Friday, January 8, 2010

Manji, Jeetu Patel waichezea Serikali


-Wachelewesha matrekta ya 'Kilimo Kwanza'

MRADI wa matrekta kwa ajili ya mpango wa uboreshaji wa kilimo nchini-Kilimo Kwanza- umekwama kutokana na kile kinachoelezwa kuwa ni mgogoro kati ya wafanyabiashara wawili nchini, Yussuf Manji na Jayantkumar Chandubhai Patel (Jeetu Patel), Raia Mwema limebaini.

Uchunguzi wa Raia Mwema umebaini kwamba mvutano kati ya Jeetu na Manji, umechangia kwa kiasi kikubwa kuchelewa kwa mchakato wa upatikanaji wa matrekta hayo kwa ajili ya mradi wa Kilimo Kwanza, mradi wenye thamani ya Sh bilioni 50.

Habari zinaeleza kwamba, kwa kutumia mtandao wa mmoja wa wafanyabiashara hao, baadhi ya maofisa wa Serikali wametumika kuuchelewesha na hivyo kuhujumu mchakato wa kukamilishwa kwa taratibu za uidhinishwaji wa fedha za ununuzi wa matrekta hayo.

Mradi huo uliokabidhiwa kwa Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) kupitia kampuni yake ya SUMA JKT, ulitakiwa kuanza mapema mwaka huu, lakini hauna dalili za kuanza kutokana na utata wa kisheria ulioilazimu Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG) kuingilia kati.

Raia Mwema imethibitishiwa kwamba kampuni mbili za nchini India zilizoshiriki zabuni hiyo moja ikiwa imepata sehemu kubwa ya kazi ya kuingiza matrekta hayo, zimeridhishwa na mchakato wa zabuni hizo, lakini tatizo limekuwa kwa mawakala wao nchini ambao ni Manji na Jeetu.

Malumbano hayo yameelezwa kuwagusa hata watendaji wa juu serikalini kabla ya uongozi wa juu wa Ofisi ya Mwanasheria Mkuu kuingilia kati na kuamuru suala hilo likamilishwe na taarifa ziwasilishwe Wizara ya Fedha na Uchumi.

Katibu Mkuu Wizara ya Fedha na Uchumi, Ramadhani Kijjah, ameliambia Raia Mwema kwamba Wizara yake haikuhusika kwa namna yoyote na ucheleweshaji wa mchakato wa Kilimo Kwanza kwa maelezo kwamba kilichochelewesha ni ushauri wa kisheria kutoka Ofisi ya Mwanasheria Mkuu, jambo ambalo amesema sasa limeshapatiwa ufumbuzi.

“Hakukuwa na tatizo la kiuhasibu ama kiuchumi. Lilikuwa ni tatizo la kisheria ambalo sisi hatuhusiki. Watu wa Exim Bank ambao ndio watoaji wa mkopo walitaka maoni ya kisheria kutoka serikalini na sisi tulilazimika kuwapelekea Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali. Kwa sasa ndiyo wametuletea na tumewapelekea Exim, wakishapitia watatujulisha kama wameridhika ama la,” alisema Kijjah.

Kijjah alisema fedha hizo ni mkopo kutoka serikali ya India kupitia Exim Bank, japo ni kwa riba nafuu mno kuliko ile ya taasisi nyingine za fedha na kwamba utalipwa na Watanzania wote wakati wake ukifika na hivyo ni lazima Serikali ijiridhishe na kila hatua kuhusiana na matumizi yake.

Kumekuwa na maoni tofauti kuhusiana na jinsi Serikali ilivyolibeba suala la ununuzi wa matrekta hayo kutokana na kuhusishwa tena kwa wafanyabiashara ambao wamekuwa wakihusishwa katika kashfa mbalimbali ikiwamo kashfa maarufu ya wizi wa Fedha za Mfuko wa Madeni ya Nje Benki Kuu ya Tanzania (EPA).

Mwishoni mwa mwaka jana baadhi ya vyombo vya habari vilimnukuu Manji akizungumzia kwa kina kuhusiana na zabuni hiyo ya matrekta ya Kilimo Kwanza, lakini Jeetu Patel amekuwa kimya kuhusiana na suala hilo akikwepa kuhusishwa nalo.

Raia Mwema ilipomuuliza Jeetu Patel kuhusiana na suala hilo alikataa kata kata kulifahamu akidai kwamba hajawahi kuhusika kwa vyovyote katika zabuni hiyo na hana cha kuzungumza akisema, “sifahamu lolote kuhusu biashara hiyo… sina cha kuzungumza, ama unataka nikudanganye?”

Kwa upande wake Manji alitoa taarifa akidai kutoridhishwa kwake na mchakato wa zabuni hiyo ambayo imeelezwa kwamba tatizo kubwa lilikuwa ni “kuzidiana kete” kati ya wafanyabiashara hao wa Tanzania, katika kamisheni ambayo ingetokana na biashara hiyo kutoka kampuni za nchini India.

Katika mradi huo, Jeetu anatajwa kuwa mwakilishi wa Kampuni ya Escort hapa nchini, yenye makao makuu yake nchini India, ambayo imeshinda zabuni hiyo, wakati Manji anatajwa kuwakilisha kampuni ya Mahindra ya India, ambayo nayo imepata kiasi kidogo cha zabuni hiyo.

Hata hivyo, baadaye Manji ambaye ni mmiliki kampuni ya Quality Group, alinukuliwa na gazeti la serikali la Habari Leo akisema kwamba ameridhishwa na mchakato wa zabuni hiyo na kukanusha taarifa za awali kwamba amekuwa akitaka kuanika anachofahamu kitakacholenga kuchafua wahusika katika zabuni hiyo ikiwamo JKT.

Awali ilielezwa kwamba zabuni hiyo ya matrekta ilipitishwa ngazi zote ikiwamo hatua ya Baraza la Mawaziri na kupatiwa baraka zote za kulitekeleza na Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga, Dk. Hussein Mwinyi, alinukuliwa akisema kwamba hakuna utata wowote katika utekelezaji wa mradi huo, isipokuwa linaweza kufanywa ajenda ya kuchafuana na watu ambao wana malengo binafsi na mradi huo.

Dk. Mwinyi alinukuliwa akisema kwamba kampuni zaidi ya 10 ziliomba zabuni hiyo na hatua zote zilipitiwa kwa uangalifu mkubwa na kwamba watakaolalamika wanalenga kuchafuana kwa malengo binafsi.

No comments: