Tuesday, March 15, 2011

Wanawake wasioona kufundishwa haki zao

IDARA ya Wanawake ya Chama cha Wasioona Tanzania, imezindua rasmi mafunzo ya kuwajengea wanawake wasioona uwezo wa kutambua haki zao na kupambana na kero mbalimbali za maisha.

Mafunzo hayo kwa viongozi wanawake wasioona yataendeshwa kwa awamu katika kipindi cha miezi tisa kuanzia mwezi huu, yakihusisha eneo la majaribio la awali la mradi huo lenye wilaya 12 katika mikoa ya Morogoro, Dodoma na Iringa.

Mratibu wa mafunzo hayo kutoka makao makuu ya Chama cha Wasioona Tanzania (TLB), Doroth Kaihuzi aliwaambia washiriki wa mafunzo hayo kutoka wilaya za Bahi, Mpwapwa, Chamwino na Dodoma mjini jana kuwa, mpango huo umegharimiwa na Mfuko wa Asasi za Kiraia (FCS) kwa gharama ya Sh milioni 45.

Amesema, wanawake wasioona wamekuwa wakiishi katika mazingira magumu bila kutambua haki zao za msingi, ambapo mradi huo utawasaidia kutambua na kudai haki zao bila kujali mtazamo hasi wa jamii na familia zao.

“Mradi unalenga kuwajengea uwezo wa kujitegemea, kujitetea wenyewe na kujisemea bila kutegemea uwakilishi wa watu wasio na ulemavu ambao hawana uchungu na hali yetu kwa vile haiwagusi.”

“Tunataka kila mwanamke asiyeona ajiamini na kwenda kwenye vyombo vya uamuzi kudai haki,” alisisitiza Kaihuzi ambaye ni mlemavu asiyeona na Katibu wa Idara ya Wanawake ya TLB.

Katika mafunzo hayo wanawake wasioona watajifunza mbinu za ushawishi na utetezi, ujasiriamali, sheria mbalimbali, haki za binadamu na sera zinazogusa huduma za kijamii wanazokoseshwa kutokana na ulemavu wao.

Mwenyekiti wa Idara ya Wanawake Wasiiona, Dorice Kulanga akizungumzia historia fupi ya idara hiyo iliyoundwa 1989, alisema ililenga kuwaunganisha walemavu wasioona Tanzania Bara na kushughulikia masuala ya kuinua uchumi kwa kuwahimiza kujiunga na vikundi vya uzalishaji mali.

Akifungua mafunzo hayo, Mwenyekiti wa TLB, tawi la Mkoa wa Dodoma, Omari Lubuva alitoa changamoto kwa Serikali na wadau kuwekeza katika elimu ya watu wenye ulemavu na kubainisha kuwa idadi yao siyo kubwa hasa wanawake wasioona.

No comments: