Wednesday, March 16, 2011

Shida ya maji Dar es Salaam mwisho 2013

SERIKALI itatumia Sh bilioni 654 katika programu maalumu ya maji jijini Dar es Salaam ili kuongeza usambazaji wa maji pamoja na kupunguza idadi ya maji yanayopotea kutoka asilimia 50 hadi asilimia 30.

Chini ya programu hiyo inayotarajia kukamilika mwaka 2013, Serikali itachangia asilimia 80 ya mradi huo ambazo ni Sh bilioni 526 , wadau wengine wa maendeleo watachangia asilimia 20 (Sh bilioni 128).

Akizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam jana, Waziri wa Maji, Profesa Mark Mwandosya alisema, programu hiyo ni kubwa inaofanywa na Serikali ukifuatiwa na mradi wa maji wa Kahama-Ziwa Victoria uliogharimu zaidi ya Sh bilioni 220.

Profesa Mwandosya alisema, programu hiyo pia itahusisha ujenzi wa mitambo ya kusafisha maji katika Bonde la mto Msimbazi, Mbezi Beach na baadaye katika maeneo ya Kurasini.

“Programu hiyo itahusisha ujezi wa visima virefu katika maeneo ya Kimbiji (Kisarawe) na Mpera katika Wilaya ya Mkuranga ili kutoa huduma ya maji kusini mwa Dar es Salaam,” alisema.

Profesa Mwandosya alifafanua kuwa, upembuzi yakinifu wa ujenzi wa Bwawa la Kidunda huko Morogoro utamalizika Juni mwaka huu; bwawa hilo la kuhifadhi maji litakuwa chanzo cha maji jijini Dar es Salaam itakayoongeza katika mto Ruvu ambao iliarifiwa kiwango cha maji kilipungua kutokana na mabadiliko ya hali ya hewa yanayotokana na uharibifu wa mazingira.

“Kwa sasa tunatafuta mkandarasi kupanua mtambo wa maji wa Ruvu Juu utakaowezesha kusambaza maji lita milioni 142 kutoka za sasa ambazo ni lita milioni 82 ikiwa ni ongezeko la lita milioni 60 kwa siku.

Upanuzi wa mtambo wa Ruvu Chini tayari unaendelea chini ya makampuni kutoka Ufaransa na Kenya ambapo uzalishaji wa maji utaongezeka kutoka lita milioni 182 hadi lita milioni 272 kwa siku ikiwa ni ongezeko la lita milioni 90 kwa siku, alieleza Waziri huyo wa Maji.

Alisema, mabomba makubwa mawili yatajengwa kutoka Ruvu Juu hadi Segerea ili kutoa huduma kwa wakazi wa Kimara, Ubungo, Kinyerezi na Segerea na bomba lingine litajengwa Ruvu Chini.

Alisema, fedha kutoka wadau wa maendeleo zitapatikana kwa kuwa , kati ya hizo zinatoka katika Akaunti ya Changamoto za Milenia na kwa kuwa programu hiyo ni ya miaka minne, Serikali imejiandaa kuhakikisha fedha zote zinapatikana.

Ingawa programu hiyo itakamilika Desemba 2013, imeanza katika Bajeti ya Serikali ya 2010/11 hadi 2013/14, na kwa zaidi ya miaka 30, Dar es Salaam haikuwa na mradi wowote wa usambazaji wa maji ambapo ule wa Mtoni ulijengwa mwaka 1949, Ruvu Juu 1959 na Ruvu Chini ilijengwa mwaka 1976.

No comments: