Tuesday, October 5, 2010

Makachero watumwa kumdhibiti Dk. Slaa

MGOMBEA Urais wa CHADEMA, Dk. Willibrod Slaa ametangaza kuwapo kwa mkakati mahususi wa kulazimisha ushindi kwa mgombea wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), ikiwa ni pamoja na kusambaza makachero nchi nzima kutimiza azma hiyo.

“Tuna taarifa za kusambazwa kwa makachero nchi nzima ambao wamepewa jukumu la kuhakikisha kwamba Kikwete anashinda kwa gharama zozote,” anasema Dk. Slaa alipozungumza na Raia Mwema, mara baada ya mkutano na waandishi wa habari jana Jumanne.

Katika mkutano huo, CHADEMA pia walitangaza kupata ushahidi kwamba kampuni ya Synovate ilifanya utafiti kuhusu wagombea wa nafasi mbalimbali ikiwamo urais, tofauti na hatua ya hivi karibuni ya kampuni hiyo kukanusha kuwapo kwa utafiti huo.

“Tumepata ushahidi kwamba Synovate walifanya utafiti kuhusu umaarufu wa wagombea na walipata matokeo ambayo hawajayatangaza. Tunawataka sasa waende mahakamani,” alisema Dk. Slaa.

CHADEMA wanasema kwamba hata watafiti waliokwenda kufanya utafiti huo wako tayari kubainisha usiri wa kampuni hiyo uliofanywa kwa maslahi ya CCM.

Hivi karibuni vyombo vya habari wiki hii vilimnukuu Mwenyekiti wa CHADEMA, Freeman Mbowe akisema kuwa chama chake kina matokeo ya kura za maoni za Synovate yanayoonyesha kuwa Dk. Slaa anakubalika kwa asilimia 45 akifuatiwa na Rais Kikwete mwenye asilimia 41, kauli ambayo ilikanushwa na Synovate.

Akizungumza na waandishi wa habari wiki iliyopita Meneja wa Synovate Limited, Aggrey Oriwo alisema taarifa hizo ni za kughushi, hazina ukweli wowote na zinaupotosha umma kwa kuwa hawajawahi kufanya utafiti wowote unaohusu kukubalika kwa wagombea wa urais.

Oriwo alisema kwa kawaida kampuni yao hufanya utafiti wa hali ya kisiasa kila baada ya miezi mitatu na kwamba wanatarajia kufanya hivyo kabla ya Oktoba 31 na kutoa taarifa yao. Mbali na Synovate, Taasisi ya Mpango wa Utafiti na Elimu Demokrasia Tanzania (Redet) ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, nayo imeeleza kuwa wataalamu wake kujiandaa kufanya utafiti wa mgombea urais anayekubalika.

Dk. Slaa anaanza awamu ya pili ya kampeni zake mkoani Morogoro Alhamisi wiki hii huku akiwa na imani kwamba sehemu kubwa ya wananchi wanamuunga mkono.

Mgombea huyo wa CHADEMA amenukuliwa akisema kwamba maeneo yote ambayo amepita sehemu kubwa ikiwa ni vijijini, wananchi wameonyesha mwamko wa hali ya juu na wamekuwa wakikusanyika bila kujali mbinu chafu za kuwalaghai ili wasihudhurie mikutano yake ya kampeni.

“Awamu ya kwanza ya kampeni zetu sehemu kubwa tumetembelea vijijini na huko wananchi wamekuwa wakifika wenyewe bila kubebwa na magari kama wenzetu. Wananchi sasa hawaogopi tena askari wa FFU wenye silaha ambao wamekuwa wakifika wakiwa wamejiandaa kwa mapambano ili kuwatisha, huu ni mwamko mkubwa sana,” alisema.

Alisema tofauti na uchaguzi wa mwaka 2005, uchaguzi wa mwaka huu CHADEMA imesimamisha wagombea wengi makini zaidi na ambao wamejitokeza wenyewe bila kushinikizwa na hivyo kuongeza nguvu ya kukubalika kwa umma ikiwa ni ishara ya ushindi katika uchaguzi wa mwaka huu.

“Unapoona sasa wasomi hadi DC (Mkuu wa Wilaya), wahandisi, wanasheria na watu wa kada nyingine wanakuja wenyewe kutaka kugombea kwa chama cha upinzani, ujue sasa nchi imejiandaa kwa mabadiliko, wakati wa CCM kuondoka umefika,” anasema.

Katika ziara yake, Dk. Slaa anasema amewaahidi wananchi kwamba ndani ya miaka mitatu ya utawala wake atahakikisha kwamba Tanzania inaondokana na aibu ya kuagiza chakula nje ya nchi wakati ina ardhi ya kutosha.

“Maisha ya Watanzania nimekuta ni mabaya sana na hii ni vijijini na mijini. Miaka 50 ya Uhuru wananchi wanaishi katika nyumba za ajabu, wakati nchi kama Rwanda zimefanikiwa kupunguza tatizo la makazi kwa watu wake.

“Suala la makazi si tu linagusa umasikini bali linahusu afya zao maana makazi mabovu yanachangia afya mbovu na ndio maana suala la kusaidia wananchi wapate nyumba bora si la mzaha, nitahakikisha naondoa kodi katika vifaa vya ujenzi ili wananchi waweze kujenga makazi bora,” anasema.

Anasema suala la elimu ameliwekea msisitizo na kwamba atahakikisha elimu ya lazima inakuwa hadi kidato cha sita na wananchi wengi waliohojiwa wanakubali kwamba inawezekana pamoja na CCM kubeza mpango huo.

Dk. Slaa anasema kwa miaka mitano ya utawala wa Jakaya Kikwete, asilimia 75 ya bajeti ya serikali imekuwa ikienda kwenye matumizi ya kawaida, sehemu kubwa yakiwa ni anasa na kuacha sekta muhimu kama afya, elimu na miundombinu zikitegemea zaidi wafadhili.

Wakati huo huo, CHADEMA wametangaza vigezo watakavyotumia kuteua wagombea wa Vitimaalumu kwenye uchaguzi Mkuu wa mwaka huu.

Akizungumza na waandishi wa habari, Mratibu wa Uchaguzi wa CHADEMA, Kitila Mkumbo, alisema vigezo hivyo ni pamoja na elimu, uzoefu wa uongozi wa kisiasa na uzoefu wa mgombea nje ya siasa.

Mkumbo alivitaja vigezo vingine kuwa ni pamoja na uwezo wa mgombea anayegombea katika jimbo, mchango wa mgombea katika operesheni na katika kampeni zinazoendelea pamoja na umri wa uanachama wa mgombea husika.

No comments: