Tuesday, January 24, 2012

Aita wake zake wawili , amuua mmoja kwa kisu

MKAZI wa Kijiji cha Busilima wilayani Musoma Vijijini katika Mkoa wa Mara, Anna Mfungo (26) ameuawa kwa kuchomwa kisu shingoni na mume wake, Shukrani Shaban (32) baada ya kudai kuwa ameoteshwa atapelekwa Polisi.

Kamanda wa Polisi wa Mkoa, Robert Boaz alisema Shaban alimuua mkewe Jumamosi iliyopita saa 7 usiku baada ya mtuhumiwa huyo kutoka kwenye ulevi.

Kwa mujibu wa madai ya Kamanda Boaz, Shaban alipofika nyumbani kwake usiku huo, aliwaamsha wake zake wote pamoja na kijana mmoja ambaye alikuwa anaishi naye na kuwaambia aliota kuwa atapelekwa Polisi.

“Mtuhumiwa ni mvuvi na anafanya kazi zake huko Busekela na anakaa hata siku tatu ndipo anarudi nyumbani.

“Anapokuwa nyumbani akitoka kwenye ulevi anawaamsha wake zake wote wawili, wanamletea chakula na akimaliza ndipo wanapotawanyike na kwenda kulala,” alidai Kamanda Boaz.

Alidai kuwa Jumamosi iliyopita, ilikuwa zamu ya mke mkubwa na mtuhumiwa aliporudi kwenye ulevi kama kawaida yake aliwaamsha pamoja na mke kijana ambaye alikuwa anaishi naye na kuwaambia kuwa alikuwa ameota atapelekwa Polisi na kisha kuchukua kisu na kumchoma shingoni mwanamke huyo,” alidai Kamanda Boaz.

Alidai kuwa baada ya kutenda kosa hilo, kijana huyo alikimbia na kutoka nje kuomba msaada lakini watu walipofika, mtuhumiwa alikuwa tayari ameshatoroka na jitihada za kumtafuta zinaendelea.

Wakati huo huo mtoto Emmanuel Joseph (5), alikufa baada ya kamba waliyokuwa wakiitumia kama bembea kumkaba shingoni na kumsababishia kifo.

Kamanda Boaz alisema kuwa ajali hiyo lilitokea Jumapili iliyopita katika Kijiji cha Kabainja wilayani Bunda ambapo Emmanuel na watoto wenzake walikuwa wakibembea.

No comments: