Friday, September 12, 2008

Mauaji ya Albino ni Ujinga

HAKUNA lugha sahihi ya kuelezea tatizo la mauaji ya albino zaidi ya kusema ni vitendo vya kinyama na vinavyokiuka haki ya msingi ya binadamu wenzetu; haki ya kuishi na kulindwa na jamii inayowazunguka.

Jambo la msingi ni kwamba yote haya yanatokea kwa sababu tu albino wanaonekana tofauti na sisi. Albinism (kuwa albino) ni ugonjwa unaosababishwa na matatizo katika utengenezaji wa chembe chembe za kutengeneza rangi ya ngozi na kwetu sisi Weusi, badala ya rangi ya mwili (ngozi na nywele) kuwa nyeusi, inakuwa nyeupe. Mboni za macho yao huwa ya rangi ya bluu na yenye shida kuona vizuri kwenye mwanga.

Kwa sababu hii, albino wanahitaji kusogeza kitu karibu sana na macho yao ili waweze kukiona vizuri; wanafunzi wanahitaji kukaa karibu na ubao darasani ili waweze kuona vizuri kinachoandikwa ubaoni.

Kuwa albino, inabidi kurithi vinasaba vya tatizo hili kutoka kwa baba na mama ambao inabidi wote wawe aidha albino au wana vinasaba vya ualbino ili mtoto aweze kurithi vinasaba hivi kutoka kwa wazazi wote wawili. Kama albino ataoa au kuolewa na mtu asiye na vinasaba hivi, watoto watakaozaliwa watarithi vinasaba hivi lakini wataonekana watu wa kawaida kama binadamu yeyote.

Unashauri jamii ifanye nini kukomesha mauaji dhidi ya ndugu zetu hawa albino!!!

3 comments:

Anonymous said...

Ukweli ni kwamba serikali itangaze janga la kitaifa juu ya mauaji ya maalbino.Naipongeza sana BBC hasa Vick Ntetema kwa ujasiri alioufanya wa tafiti juu ya mauaji ya maalbino huko MARA na MWANZA.Mwisho naipongeza team nzima ya habari za GDSS kwenye glob.
HASHIM SAID LUANDA,GDSS

Anonymous said...

Mara ya kwanza watu walichinwa ngozi,watu tena wakakatwa sehemu za siri,hatujasahau mauaji ya wanawake vikongwe huko SHINYANGA NA MWANZA,na sasa ni mauaji ya maalbino.
Cha ajabu hakuna jitihada za makusudi ambazo Serikali imezifanya kuondoa matatizo haya.Ila wanazidi kutushawishi tuwapigie kura!!!! za kula!
by,
HASHIM SAID LUANDA; GDSS

Anonymous said...

Nashauri Serikali,iandae mkakati wa kukutana na wachimba madini na wavuvi ambayo kwa tafiti mbalimbali ndiyo wahusika wakuu wa mauaji wa maalbino ili wajadili mbinu na hatua kali za kuchukua dhidi ya wahusika watakaopatikana na kashfa hii.
Pia Elimu itolewe zaidi hasa kwa wananchi ju ya imani-zembe(potofu).
by,
Hashim Said Luanda GDSS.