Thursday, October 13, 2011

Waziri Mkulo akumbwa na kashfa

AVUNJA BODI YA CHC KABLA HAIJAPOKEA RIPOTI YA UFISADI KUTOKA KWA CAG, ZITTO KUZUNGUMZA LEO

WAZIRI wa Fedha na Uchumi, Mustafa Mkulo ameivunja Bodi ya Wakurugenzi ya Shirika Hodhi la Mashirika ya Umma (CHC), wakati ambao bodi hiyo ilikuwa ikisubiri kupokea ripoti ya ukaguzi uliofanywa na Ofisi ya Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), ukilenga kubaini tuhuma za kuwapo kwa ufisadi katika shirika hilo.

Msingi wa uchunguzi ndani ya CHC, ni maombi ya Bodi ya shirika hilo hodhi kwa CAG, kufuatia kuwapo kwa tuhuma kwamba menejimenti yake ilihusika na vitendo vya ufisadi, hivyo kusababisha kusimamishwa kwa Kaimu Mkurugenzi wake, Methusela Mbajo.

Ofisi ya CAG ilifanya uchunguzi kwa kutumia kampuni ya kimataifa ya ukaguzi wa hesabu ya Ernst&Young, ukaguzi ambao pia ulilenga kubaini tuhuma dhidi ya Kamati ya Bunge ya Hesabu za Mashirika ya Umma (POAC), inayoongozwa na Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe.

Katika Mkutano wa Nne wa Bunge, Mkulo aliingia katika mvutano na Zitto baada ya waziri huyo kumtuhumu mbunge huyo na Kamati yake kwamba walihongwa ili kutetea nyongeza ya muda wa CHC, tofauti na mawazo ya Serikali ya kutaka kufutwa kwa shirika hilo.

Baada ya tuhuma hizo, Zitto aliapa bungeni kwamba kama uchunguzi utathibitisha yeye au wajumbe wa POAC wamehongwa, angejiuzulu uenyekiti na ubunge na kumtaka Waziri Mkulo nae atoe kiapo chake bungeni kama atajiuzulu akibainika amefanya ufisadi ndani ya CHC.

Mkulo akijibu swali hilo alishindwa kula kiapo na Spika wa Bunge, Anne Makinda akamkumbusha kuhusu kula kiapo kama atajiuzulu, lakini waziri huyo aligoma kufanya hivyo.

Lakini wakati CAG akiwa katika hatua za mwisho kukamilisha ripoti yake ambayo kimsingi ilipaswa kukabidhiwa kwa bodi ya CHC, uchunguzi wa Mwananchi umebaini kuwa Mkulo amevunja bodi hiyo kabla ya kumaliza muda wake wa nyongeza ambao ulipaswa kumalizika Desemba 31, mwaka huu.

Uhai wa Bodi ya CHC
Awali bodi ya CHC ilikuwa imalize muda wake Juni 30 mwaka huu, lakini Mkulo aliiongezea muda hadi Desemba 31, mwaka huu na barua ya hatua hiyo ilitumwa kwa wajumbe wa bodi hiyo kuwajulisha hatua hiyo ya waziri Julai 29, 2011.

Hata hivyo, ghafla Mkulo alibadili uamuzi wake Oktoba 10, 2011, kwa kumwandikia Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa CHC kwamba awaarifu wajumbe wa bodi kuhusu uamuzi huo.

Sehemu ya barua kutoka Wizara ya Fedha kwenda CHC ambayo Mwananchi imeiona inaeleza: “Nimeelekezwa nikuarifu kwamba Waziri wa Fedha, Mh. Mustafa H. Mkulo (Mb), ametengua uamuzi wake wa kuongeza muda wa Bodi ya CHC hadi tarehe 31 Desemba, 2011 au hapo Rais atakapoteua Mwenyekiti wa Bodi hiyo kuanzia tarehe ya barua hii (10, Oktoba, 2011).”

Barua hiyo iliyosainiwa kwa niaba ya Katibu Mkuu Hazina na Geoffrey Msella pia inasema; “Kwa barua hii unatakiwa kuwaandikia barua waliokuwa Wajumbe wa Bodi ukiwashukuru kwa michango yao kwa Shirika hili katika kipindi walichotumikia CHC.”

Kufuatia barua hiyo, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa CHC, Dome Malosha siku hiyo hiyo ya Oktoba 10, 2011 aliwaandikia barua wajumbe hao wa Bodi akiwaarifu kuhusu uamuzi wa Waziri Mkulo kuvunja bodi hiyo.

Ukaguzi wa CAG
Uchunguzi wa Mwananchi umebiani kuwa hatua ya Mkulo kuvunja bodi ya CHC ilifanyika muda mfupi tu, tangu alipojibu hoja za Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali, Ludovick Utuoh kuhusu kile ambacho kinaonekana kuwa ni matokeo ya awali ya ukaguzi uliofanywa na Ernst & Young.

Uchunguzi wetu unaonyesha kuwa kulikuwa na mawasiliano baina ya Mkulo na Utouh kati ya Oktoba 6 na 8, 2011, na baadaye kuvunjwa kwa bodi Oktoba 10.

Oktoba 8, 2011, Mkulo alimwandikia barua Utouh akikanusha kwamba hahusiki na ufisadi wowote ndani ya CHC, kauli inayothibitisha kwamba alitajwa katika taarifa yake hiyo.

Katika barua hiyo ambayo pia Mwananchi imeiona, Mkulo anakanusha kile alichosema kuwa ni tuhuma za kuhusishwa na uuzwaji wa mali za CHC kinyume cha sheria.

Barua hiyo ya Mkulo kwenda kwa CAG ina kumbukumbu Namba TYC/B/70/03 na kichwa cha habari, YAH: UKAGUZI WA CONSOLIDATED HOLDING CORPORATION ikirejea mazungumzo ya simu baina ya viongozi hao wawili Oktoba 7, mwaka huu, pia ujumbe mfupi wa simu kutoka kwa Utouh kwenda kwa Mkulo Oktoba 6, 2011.

Soma zaidi

No comments: