mwezi Novemba mwaka 2010 wakati wa utafiti uliofanywa na Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP).

  • Serikali yakifuta kijiji ,wananchi watakiwa kondoka
  • Wanafunzi wanatembea kilomita zaidi ya 10 kufuata shule

Halmashauri ya wilaya ya Kisarawe ni moja ya wilaya zinazokumbwa na tatizo la migogoro ya ardhi kwa kiasi kikubwa hapa nchini pamoja na kuwa ina eneo kubwa la ardhi linaloonekana kutokutumika.

Pamoja na kuwepo kwa eneo kubwa la ardhi ambalo halitumiki bado sehemu kubwa inagombaniwa kwaajili ya makazi ya watu binafsi, na shughuli nyingine.
Kwa mujibu wa uchunguzi uliofanywa, eneo kubwa la ardhi ya Kisarawe, hivi sasa linamilikiwa na wafanyabiashara wakubwa, ambao wanamiliki zaidi ya hekta 500 kwa mtu mmoja, taasisi za kiserikali kama vile Jeshi la wananchi(JWTZ),Shirika la Elimu Kibaha, Shirika la Umeme (Tanesco) na Wakala wa Taifa wa Barabara (Tanroads).

Kutokana na sehemu ya eneo kubwa la ardhi kuchukuliwa na taasisi hizo, sehemu ndogo inayobaki imeibua migogoro mikubwa ya ardhi na kusababisha vurugu, chuki na uhasama kati ya wananchi na wanajeshi.

Tayari wananchi wa kijiji cha Mloganzila na Tondoroni wameenza kujega uhasama na chuki didhi ya jeshi na serikali, wakidai kuwa wanawanyanyaswa, na kudhulumiwa ardhi yao ikiwemo shule yao ya msingi.

Sekta ya elimu ndiyo inayoadhirika zaidi kwa kiasi kikubwa kutokana na kukosekana kwa maeneo ya kujenga madarasa, shule mpya, na hata nyumba za walimu.
Moja ya kata yenye changamoto kubwa ya ardhi ni kata ya Kiluvya katika vijiji vya Tondoroni, Mloganziala, na Kiluvya A na B.

Vijiji hivi kila kimoja kinakabiliwa na tatizo la ardhi. Moja ya kijiji ambacho kimeadhirika zaidi ni Tondoroni, ambacho shule ya msingi Tondoroni, imelazimika kufutwa kabisa kutokana na tatizo la ardhi. Eneo lote la ardhi ya kijiji cha Tondoroni, limekuwa eneo la jeshi, na kulazimika kuifunga shule hiyo.

Shule ya ya msingi Tondoroni iliyojengwa mwaka 1980 ilikuwa shule ya kwanza kujengwa katika kata hiyo, na kusajiliwa na Wizara ya Elimu kwa namba PW 54-02-42, lakini hivi sasa bado imejengwa kwa miti na kizibwa kwa tope.

Afisa Mtendaji wa kijiji cha Tondoroni Lister Bunzu, anaeleza kuwa shule hiyo ilijengwa kwa nguvu za wananchi lakini, ikasajiliwa ikiwa na walimu wawili tu na madarasa saba wakati huo.
Bunzu anasema wananchi wameshangaa kusikia serikali ikitoa tangazo la kuifuta shule hiyo na kuwahamishia wanafunzi shule za jirani badala ya kuiboresha.

“Sisi tulifikiri kuwa serikali ingechukua jukumu la kuijenga upya hii shule, lakini imeamua kuifuta kwa sababu kuwa eneo hili limepewa jeshi, yaani sisi wananchi hatuna haki tena na shule yetu tuliyoijenga, ardhi anapewa mtu na shule yetu inafutwa,”anasema Bunzu.
“Hatukatai serikali kulipa jeshi ardhi, sisi tunataka utaratibu ufuatwe na wananchi wanaokutwa wakimikili ardhi wapewe haki zao stahili. Shule yetu iliyopo hapa iendelee, siyo kufutwa,”anaongeza Mtendaji huyo.

Wanafunzi zaidi ya 250 waliokuwa wakisoma katika shule ya Tondoroni kwa sasa wamehamishiwa shule za msingi, Visegese,Chanziga,Kiluivya A na B, na Mloganzila.
Kwa sasa baadhi ya wanafunzi kuanzia wa darasa la kwanza hadi la saba wanaohamishwa kutoka katika shule hiyo watapaswa kutembea umbali wa kilomita zaidi ya saba hadi 18 kwa siku ili kufika shuleni.

Tatizo kubwa ambalo linaonekana na ni changamoto kwa watoto wadogo wanaokwenda shule ni suala la umbali kwasababu mazingira ya vijiji hivyo ni pori, watoto hao wanapaswa kukatiza maeneo ya porini, kuzifikia shule.
Bunzu anasema: “hapa watoto wetu wenye umri mdogo wamekwama, wale wenye umri wa miaka saba hadi 10. wanasubiri nyumbani, wakifika miaka 11 hadi 14, ndiyo wanaoweza kumudu umbali na kukatiza porini ili kwenda shuleni,”

Kwa mujibu wa Barua ya Halmashauri ya Wilaya ya Kisarawe ya iliyoandikwa kwa wananchi wa Tondoroni Machi 10,2009, ya kuifunga shule hiyo, imeeleza kuwa shule hiyo imefutwa kutokana na tatizo la ubovu wa majengo yake.
Mwanaisha Kassimu (7), ni mmoja wa wanafunzi wanaosoma shule ya msingi Visegese, anatembea kilomita nne kwenda shule tu akikatiza katika eneo la kijiji cha jirani, kutokana na shule yake ya awali ya Tondoroni kufutwa.
“Shule yangu ipo katika kijijni cha jirani, ninatembea saa mbili kuitafuta shule, wakati mwingine siendi kwasababu kuna nyoka, na unatemebea porini mwenyewe,”anasema Mwanaisha.
Adelina Mathias Mbowetu, ni mwalimu wa kwanza wa shule hii, aliyeanza kazi shuleni hapo mwaka 1980, yeye anaelezea jinsi walivyoianzisha shule hiyo na ilivyokuwa muhimu wakati huo.
Anasema kuwa wakati huo walikuwa walimu wawili, yeye na mwingine ambaye alimtaja kwa jina moja la marehemu Mwamvita, na shule ilikuwa msaada mkubwa kwa wananchi wa Kiluvya kutokana na kuwa shule pekee katika kata hiyo.

“Nimeingia katika kijiji hiki mwaka 1980, nikiwa nimehitimu masomo, nikaamua kufanya kazi hapa mazingira yalikuwa ya kujitolea zaidi, tulikuwa walimu wawili tu, lakini hatukukata tamaa, tumefundisha, tukitegemea kuwa shule hii ingeboreshwa lakini hadi nimehama na hata kufikia kustaafu miaka 30 baadaye shule imebakia vilevile,”anasema Mwalimu Adelina ambaye amestaafu sasa.

Afisa Mtendaji wa kata ya Kiluvya, Godfrey Lamecky, anasema kuwa eneo yeye hana taarifa kama kijiji cha Tondoroni kimefutwa na na kama hakijafutwa rasmi shule hiypo ingepaswa kuendelea kuwepo.
Lamecky anasema kuwa kata yake imekuwa na kesi nyingi za ardhi ikiwepo migogoro inayotokana na ukosefu wa ardhi kwasababu watu wachache au taasisi kujichukulia maeneo ya wananchi.

“Hapa kuna migogoro mingi, badhi ya kesi zipo kwenye baraza la ardhi la kata, na nyingine mahakama kuu kitengo cha ardhi, hii inatokana ana mgawanyo wa ardhi ambao kwa baadhi ya maeneo haukuzingatia sheria na taratibu,”anasema.

Kauli ya Mtendaji huyo, inaungwa mkono na Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauiri ya Kisarawe, Isaya Moses, anayesema kuwa mgawanyo wa ardhi katika wilaya yake haukuzingatia taratibu na sasa anaanza operesheni ya kupitia upya taratibu zinazotumika.
Kuhusu Shule hiyo ya Tondoroni, Moses anasema serikali imeifuta shule hiyo na wanafunzi watapaswa kufuata maagizo ya serikali kwa kuhamia katika shule walizohamishiwa.
“Nikueleze ukweli, shule hii imefutwa, haruhusiwi mtu yoyote kutumia majengo ya shulke hiyo, akikutwa mtu pale sisi tutamkamata,”anasema Isaya.
Migogoro ya ardhi kwa kiasi kikubwa inakwamisha ari ya wananchi ya kuchangia elimu kwasababu wanaona kuwa hakuna haja ya kujenga shule ambazo zipo mbali na makazi yao na watoto wao hawataweza kusoma kutokana na umbali.

Kutokana na kufutwa kwa kujiji hicho kinyemela wananchi wa Tondoroni hivi sasa hawana huduma za msingi za kijamii, kama vile afya, maji, elimu, chakula kutokana na kukatazwa kuliendeleza eneo hilo.

Akizungumza kwa uchungu, Afisa Mtendaji wa Kijiji hicho, Lister Bunzu, alisema anashangaa kuambiwa kuwa kijiji hicho kimefutwa wakati yeye na wananchi wake hawajawahi kupewa barua ya kufutwa kwa kijiji.
“Tondoroni ni kijiji cha siku nyingi, tulijenga shule yetu ya msingi hapa mwaka 1980, na mwaka 1986 kijiji hiki kiliandikishwa na serikali. Mwaka 1992 kijiji chetu kilipewa hati ya usajili kutoka serikalini, na hati hiyo tunayo hadi leo, haijafutwa,”alisema Bunzu.

Bunzu amesema mgogoro huo umesababishwa na serikali ya Wilaya kushindwa kuwatetea wananchi wake wakati Jeshi linapotaka kukichukua kijiji hicho, kwani wananchi wanishi hapo kihalali, na walipaswa kupewa eneo lingine la kuishi na kulipwa fidia ikiwepo kupewa barua rasmi ya kukifuta kijiji hicho.

Kwa Mujibu wa hati ya Usajili wa kijiji hicho, Kijiji kiliandikishwa kwa hati namba PW/KIJ/539. Chini ya sheria namba 7 ya mwaka 1982 chini ya kifungu namba 22(sheria ya serikali za mitaa na mamlaka ya Wilaya) na kutolewa septemba 14,1993.
Akizungumzia saula hilo, Mtandaji wa kata ya Kiluvya, Godfrey Lamecky, alisema yeye hana taarifa za kufutwa kwa kijiji hicho kwani hajawahi kuona barua kutoka serikalini ya kukifuta kijiji licha ya kuona hati ya usajili wa kijiji.
“Mimi ninashangaa ninaposikia kuwa kijiji kimefutwa, kwasababu nimeingia katika ofisi hii sikukukuta barua, na sijawahi kupewa, sasa mimi mnataka niseme uongo kuwa kijiji kimefutwa wakati sina ushahidi?

“Nimeuliza katika vikao vya halmashauri juu ya kijiji hicho, tena cha kushangaza bado tunapeleka huduma pale, kama vile vyandarua vya mbu tumegawa pale juzi, kuna afisa kilimo na mifugo ambaye analipwa na halmashauri, na kuna tawi la Chama cha Mapinduzi(CCM) na wanapiga kura za maoni” aliongeza Lamecky.

Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Kisarawe, Isaya Moses, alisema yeye hakitambui kijiji hicho na yeye kama msimamizi mkuu wa uchaguzi wa jimbo hilo, hataweka kituo cha kupiga kura katika kijiji hicho.
“Mimi sikitambui kile kijiji, watu wamelipwa wanatakiwa kuondoka kama hawataondoka pale sisi tutawakamata, lile ni eneo la jeshi. Nimesema tena serikali imeshakifuta kijiji hicho” alisema Moses

Alipoulizwa kama ofisi yake imeandika barua ya kukifuta kijiji hicho kwa uongozi wa ngazi za chini na wanakijiji alisema “ kwakweli sijui kama wamepewa barua ya kufutwa kijiji, lakini ninakiri kuwa mimi sijawaandikia, kama hawana barua ni makosa yalifanyika huko nyuma. Lakini sikitambui kijiji hicho!” alimalizia Mkurugenzi huyo.

Alipotakiwa kulitaja aneo mbadala ambalo limetengwa kwajili ya wananchi hao, ili kulipisha jeshi, alisema yeye hajui kama eneo mbadala lilitengwa kwaajili ya wananchi, ila anaamini kuwa walioanza kuwahamisha watakuwa waliandaa sehemu nyingine.
“ Nafikiri waliofanya wakati huo, watakuwa waliandaa eneo lingine, la kwenda lakini sina uhakika”alisema Moses.

Wakazi hao wamedai kuwa wamekuwa wakiishi katika maeneo hayo tangu mwaka 1976.
Agizo la kuondoka kwa wananchi hao lilitolewa na uongozi wa 83 KJ kilichopo wilayani humo na Mkuu wa Wilaya ya Kisarawe Halfa Karamagi.

Naye mkazi mwingine wa kijiji cha Mloganzila, Bi. Asha Shomari (80), alisema kitendo kinachofanywa na wanajeshi hao ni ukatili kwani yeye alianza kuishi hapo tangu akiwa msichana na hajawahi kulipwa fidia wala kuambiwa hatakiwi kukaa hapo.

Anasema katika jambo hilo, lazima serikali iingilie kati kwani na wao ni Watanzania sawa na wengine hivyo wanahitaji haki ya kulindwa wao na mali zao.
Amesema kuwa mwaka 1986 Wilaya ya Kisarawe ilitangaza kuwalipa fidia lakini walipokwenda wengine waliambulia Sh. 2,000 zikiwa ndani ya habasha ambapo wengi wao walizikataa.
Amefafanua kuwa, wananchi wengi walipofika njiani na wengine nyumbani, walichokikuta hawakuamini.

No comments: