Monday, March 7, 2011

Maadhimisho Siku Ya Wanawake Duniani Machi 8

Siku ya Wanawake Duniani huadhimishwa na nchi wanachama wa Umoja wa Mataifa kila mwaka tarehe 8 Machi. Madhumuni ya Maadhimisho haya ni kupima utekelezaji wa maazimio, matamko na mikataba mbalimbali ya kimataifa inayohusu masuala ya wanawake. Aidha, madhumuni mahususi ni pamoja na:

• Kujenga mshikamano wa wanawake wote duniani.
• Kuweka msisitizo na kuhamasisha jamii kuhusu kaulimbiu ya kimataifa wakati wa
Maadhimisho ya kila mwaka
• Kuelimisha jamii kuhusu jitihada mbalimbali zilizofanywa na Serikali, asasi mbalimbali yakiwemo Mashirika Yasiyo ya Kiserikali katika kuwaendeleza wanawake.
• Kuhamasisha jamii kuhusu utekelezaji wa sera, mipango na ahadi mbalimbali za kudumisha “Amani, Usawa na Maendeleo”.

Vilevile, Maadhimisho haya hutoa fursa maalum kwa Taifa, Mikoa, Wilaya mashirika ya dini, vyama vya siasa, mashirika ya hiari, jamii na wanawake, kupima mafanikio yaliyofikiwa kimaendeleo na kubainisha changamoto zilizojitokeza katika kufikia azma ya ukombozi na maendeleo ya wanawake na hivyo kuweka mikakati ya kukabiliana na changamoto hizo.

Hapa nchini maadhimisho haya yalifanyika Kitaifa kuanzia mwaka 1997 hadi mwaka 2005 na baada ya hapo Serikali ilipitisha uamuzi kuwa yafanyike kila baada ya miaka mitano. Uamuzi huu ulipitishwa ili kutoa muda wa kutosha wa utekelezaji wa maazimio mbalimbali na kuweza kupima mafanikio ya utekelezaji wa shughuli hizo za kila baada ya miaka mitano.

Madhumuni ya kufanya maadhimisho hayo kila baada ya miaka mitano:-

1. Kutoa fursa kwa Serikali, vyama vya siasa, jamii na wadau wengine kuweza kupima mafanikio ya utekelezaji wa sera, mikakati na programu mbalimbali za kitaifa na kisekta.

2. Kubaini changamoto na kuweka mikakati ya kutatua changamoto zinazojitokeza.

Kwa kuzingatia uamuzi huo maadhimisho ngazi ya Kitaifa yalifanyika mwaka 2010, sambamba na maadhimisho ya miaka 15 ya utekelezaji wa Azimio na Ulingo wa Beijing, 1995. Maadhimisho haya yalifanyika Mkoani Tabora, na Mgeni rasmi akikuwa Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Hivyo maadhimisho haya kwa mwaka 2011 yataandaliwa katika ngazi ya mkoa, na kila mkoa umejiwekea utaratibu wa maadhimisho haya kwa kuzingatia ujumbe wa Kaulimbiu ya mwaka 2011.

Kaulimbiu ya Mwaka 2011
Kaulimbiu ya Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani kwa mwaka 2011 ni ‘Fursa sawa katika elimu, mafunzo, sayansi na teknolojia: Njia ya Wanawake kupata ajira bora” na katika lugha ya kingereza ni ‘Equal access to education, training, science and technology: Pathway to decent work for women”.
Kaulimbiu hii inasisitiza umuhimu wa kuwapatia wanawake na wanaume fursa sawa katika elimu, mafunzo, sayansi na teknolojia ili nao waweze kupata ajira bora kama ilivyo kwa wanaume. Kaulimbiu hii inaenda sambamba na utekelezaji wa Ulingo wa Beijing, kwa kuzingatia kuwa mojawapo ya maeneo yaliyopewa kipaumbele katika utekelezaji wa Ulingo wa Beijing ni kuwapatia wanawake elimu mafunzo na Ajira.

Kaulimbiu ya mwaka 2011 inahamasisha Serikali katika kutoa fursa sawa kwa watanzania wote bila kujali jinsi zao.
Katika kuhakikisha kuwa kunakuwepo na fursa sawa kwa wanawake na wanaume, Serikali imekuwa ikichukua hatua mbalimbali, ikiwa ni pamoja na kurekebisha baadhi ya sheria na inapobidi kutunga mpya ili kuhakikisha kuwa kunakuwepo na fursa sawa kati ya wanawake na wanaume katika elimu, mafunzo sayansi na teknolojia.

Katika kuhakikisha kuwa kunakuwepo na maendeleo ya sayansi na teknolojia, Serikali imeandaa mpango wa uboreshaji wa mfumo wa sayansi na teknolojia na ubunifu hapa nchini. Aidha, imeendelea kutoa elimu kupitia vyombo vya habari kuhusu matumizi ya vyombo vya sayansi na teknolojia.

No comments: