Monday, October 4, 2010

Dewji amfagilia Kikwete

Mgombea ubunge wa Jimbo la Singida Mjini kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), Mohamed Dewji, amesema Mgombea urais wa chama hicho, Rais Jakaya kikwete ameiongoza nchi na CCM vizuri tangu achukue madaraka mwaka 2005.

Alisema hayo juzi alipokuwa anasoma mafanikio ya utekelezaji wa ilani ya CCM kwa miaka mitano iliyopita na kusema wananchi wa Singida wamenufaika na mengi hata wakati wa mtikisiko wa uchumi na upungufu wa chakula walipata msaada kutoka serikalini.

Kwenye upande wa upatikanaji wa maji safi na salama, Dewji alisema sasa maji safi yanapatikana kwa asilimia 85, ukilinganisha na miaka mitano iliyopita.

Vilevile kwenye elimu, alisema sasa Singida Mjini ina shule za sekondari zaidi ya 20 ikilinganishwa na shule mbili tu miaka mitano iliyopita.

Hata hivyo alisema changamoto iliyopo kwa upande wa elimu ni ujenzi wa shule za kidato cha tano na sita ili wanafunzi wengi zaidi watakaofaulu kidato cha nne wapate nafasi ya kidato cha tano na sita.

Changamoto nyingine ni upande wa afya na ugonjwa sugu wa macho (mtoto wa jicho), ambao alieleza unatokana na hali ya hewa ya mji wa Singida. Alisema amefanya jitihada kwa kushirikiana na mashirika yasiyo ya kiserikali na hadi sasa wagonjwa 500 wamefanyiwa upasuaji kati ya wagonjwa 2,000.

Aliwataka wakazi wa Singida Mjini wafanye maamuzi mazuri ya kuchagua viongozi bora kipindi cha uchanguzi.


CHANZO: NIPASHE

No comments: