Tuesday, March 8, 2011

Wanawake, tujikwamue na changamoto zinazotukabili

LEO duniani kote wanaadhimisha Siku ya Wanawake, lakini pia ni siku muhimu kwa kuwa siku hiyo pia inatimiza miaka 100 tangu kuanzishwa kwake.

Kwa Tanzania kama zilivyo nchi nyingine, leo wanaungana na wenzao kuadhimisha siku hiyo ambayo hutumiwa kwa ajili ya kuhamasisha juu ya haki za mwanamke lakini pia kuamsha hamasa kwa wanawake kushiriki katika shughuli mbalimbali za kisiasa, kiuchumi na hata kijamii.

Ukweli ni kwamba siku hiyo ni maalumu ambayo wanawake wengi wanaokosa nafasi ya kusikika hutumia fursa hiyo angalau kutoa kilio chao au kuonyesha mfano kwa wanawake wengine ambao bado wana uoga wa kujaribu.

Ni siku ambayo pia hutumika kutathmini jitihada zinazofanywa na taasisi na vyama mbalimbali vya wanawake pamoja na harakati za wanawake kuona kama jitihada hizo ama zimefanikiwa, kupunguza au zimeshindwa kutatua matatizo ya wanawake.

Kihistoria siku hiyo ilianza kuadhimishwa tangu mwaka 1911 wakati makundi ya wanawake nchini Marekani yalipokusanyika na kupinga udhalilishaji, ukandamizaji, uonevu na ubaguzi wa kijinsia hususani sehemu za kazi.

Kutokana na hamasa ya wanawake hao na matatizo mengi yaliyokuwa yakiwakabili wanawake
katika mataifa mbalimbali duniani, nchi nyingi nazo zilijiunga na kuteua siku moja ambayo ni Machi 8 ya kila mwaka kuadhimisha siku hiyo.

Na hiyo ilitokana na ukweli kuwa matatizo mengi yanayohusu wanawake katika nchi nyingi yalikuwa ama yakifanana au baadhi ya maeneo yalizidiana.

Hivyo hadi leo, maadhimisho hayo sasa yanatimiza miaka 100, huku bado wanawake wakiendelea kukabiliwa na changamoto nyingi ambazo bado zimelalia katika tatizo sugu la mfumo dume, bila kusahau matatizo ya uzazi ambayo yanaondoa duniani wanawake wengi huku wengine wakiachwa na magonjwa sugu.

Sasa wakati umefika kwa wanaharakati nchini lakini pia Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto, kuziangalia kwa karibu changamoto hizo na kuzichukulia hatua kwa vitendo na si kubaki na maneno jukwaani.

Tumekuwa tukisikia kila kukicha maneno ya kukemea vitendo vya kikatili kama vile unyanyasaji wa wanawake, ukeketaji kwa wanawake, vitendo vya kubakwa na ndoa za utotoni
na hata kufikia kuomba sheria ya ndoa kufanyiwa marekebisho huku bado matatizo hayo yakizidi kuendelea katika baadhi ya maeneo.

Sisemi kwamba hakuna mafanikio yoyote mpaka sasa, lakini ninachosisitiza ni hatua thabiti zinazoonekana kuchukuliwa dhidi ya matatizo hayo sugu hususani hilo la vifo vya akinamama
wajawazio ambalo bado ni mzigo.

Tuadhimishe siku hii, kwa wanawake wenyewe kuwa mstari wa mbele na kushirikiana kukabiliana na changamoto hizo, na jambo la msingi ni kuacha ubinafsi na kutopendana na
kuungana pale inapodi ndipo mafanikio yataonekana.

Katika kutatua matatizo makubwa na sugu yanayowakabili wanawake duniani kote na si Tanzania pekee, ushirikiano, umoja na upendo na kujituma kunatakiwa na si kuingiza siasa.

Imeandikwa na Halima Mlacha

No comments: