Friday, October 8, 2010

Redet:Kikwete yupo juu

ASILIMIA 68.5 ya Watanzania waliohojiwa na Mpango wa Utafiti na Elimu ya Demokrasia (Redet) wamesema wanataka mgombea urais wa Tanzania, Jakaya Kikwete, achaguliwe kuwa Rais.

Mgombea anayefuatia kwa mujibu wa matokeo ya utafiti huo wa taasisi hiyo ni wa Chadema Dk Willibrod Slaa, ambaye amependekezwa na asilimia 11.9 ya waliohojiwa huku Profesa Ibrahim Lipumba wa CUF akitajwa na asilimia 9.3.

Maoni hayo yamechukuliwa katika mikoa yote nchini katika utafiti ulioanza Septemba 20 hadi 28 ukishirikisha watu wapatao 2,600 kwa kutumia sampuli nasibu kwa wahojiwa kutoka katika kila wilaya mbili.

Akizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam jana, Mwenyekiti Mwenza wa Redet, Dk. Benson Bana, alisema matokeo hayo yanaashiria kwamba endapo uchaguzi ungefanyika Septemba CCM ingeshinda katika urais, ubunge na udiwani.

Licha ya Watanzania kupiga kura za kupenda kuongozwa na Kikwete, asilimia 71.2 walisema watachagua mgombea yeyote wa CCM, asilimia 12.3 wa Chadema, asilimia 10.1 wa CUF, huku vyama vingine vikipata idadi ndogo ya wahojiwa na asilimia 5.6 wakishindwa kuamua.

Dk. Bana alisema kwa upande wa ubunge, asilimia 66.7 ya wahojiwa walisema watachagua wa CCM, asilimia 11.7 wa CUF na asilimia 11.5 Chadema huku asilimia 7.8 walioshindwa kuamua.

Kwa madiwani, asilimia 66 walisema watachagua wa CCM, asilimia 11.5 wa CUF na asilimia 10.3 wa Chadema huku asilimia 10.4 wakikosa msimamo.

Alisema utafiti wa Redet wa Machi ulionesha wahojiwa wengi wangechagua mgombea yeyote wa CCM kwa asilimia 77.2 lakini katika utafiti wa Septemba walimkubali kwa asilimia 71.2 hivyo kupungua kwa asilimia sita na wabunge ilikuwa asilimia 68 na madiwani 68.2, hivyo kwa utafiti huu, CCM bado inaongoza, lakini kiwango cha asilimia za kura kimepungua.

Wakati kwa vyama vinne vya upinzani vikiongozwa na Chadema, vimeongeza idadi ya kura ambapo katika miezi sita, waliosema watachagua mgombea wa Chadema imeongezeka kwa asilimia nane, CUF asilimia 0.9, TLP imeongeza kutoka asilimia 0.2 hadi 0.4, NCCR-Mageuzi kutoka asilimia 0.2 hadi 0.3.

Kwa upande wa wabunge, wakati asilimia 68 ya wahojiwa walisema wangechagua mgombea wa CCM kama uchaguzi ungefanyika Machi; lakini kwa Septemba waliosema hivyo ni asilimia 66.7.

Chadema imeongeza kwa asilimia 2.9, CUF asilimia 1.5 , TLP asilimia 0.8 na NCCR-Mageuzi asilimia 0.8.

Alisema hata hivyo baada ya takribani mwezi mmoja wa kampeni za uchaguzi, kiwango cha uungwaji mkono cha CCM kinapungua wakati kile cha vyama vya upinzani hasa Chadema na CUF kinaongezeka, huku wananchi wengi wakitegemea redio kama chanzo kikuu cha taarifa za kampeni za vyama na wagombea.

Profesa Bana alisema waliohojiwa walitaka vyombo vya habari kutoa nafasi sawa kwa vyama vya siasa, huku wakitaka elimu kuwa suala la kupewa kipaumbele katika serikali ijayo ikifuatiwa na kilimo, afya na maji.

Walitoa angalizo kuwa matokeo ya utafiti huo ni kwa Septemba tu, hivyo katika kipindi cha kuelekea uchaguzi, mambo kadhaa yanaweza kutokea na kubadilisha mwelekeo na mtazamo wa wapiga kura.

Alisema waliohojiwa waliulizwa sifa kubwa itakayowafanya wampigie kura mgombea urais wakisema ni uzoefu katika uongozi (14.8%), anayejali wanyonge na masikini (14.1%), mgombea wa chama chao (14.1%), mgombea asiyeshiriki rushwa au ufisadi (9.9%) na mgombea mwenye elimu (1.9%).

Alisema, mgombea urais wa CCM alitajwa kuchaguliwa zaidi ya asilimia 50 katika wilaya 43 zilizofanyiwa utafiti huku katika wilaya tisa akitajwa chini ya asilimia 50 na wa Chadema akitajwa kwa zaidi ya asilimia 50 katika wilaya tatu za Kinondoni (64%), Kigoma Mjini(56%) na Babati (58%) na mgombea wa CUF kwa zaidi ya asilimia 50 anatajwa katika wilaya moja ya Mkoani kwa asilimia 68.

Kuhusu uchaguzi wa wabunge CCM inaungwa mkono zaidi ya asilimia 50 katika wilaya 40 zilizofanyiwa utafiti huku Chadema ikiungwa mkono kwa asilimia 50 katika wilaya ya Kinondoni asilimia 60, Kigoma Vijijini asilimia 58, Mvomero asilimia 50 na nyinginezo na CUF wakiungwa mkono Micheweni asilimia 49, Wete asilimia 42 na Lindi Mjini asilimia 36.

Walipoulizwa kuhusu utendaji kazi wa Chama tawala asilimia 57.4 walisema wanaridhika na utendaji kazi wa CCM,20.7 walisema wanaridhika kiasi, asilimia 12.3 hawaridhiki na asilimia saba hawaridhiki kabisa, upande wa utendaji kwa vyama vya upinzani asilimia 35.6 walisema wanaridhika sana, asilimia 22.6 wanaridhika kiasi, asilimia 23 hawaridhiki na asilimia 7.2 hawaridhiki kabisa.

Alisema,walipoulizwa kuhusu sababu za kuridhika kiasi au kutoridhika na utendaji kazi wa chama tawala, asilimia 12.7 walisema hawatimizi ahadi 7.7 wala rushwa, asilimia 4.3 hawaaminiki huku kwa upinzani asilimia 7.6 hawaaminiki, 6.5% havina sera, 6.2% vina migogoro na 5.3% havina uwezo wa kuongoza nchi.

Kuhusu chanzo kingine cha habari za kampeni za uchaguzi walisema mikutano ya hadhara inaongoza kwa asilimia 38, ndugu na marafiki 21%, vyama vyao vya siasa asilimia sita, mabango na vipeperushi asilimia nne huku kwa asilimia ndogo makanisa 0.6% na misikiti 0.3%.

Mtafiti Mkuu wa Redet, Dk. Bernadeta Killian, alisema sababu za kutoa utafiti huo sasa, ni utaratibu wao wa kawaida kila baada ya miezi sita huku akikanusha baadhi ya shutuma kuwa watafiti hupewa fedha kupendelea upande fulani.

No comments: