Monday, March 14, 2011

Weza yanufaisha wanawake 7,686 Zanzibar

Wanawake 7,686 wanaonufaika na mradi wa kuwawezesha Wanawake Zanzibar(Weza) wameanza kuchukua hatua za pamoja katika kutatua matatizo yao yakiwemo ukatili wa kijinsia na upatikanaji wa huduma muhimu.

Wanawake kutoka Shehia ya Mgogoni walisema wamechanga Sh. 480,000 na kuchimba kisima ambacho hivi sasa ndicho kinachotumiwa Shehia nzima kupata maji safi.

Wanawake hao waliyabainisha hayo walipotembelewa na wataalamu wa jinsia na maendeleo kutoka Umoja wa Ulaya (EU) na Care Austria hivi karibuni.

Wanawake hao kutoka Shehia za Mchangani Unguja Kusini, Mtambwe Kaskazini, Mgogoni na Kisiwani Kaskazini Pemba wamesema wenyewe wameweza kufuatilia kesi za udhalilishaji na ukatili dhidi ya wanawake na watoto katika ngazi tofauti ambapo baadhi zimefanikiwa kuchukuliwa hatua zinazostahili.

Fatma Said (29) wa Shehia ya Mgogoni alisema yeye alijenga nyumba yake aliyoishi na mumewe, lakini baadaye mume wake alimuacha na kumfukuza ndani ya nyumba hiyo.

Amesema kwa kusaidiana na wanawake wenzake walifuata taratibu za kisheria na iliposhindikana kupata haki ya nyumba yake mahakamani walikwenda Wizara ya Wanawake na Watoto Pemba ambapo iliamuliwa arejeshewe nyumba yake.

Alisema hata hivyo baadaye alimuomba kumrejea na hivi sasa wameoana tena na wanaishi pamoja.

Naye Mratibu wa Shehia ya Mchangani, Nawaje Mussa, alisema hivi karibuni wamesimamia kesi ya msichana ambaye alipewa ujauzito kuhakikisha kuwa anarejea shuleni badala ya kuolewa kama baadhi ya wazee wake walivyopanga kufanya.

Wanawake wa Mtambwe kaskazini wamesema wameweza kushughulikia kesi sita zinazohusiana na ukatili dhidi ya wanawake na watoto ambazo baadhi ziko mahakamani.

Mmoja wa wanaharakati wanaotetea haki za wanawake na watoto Pemba, Jaria Hamad amesema kesi hizo zinahusu wanawake kupigwa, ubakaji na mimba za utotoni.

No comments: