Friday, October 15, 2010

Kikwete:Wakataeni wanasiasa wachochezi

KAULI za umwagaji damu katika majukwaa ya siasa nchini ndizo zitakazolazimisha vyombo vya ulinzi na usalama nchini kuingilia kati kudumisha amani kwa kuwa ni kazi yao.

Sambamba na hilo, Watanzania wametakiwa kuwakataa wanasiasa wanaochochea umwagaji damu na ubaguzi wa dini, kabila na uchochezi wa chuki.

“Wanasiasa kama wanataka kuzuia vyombo vya ulinzi kuingilia ni kuacha kuzungumzia kumwaga damu, tuwaache wafanye kazi yao tusiwaingilie na sisi tuzungumzie barabara, madaraja, maji”.

Hiyo ni kauli ya Rais Jakaya Kikwete aliyoitoa katika sherehe za kuzima Mwenge wa Uhuru zilizofanyika katika uwanja wa Lake Tanganyika mjini Kigoma jana, sambamba na maadhimisho ya miaka 11 tangu kifo cha Mwalimu Julius Nyerere.

Aliwataka Watanzania kukemea na kukataa wanasiasa wanaochochea na kupandikiza chuki, kugawa watu kwa udini, ukabila, rangi, jinsia na wanakotoka watu.

“Tuwakemee wanaopandikiza chuki, kuna watu sasa wanatuma ujumbe mfupi wa simu za mkononi wa hovyo, matusi na kuwabagua watu kwa dini, wanasiasa wanataka tuchaguliwe kwa umwagaji damu wakati katika uongozi wa Nyerere, hakukuwa na mgogoro wa Wahaya na Wachaga wala Wakristo na Waislamu.

“Lakini sasa kuna wanasiasa wanaotaka uongozi kwa chuki na wana uchu wa madaraka hawajali, potelea mbali hata damu ikimwagika wao wanataka uongozi … tuwaambieni mzee tunakuheshimu sana, lakini haya unayotwambia hatutaki …tumeona ya Burundi na Rwanda na hapa Kigoma mna uzoefu nayo, hivi kwetu kukitokea mauaji hata hawa wa Kasulu hawatoshi Burundi kutokana na ukubwa wa nchi yetu,” alisisitiza.

Alisema, Watanzania kwa asili si watu wenye matatizo, lakini viongozi wa kisiasa wakiwachochea kufanya fujo na kuwabagua, nao watafanya na kuwataka kuwa makini katika kipindi hiki cha kuelekea kwenye uchaguzi, ambapo wanasiasa wako tayari kufanya lolote ili kupata uongozi.

Katika maadhimisho hayo yaliyopambwa na nyimbo na halaiki, Rais Kikwete alisema Serikali imejipanga kufanya kila iwezalo ili nchi iwe na amani na uchaguzi ufanyike kwa njia ya usalama na amani.

“Nimetoka mikoa ya Kusini kuna mgombea mmoja anasema watoto wakilalia vyandarua wanakufa … ni uongo wa mchana, hivi sisi wanasiasa hatuwezi kuomba kura bila uongo?
Tunatisha watu bure, hii si siasa bali ni ‘sihasa’…”, alisema Rais Kikwete ambaye pia ni mgombea urais kwa tiketi ya CCM.

Akizungumzia mipango ya Serikali kutokomeza malaria, alisema tayari mkoa wa Kagera umemaliza kupuliza dawa nyumba kwa nyumba na mwanzoni mwa mwezi huu, wameanza mkoani Mara, ambako lengo ni kupulizia dawa za kuua malaria katika mikoa yote.

Alisema Serikali ina mpango wa kupulizia dawa kwenye madimbwi ya maji ili kuua viluwiluwi na ifikapo mwaka 2015 malaria iwe imetokomezwa nchini.

Kuhusu tatizo la maji Kigoma, alisema kwa sasa kunajengwa matangi ya maji mapya yenye uwezo wa kuhifadhi maji meta za ujazo 16,000 wakati yaliyopo sasa yanahifadhi meta za ujazo 4,000.

Alisema kutawekwa mabomba mapya na mitandao mipya ya maji. Katika kuwezesha vijana, alisema katika halmashauri, kutaajiriwa maofisa vijana watakaokuwa na kazi ya kuwaendeleza vijana na kusimamia shughuli za kuwawezesha vijana kujiendeleza kiuchumi.

1 comment:

Anonymous said...

Bado sielewi nchi inakokwenda.
Kama uchaguzi umeisha tunapaswa kushirikiana kuijenga nchi yetu. Tofauti za kisiasa, kimila, kidini na rangi zisipewe nafasi hata sekunde moja.