Monday, February 7, 2011

Mfumo wa Bodi ya Mikopo kubadilishwa

RAIS Jakaya Kikwete ameteua tume ya wataalamu 11 kufanya mapitio ya mfumo wa uendeshaji wa Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu (HLSLB) kwa lengo la kuboresha utoaji wa mikopo.

Katika hadidu za rejea, tume hiyo imeagizwa kuangalia upya vigezo na sifa zinazozingatiwa katika utoaji wa mkopo endapo vinakidhi haja na mahitaji halisi ya waombaji na taifa kulingana na makusudio ya kuundwa kwa bodi hiyo.

Kabla ya kuangalia vigezo hivyo, tume hiyo imeagizwa kuchambua kwa kina Sheria iliyounda bodi hiyo na kanuni zake na kubainisha vifungu vinavyohitaji marekebisho kulingana na hali halisi ya utoaji mkopo.

Akizungumza mkoani hapa jana, Waziri Mkuu Mizengo Pinda alisema tume hiyo imetakiwa kufanya kazi kwa muda wa siku 60 kuanzia Februari 14 mwaka huu na kuwasilisha ripoti yake kwa Katibu Mkuu Kiongozi, Philemon Luhanjo Aprili 15, mwaka huu.

Alisema pia imeagizwa kuangalia kwa kina muundo wa bodi na ufanisi wake katika utoaji na urejeshwaji wa mikopo na kutoa mapendekezo.

Mbali na muundo pia imetakiwa kuchunguza kiini cha malalamiko na uhusiano usioridhisha kati ya bodi na wanafunzi, bodi na taasisi ya elimu ya juu na kati ya bodi na Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi na katika mapendekezo, yawepo ya namna ya kurejesha uhusiano mzuri.

Katika kufanya kazi yao wajumbe wa bodi hiyo wameagizwa kuangalia nchi nyingine zenye mazingira kama ya Tanzania zilizofanikiwa kugharimia elimu ya juu kwa mfumo wa mikopo. Lengo lake ni kuwezesha mikopo itolewe kwa wanafunzi wengi wahitaji wa elimu ya juu bila lawama na kuboresha mfumo huo kwa kadiri inavyoonekana inafaa.

Hatua hiyo ya Serikali, imechukuliwa kukiwa na shinikizo kutoka kwa Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM), wa kuipindua au kuivunja bodi hiyo na kuundwa upya.

Shinikizo hilo la UVCCM, lililotolewa na Kamati ya Utekelezaji ya Baraza Kuu la umoja huo wakidai ndio suluhisho la migomo iliyokuwa ikilipuka kutoka katika vyuo vikuu zaidi ya 10 sasa huku kero kuu ikiwa kucheleweshewa mikopo.

Hata hivyo, uundwaji wa tume hiyo, ambao uliahidiwa na Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Dk. Shukuru Kawambwa mara tu alipofanya ziara ya kwanza kutembelea bodi hiyo, umeonekana kutofuata shinikizo hilo la UVCCM.

Mbali na ahadi hiyo, hata tamko la bodi hiyo lililotolewa siku chache baada ya tamko la UVCCM kutaka ipinduliwe, lilieleza kuwa changamoto iko katika mfumo na kwamba hata ikivunjwa, watakaorithi mfumo huo watakumbana na changamoto hiyo hiyo.

Katika tamko hilo la HELSB, ambalo lilitamka wazi kwamba UVCCM walikurupuka, bodi hiyo ililaumu Tume ya Vyuo Vikuu (TCU) na menejimenti za vyuo husika kwa kuchelewesha majina ya wanafunzi wanaopaswa kupewa mikopo.

Hata hivyo, UVCCM katika moja ya malalamiko yaliyokuwepo katika shinikizo hilo, lilikuwepo la mtindo wa bodi hiyo kupeleka fedha za wanafunzi hao kwa uongozi wa vyuo badala ya akaunti binafsi za wanafunzi.

Malalamiko hayo ya kutupiana lawama yameonekana kuzingatiwa, kwani wataalamu wa tume hiyo ya Rais, wamechaguliwa kwa uwakilishi kuunda sura ya Muungano na kutoka menejimenti za vyuo vikuu vya umma na binafsi na TCU zilizolalamikiwa na bodi.

Pia wapo wawakili wa serikali za wanafunzi, Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi, wahadhiri na wataalamu wa benki na kutoka kwa wadau wengine wa elimu zikiwemo asasi za jamii.

Kati ya wajumbe hao yupo Mwenyekiti ambaye ni Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) anayehusika na Taaluma, Profesa Makenya Maboko na Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Waislamu Morogoro, Kassim Almas Umba anayehusika na Utawala wa Fedha.

Pia yupo Ofisa Uhusiano wa Kimataifa wa Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Zanzibar, Masoud Mohamed Haji na Mhadhiri Mwandamizi wa elimu kutoka Chuo Kikuu cha Tumaini Arusha, Dk. Eliawony Meena.

Wengine ni Naibu Katibu Mkuu TCU, Daniel Magwiza, Mkurugenzi Msaidizi (Uandishi Sheria) kutoka Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali Sarah Baharamoka na Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi Inayopigania Elimu kwa Wanawake tawi la Tanzania, Profesa Penina Mlama.

Wengine ni Ofisa Taaluma Chuo cha Usimamizi wa Fedha, Deo Daudi ambaye alikuwa Rais wa Serikali ya Wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (Daruso) kwa mwaka 2006/2007.

Rais pia amemteua katika bodi hiyo Mkurugenzi wa Mikopo Benki ya CRDB, Anderson Mlambwa, Mkurugenzi wa Elimu ya Juu, Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Profesa Wilbert Abel na Mkurugenzi Mkuu Mamlaka ya Elimu Tanzania, Rosemary Rulabuka.

No comments: