Friday, October 8, 2010

Membe:Shimbo hakukosea

SERIKALI imesema vyombo vya usalama vina haki ya kutahadharisha wananchi juu ya jambo lolote tofauti na baadhi ya vyama vya siasa, wanaharakati na watu mbalimbali wanavyosema.

Aidha, imeelezwa kuwa kauli ya Mnadhimu Mkuu wa Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ), Jenerali Abdulrahman Shimbo, kuwa vyombo hivyo vimejiandaa kuhakikisha amani wakati wa uchaguzi, imepotoshwa na kukuzwa bila sababu za msingi.

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe amesema hayo wakati wa mkutano na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana.

“Tuache kukuza mambo, alichozungumza Shimbo ni sahihi na wala hakina utata wowote. Matamshi yake yametafsiriwa vibaya na kupotoshwa.

“Vyombo vya usalama sio vya chama fulani na wala havitetei maslahi ya chama chochote, ni kwa ajili ya amani na utulivu wa kila mmoja na nchi kwa ujumla,” alisema Membe na kuongeza:

“Kazi ya vyombo hivi ni kutahadharisha, kuonya na ikilazimika kukamata, sasa sioni ni wapi vilikosea, wahusika warejee kauli ya Shimbo au wasome ujumbe huo kwa sababu haukutolewa kiholela, uko wazi na hauna utata wowote.”

Alisema ameshuhudia uchaguzi katika nchi nne tofauti duniani na kauli za tahadhari zenye kusisitiza utulivu na amani kama ya Shimbo hutolewa bila kuleta utata.

“Ni aibu na siogopi ninathubutu kusema tunatia aibu, vitu vidogo tunavikuza na kuvishabikia sana. Nilikuwa Brazil Septemba 3, mwaka huu wakati wakipiga kura katika uchaguzi mkuu wao, vyombo vya usalama viliheshimiwa kufanya kazi yake ya kulinda amani ikiwa ni pamoja na kutoa kauli mbalimbali za tahadhari,” alisema.

No comments: