Wednesday, October 13, 2010

Waangalizi wa EU wasema hawatabeba chama chochote

Timu ya waangalizi 70 kutoka Umoja wa Ulaya (EU) imewasili nchini kwa ajili ya kuangalia Uchaguzi Mkuu na kusema kuwa haitakipendelea chama chochote.

Kiongozi wa waangalizi hao, David Martin, alisema hawatarajii kupendelea chama chochote kwa kuwa sio moja ya kazi iliyowaleta.

Alisema wakiwa hapa nchini watatathmini kwa kina mchakato wa kampeni zinazoendelea na kuangalia kiasi gani uchaguzi huo unavyoheshimu kanuni za kimataifa.

Aidha, alisema wataangalia namna gani haki za kisiasa zinavyoheshimiwa na matamko mbalimbali ya kimataifa yaliyoridhiwa na serikali ya Tanzania ili mwishoni waweze kuandika ripoti yao na kuikabidhi kwa serikali ya Tanzania.

Martin alisema EU imewahi kushiriki katika uangalizi wa uchaguzi zaidi ya mara 80 katika nchi 50 duniani na kwamba wanao watalaamu wa kutosha ambao hawaegemei upande wowote.

Aliongeza kuwa wakiwa hapa nchini watakuwa wanawasiliana na wagombea wote, vyama vya siasa, mabalozi waliopo nchini na wapiga kura.

Alifafanua kuwa watatekeleza majukumu yao kwa kuzingatia makubaliano kati yao na Tume ya Uchaguzi za Zanzibar (Zec) na Tume ya Taifa ya Uchaguzi (Nec).

Chini ya makubaliano hayo, waangalizi hao watakuwa na uhuru wa kwenda mahali popote na kumhoji mtu yeyote wanayemtaka bila masharti.

Uhuru mwingine watakaokuwa nao ni kuzungumza na vyombo vyote vinayohusika na uchaguzi ikiwemo kuruhusiwa kuingia bila masharti kwenye vituo vya kuhesabia kura.

Alidha, Martin alisema watakuwa na haki ya kupata taarifa zozote kabla na baada ya kufanyika kwa uchaguzi.

Kuhusu vyombo vya usalama kutoa tamko dhidi ya wanasiasa wanaotaka kuvuruga amani lililotolewa na Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) na Jeshi la Polisi, Martin alisema hana maoni yoyote juu ya suala hilo.

Akijibu madai ya kuwepo karatasi za kutoka nchi moja ya Asia ambazo inadaiwa mtu akipiga kura inabadilika na kuandika jana la mtu mwingine, alisema madai hayo hajawahi kuyasikia na kuongeza kuwa kama yalikuwepo, mwaka huu halitatokea kwa kuwa safari hii karatasi za uchaguzi zimetengezwa kwa ubora nchini Uingereza.

No comments: