Monday, January 25, 2010

Warioba aacha ‘maswali’ CCJ

TUHUMA za kuwepo kwa wanasiasa waandamizi na wakongwe wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), wanaopanga kujitoa katika chama hicho tawala na kujiunga na chama kipya wanachodaiwa wamekiandaa kinachoitwa Chama Cha Jamii, zimeendelea kutoa sura tofauti miongozi mwa wanasiasa hao.

Wakati juzi Waziri Mkuu Mstaafu na Mbunge wa Mtera, John Malecela alikanusha vikali kuhusika na uasisi wa chama hicho, jana Habari Leo liliwapata viongozi wengine waandamizi wanaotuhumiwa kuazisha chama hicho ambao hawakuthibitisha kuwa miongoni mwa waasisi wa chama hicho wala kukana tuhuma hizo.

Waziri Mkuu mstaafu, Joseph Warioba alizungumza na Habari Leo kuhusu tuhuma kwamba yeye ni mmoja wa mawaziri wakuu watatu wanaotuhumiwa kuunda CCJ, alisema hawezi kuzungumzia chochote kuhusiana na madai kuwa yeye ni miongoni mwa waasisi wa chama hicho.

“Siwezi kusema chochote kuhusiana na taarifa zinazosambazwa na mtu asiyejulikana,” alisema.

Aidha Waziri Mkuu huyo wa zamani alishauri mwandishi wa habari hizi kuwasiliana na uongozi wa CCJ kuhusiana na shauri hilo.

Habari Leo lilimpata mwanasiasa mwingine mkongwe ambaye pia ni Mwenyekiti wa Taasisi ya Mwalimu Nyerere, Joseph Butiku na kumuuliza iwapo anahusika na uanzishwaji wa chama hicho, kama ilivyo katika waraka wenye tuhuma hizo na yeye alisema hajaona nyaraka zinazomuhusisha yeye na CCJ.

“Sijaona nyaraka hizo,” alisema Butiku na kukataa kuendelea na mahojiano na mwandishi wa habari hii hata baada ya kuhakikishiwa kuwa waraka huo upo.

Mwandishi wa habari alitaka kujua kama mwanasiasa huyo alikuwa ameona nyaraka za chama hicho na kama ana maoni yoyote kuhusiana na madai kwamba anahusika katika kuiasisi CCJ.

Kuomba usajili kwa chama hicho kipya cha siasa kumezua maswali mengi miongoni mwa watu kadhaa wakiwemo wanasiasa kutokana na madai kuwa viongozi wakubwa wa CCM wamekiandaa na wanapanga kujiunga nacho kwa nia ya kuiangusha CCM katika uchaguzi mkuu ujao.

Tayari Katibu Mkuu wa CCM, Yusufu Makamba ametoa kauli kuwa CCJ hakiwatishi huku Katibu wa Uenezi wa Kamati Kuu ya CCM (NEC), John Chilighati akisema kuwa watakaotoka CCM, watakuwa wamejimaliza wenyewe.

Licha ya viongozi hao waliokwisha zungumzia CCJ, viongozi wengine wanaodaiwa kuhusika nacho ni pamoja na kundi la wabunge wanaojipambanua kuwa makamanda wanaopiga vita rushwa.

Kutokana na misimamo ya vigogo hao wanaotuhumiwa kutaka kujiunga na chama hicho, ilidaiwa pia kuwa vigogo hao wameandaa kongamano la kumuenzi Mwalimu Julius Nyerere, litalaotumika kama uwanja wa kukitangaza chama hicho.

Kongamano hilo limedaiwa kuwa lingefanyika kwa mgongo wa taasisi isiyokuwa ya kiserikali ya Aford ambayo haijapata usajili lakini lengo lake likiwa kutoa ishara za awali za chama hicho cha CCJ.

Habari Leo lilifanikiwa kumpata kiongozi wa taasisi hiyo ya Aford, Julius Miselya ambaye alianza kuvishutumu vyombo vya habari kwa kutumia vibaya jina la taasisi yake kuisakama serikali ya Rais Jakaya Kikwete.

“Ni nyie waandishi wa habari mnaosambaza taarifa hii inayotoka kwa mtu asiyejulikana na kuleta mtafaruku nchini,” alisema.

“Mimi sifungamani na chama chochote, nimewatambua watu wanaojihusisha na CCJ kwa kusoma magazeti asubuhi hii,” alisema Miselya.

Amesema kongamano hilo ambalo bado lipo katika maandalizi limeibuliwa kwa waandishi wa habari kwa lengo la kupotosha ukweli.

“Muulize Waziri Mkuu kama amethibitisha kushiriki, sitazungumzia kitu hicho,” alisema. Waziri Mkuu Mizengo Pinda, ametajwa katika waraka huo kuwa ndiye atakayefungua kongamano hilo.

Alipohojiwa kama kongamano hilo litaendelea kama lilivyopangwa, alisema kwamba hatasema chochote kwa vyombo vya habari.

Baadhi ya viongozi wa CCM waliounganishwa na uanzaji wa chama kipya cha siasa nchini walipoulizwa walisema kwamba ndio kwanza wanajua kuwa kuna chama kipya.

Mwanasiasa mwingine aliyehusishwa na chama hicho kipya na kukanusha ni mbunge wa Maswa, Magale Shibuda.

Juhudi za gazeti hili kupata maoni ya wahusika wengine zilishindikana jana na bado zinaendelea.

Juzi Msajili wa Vyama vya Siasa, John Tendwa, aliliambia Habari Leo kuwa chama hicho kipya kina safari ndefu kwa kuwa taratibu za kusajili chama huchukua muda.

Alisema licha ya chama hicho, tayari kuna vyama vingine vingi ambavyo vinasubiri kupewa usajili na kuongeza kuwa huenda CCJ kikapata usajili wa muda kabla ya Machi mwaka huu.

No comments: