Tuesday, February 15, 2011

Serikali yaeleza mikakati upatikanaji maji

SERIKALI imewasilisha bungeni kauli ikielezea mikakati mbalimbali iliyochukuliwa na inayoendelea kuchukuliwa katika kutekeleza miradi ya maji nchini.

Katika mikakati hiyo, upo ule unaofadhiliwa na mfanyabiashara maarufu nchini, Mustafa Sabodo wa kutoa fedha ili kuchimba visima 700 nchini kote isipokuwa katika Jiji la Dar es Salaam.

Waziri wa Maji, Profesa Mark Mwandosya, aliliambia Bunge mjini hapa Februari 14 kwamba mikakati hiyo inalenga katika kuboresha upatikanaji wa maji katika maeneo mbalimbali nchini yakiwemo maeneo ya vijijini.

Alisema hivi sasa Serikali ipo katika utekelezaji wa miradi mipya ya maji ambayo itagharimu dola za Marekani milioni 951, zitakazotokana na fedha za Serikali na wafadhili mbalimbali wakiwemo Benki ya Dunia.

Alisema Serikali imesimamia kwa ukaribu utekelezaji wa Programu ya Maji Vijijini ya mwaka 1971 hadi 1991 ambapo miradi 20 ya maji ilijengwa na Serikali.

Alisema ili kuona kama utekelezaji wa miradi ya maji inaleta ufanisi, Serikali ililazimika kuifanyia tathmini Sera ya Maji ya mwaka 1991, tathmini ambayo ilifanyika mwaka 1997 na kufanya Serikali kuunda Sera nyingine ya Maji ya mwaka 2002, ambapo miradi ya maji iliwekewa mikakati bora zaidi ya utekelezaji.

Alisema msukumo mwingine uliwekwa katika programu ya maji ya miaka 25 ambayo utekelezaji wake ulianza mwaka 2006 na utaendelea hadi mwaka 2025, ambapo miradi mbalimbali ya maji imeainishwa na kuanza utekelezaji wake ili kuboresha hali ya upatikanaji wa maji.

Alisema hata hivyo msukumo mkubwa umekuwa katika miradi ya maji yenye uwezo wa kutoa matokeo ya haraka ambapo miradi 2024 imeweza kutekelezwa na hivyo kuwafanya wananchi milioni 2 kupata maji.

“Pamoja na miradi mingine ya maji, upo mradi ambao utafadhiliwa na mfanyabiashara Mustafa Sabodo ambaye yeye ataisaidia Serikali kuchimba visima 700, nchini kote isipokuwa Dar es Salaam, hatua ambayo itawezesha wananchi zaidi kupata maji safi na salama," alisema Profesa Mwandosya.

No comments: