Wednesday, October 13, 2010

Nipeni urais niwakomeshe wauaji wa maalbino, asema Prof. Lipumba

Mgombea urais kupitia Chama Cha Cha Wananchi (CUF), Profesa Ibrahim Lipumba, amesema kuwa akishaguliwa atahakikisha anachukua hatua madhubuti kukomesha mauaji ya watu wenye ulemavu wa ngozi (albino).

Mgombea huyo pia ameiponda serikali kwa kujenga vituo maalum kwa ajili ya kuhifadhi watu wenye ulemavu wa ngozi (albino) na kuahidi kuvifuta iwapo atachaguliwa.

“Nitahakikisha pia kwamba ninaondoa utaratibu wa sasa wa serikali kutenga maeneo maalum kwa ajili ya hifadhi kwa watu wenye ulemavu wa ngozi kwa sababu siyo utaratibu mzuri wa kuwawekea kambi,” alisema jijini Mwanza wakati akihutubia mkutano wa kampeni katika eneo la Pasiansi.

Profesa Lipumba alisema kuwa mauaji ya watu wenye ulemavu wa ngozi nchini yanashamiri kutokana na tabia ya baadhi ya vigogo ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) kuendekeza vitendo vya ushirikina.

Alisema vitendo hivyo visingeshamiri iwapo viongozi wa serikali ya CCM wangelikuwa na uchungu.

Lipumba alisema mfano unaodhihirisha serikali ya CCM kutokuwa makini ni kuwanadi katika majukwaa watuhumiwa wa ufisadi kwamba ni watu wasafi.

Kwa mujibu wa Profesa Lipumba, akichaguliwa kuwa Rais atahakikisha watuhumiwa wa mauaji dhidi ya watu wenye ulemevu wa ngozi nchini wanakamatwa haraka na kesi zao kutolewa hukumu mapema.

Aidha, aliahidi kuwa atahakikisha kwamba kila mwanafunzi anakuwa na kompyuta moja, kuanzia elimu ya msingi. “Mkinichagua mimi nitahakikisha kwamba Tanzania inajiunga na utaratibu wa Kimataifa wa kila mwanafunzi kuwa na kompyuta moja ya kujifunzia,” alisema Profesa Lipumba.

Aliahidi pia kwamba akiwa Rais, atahakikisha kuwa anafumua mikataba yote ya madini pamoja na kupitia upya misamaha ya kodi kwa wafanyabiashara.

Profesa Lipumba jana aliendelea na kampeni katika Jimbo la Magu.


CHANZO: NIPASHE

No comments: