Monday, January 18, 2010

KAMATI YA BUNGE YAKATAA RIPOTI YA BODI YA MIKOPO!!!

Kamati ya Hesabu za Serikali na Mashirika ya Umma imekataa kupokea ripoti ya hesabu ya Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu (HESLB) baada ya bodi hiyo kushindwa kuchanganua matumizi ya Sh33.9 bilioni.
Kati ya fedha ambazo bodi hiyo ilishindwa kutoa mchanganuo, Sh12.9 bilioni ni marejesho ya mikopo iliyotolewa kwa wanafunzi katika vyuo mbalimbali vya elimu ya juu kama ada ya masomo na posho.
Ripoti hiyo iliyowasislishwa na bodi ya wakurugenzi wa HESLB ikiongozwa na mwenyekiti wakezi, Anselim Lwoga haina mchanganuo wa matumizi ya Sh21 bilioni zilizotolewa na Wizara ya Fedha.
"Hii ripoti hatutaipitisha lakini nendeni mkaipitie tena tukutane Dodoma... kabla vikao vya Bunge havijaanza muilete ikiwa imechanganuliwa nama fedha hizo zilivyotumika,"alisema Kilasi na kuongeza.
"Ripoti hii tulishaipitia wakati fulani na tukawaandikia barua ya kutaka watuletee kwa maandishi lakini hawakufanya hivyo."
Kilasi alisema matumizi ni makubwa kuliko hata kiasi cha fedha wanazoingiza kitu ambacho ni hatari kwenye utawala wowote ule.
Kama hiyo haitoshi bodi hiyo imebainika kufanya uzembe kwa kushindwa kuomba serikalini Sh58 bilioni katika bajeti yao ya kila mwaka ili iweze kulipa deni inalodaiwa kwa kuwa serikali ndio iliyoidhamini mkopo huo.
"Hawa walitakiwa kila bajeti watoe mchanganuo wa deni la Sh58 bilioni ambalo serikali iliwadhamini kwa ajili ya kutoa mikopo kwa wanafunzi wa elimu ya juu, lakini wameshindwa kufanya hivyo hali ambayo inawalazimu kuangalia namna watakavyweza kulilipa deni hilo," alisema Kilasi.
Hata hivyo kamati hiyo ilishangazwa na bodi hiyo kwa kutokuwa na mkurugenzi kwa muda wa miaka miwili. Nafasi hiyo inashikiliwa na kaimu mkurugenzi, Yusufu Kisare.
Kamati hiyo ilibaini kutokuwepo kwa mkurugenzi wakati wa utambulisho baada ya Kisare kujitambulisha kuwa anakaimu na alipoulizwa mwenye nafasi hiyo yuko wapi, alijibu kuwa alisimamishwa kazi na serikali tangu mwaka 2007
Kumekuwa na utata mkubwa katika swala la wanafunzi kupewa mikopo na serikali kupitia bodi ya mikopo, Je mnafikiri tatizo hili liko wapi katia ya watekelezaji na sera au sera zenyewe? Leo jioni tutatuma maoni mbali mbali ya wanafunzi wa chuo kikuu cha Dar-es-salaam UDSM wakiongelea juu ya mikopo kwa wanafunzi.

No comments: