Wednesday, October 27, 2010

Rais Kikwete atukanwa 'live'

MALALAMIKO ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) dhidi ya kampeni za mgombea urais wa Chadema, Dk. Willibrod Slaa kuwa zimejaa matusi, yalidhihiri jana pale kampeni za mgombea huyo zilipotumika kumtukana Rais Jakaya Kikwete na mama yake mzazi.

Kabla ya kuanza kumtukana Rais wa nchi ambaye pia ni mgombea urais kwa tiketi ya CCM, Dk. Slaa mwenyewe alitamba kuwa katika viwanja hivyo vya Mwembeyanga, Temeke ndipo alipotoa tuhuma dhidi ya viongozi wengine bila kushitakiwa wala kukamatwa.

Dk. Slaa ambaye alianza hotuba yake kwa kutoa maneno machafu dhidi ya CCM na viongozi wake na kutumia muda kidogo kuelezea hoja za Ilani ya uchaguzi ya chama chake na kujibu hoja za wapinzani wake, kabla ya kumaliza alitoa nafasi kwa mgombea ubunge wa Temeke kuonesha umahiri wa kujenga hoja.

Mbali na kumpa nafasi mgombea huyo aoneshe umahiri huo kwa dakika mbili ili apimwe kama anaweza kutumia dakika tatu wanazopewa wabunge kujenga hoja bungeni, Dk. Slaa aliwaomba wananchi wampigie kura mgombea huyo, kwa kuwa kupitia wagombea wa ubunge wa Chadema akiwemo huyo, ndipo anapotarajiwa kumpata Waziri Mkuu na mawaziri wengine wasiozidi 20.

Hata hivyo mgombea huyo, Dickson Amos, alitumia nafasi hiyo kumtukana matusi ya kumdhalilisha Rais Kikwete na mama yake mzazi na kusababisha matangazo ya moja kwa moja ya TBC1 kutoka katika viwanja hivyo, kukatishwa ghafla ili kustahi ustaarabu wa jamii ya kitanzania.

Matusi hayo ambayo ni aibu kuyaandika, yalitolewa katika mkutano wa hadhara na uliokuwa ukisikilizwa na wasikilizaji mbalimbali wa TBC 1 nchi nzima.

Katika muda mfupi alioutumia kujibu hoja zilizoelekezwa kwake na wapinzani wake kisiasa, Dk. Slaa alisema hahitaji shahada ya uzamivu kwa ajili ya kusimamia masuala ya uchumi wa nchi.

Alikiri kweli yeye ni mbumbumbu wa uchumi kwa sababu amesomea sheria, lakini uchumi aliosoma mwaka 1972 unatosha kujua hali ya Mtanzania na jinsi ya kumsaidia.

Alikuwa akimjibu Waziri wa Afrika Mashariki, Dk. Diodorus Kamala aliyesema mgombea huyo hajui mambo ya uchumi na kumtaka aache kuyajadili.

Aliwataka Watanzania kumpatia wabunge wengi wa Chadema ambao watafuta sheria iliyopandisha bei ya bati na ya saruji na kudai kuwa Watanzania wanalipa kodi nyingi katika bidhaa zao kuliko hata ilivyo kwa nchi za Afrika Mashariki.

“Kama Dk. Kamala haelewi ninachosema akasome gazeti la East Afrika ukurasa wa tatu, ila nina mashaka kama anajua Kiingereza vizuri… na afahamu kuwa Dk. Slaa ni rais wa Watanzania na sio wa Afrika Mashariki,” alisema na kuongeza kuwa yuko tayari kufuta mikataba yote inayowaumiza wananchi.

Kuhusu elimu, alirudia ahadi ya Ilani ya chama chake kuwa akiingia madarakani elimu itakuwa bure kwa kuwa sasa kuna matabaka matatu katika elimu ambayo anataka kuyaondoa.

Alitaja matabaka hayo kuwa ni ya watu wenye uwezo wa kupeleka watoto wao shule za kimataifa, wengine shule za kata ambazo alidai hazina vitabu wala walimu na wengine ni wale ambao wazazi wanakosa hata kufikia kuwapeleka shule.

Akiwa katika viwanja vya Manzese, alitoa nafasi kwa mchumba wake ambaye ni mke wa mtu, Josephine Mushumbusi ambaye alisema kama urais wa Dk. Slaa ni wa familia, yeye angekuwa wa kwanza kumwambia mchumba wake akae nyumbani.

Alisema amezunguka naye nchi nzima na mambo aliyoyaona ya umasikini wa Watanzania, yamemfanya Dk. Slaa hata wakati mwingine kukosa usingizi na yeye kama mchumba amekuwa akimtia moyo.

“Nitahakikikisha Dk. Slaa analala vizuri, na ninamwahidi kumtunza ili aweze kutekeleza majukumu yake vizuri,” alisema Josephine.

No comments: