Tuesday, January 26, 2010

Gharama za uchaguzi kutawala Bunge

MKUTANO wa 18 wa Bunge unaanza leo mjini hapa, huku ukitarajiwa kutawaliwa na mjadala kuhusu mambo mbalimbali, ikiwamo Miswada ya Sheria ya Gharama za Uchaguzi na Marekebisho ya Sheria za Uchaguzi.

Huu ni mkutano wa kwanza kati ya mitatu iliyobakia ambayo inakamilisha kipindi kilichoanza mwaka 2005 huku baadhi ya wabunge wakisema muswada wa gharama za uchaguzi umekuja wakati muafaka.

Akizungumza na waandishi wa habari jana, Ofisa Habari Mkuu wa Bunge, Ernest Zulu, alisema kikao cha leo kitaanza na maswali na majibu.

Baadaye kutakuwa na kikao cha wabunge kinacholenga kutoa ufafanuzi kuhusu maazimio yaliyofikiwa na Kamati ya Uongozi kuhusu Mkutano wa 18 kabla ya kuanza vikao vya Kamati za Vyama vya Siasa.

Katika mkutano huu miswada minane inatarajiwa kuwasilishwa na kujadiliwa. Nayo ni wa Sheria ya Uuguzi na Ukunga ya mwaka 2009; Sheria ya Mawasiliano na Eletroniki na Posta 2009; Sheria ya Kurekebisha Sheria mbalimbali, Sheria ya Usajili wa Wabunifu Majengo, Wakadiriaji Majengo 2009 na wa Sheria ya Nyongeza wa 2009/10.

Pamoja na miswada hiyo ambayo baadhi yao inatarajiwa kuanzisha mjadala mkali bungeni, pia maazimio matano yatawasilishwa likiwamo la Kuridhia Mkataba wa Kimataifa wa pamoja wa nchi za Jumuiya ya Maendeleo ya Nchi za Kusini mwa Afrika (SADC).

Lingine ni la kulinda hakimiliki za wagunduzi wa aina mpya za mimea; la Bunge la Kuridhia Itifaki ya Jinsia na Maendeleo ya SADC na la Kuridhia kuanzishwa Mkataba wa Kamisheni ya Maji ya Mto Zambezi ambalo lilibaki katika maazimo yaliyopitishwa katika mkutano wa 17 uliomalizika mwaka wa jana. Katika mkutano huu, Bunge litapata taarifa ya ufafanuzi kuhusu hoja binafsi iliyowasilishwa na Mbunge wa Ngorongoro, Aika Telele (CCM) katika mkutano wa 17 kuhusu vitendo vya ukiukwaji wa haki za binadamu katika kuhamisha jamii ya wafugaji katika msitu wa hifadhi ya Loliondo.

Ingawa taarifa kamili ya yatakayojiri katika mkutano huu wa Bunge haikutolewa rasmi jana, ripoti ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini itawasilisha taarifa ya utekelezaji ya Serikali kuhusu mkataba tata wa kampuni ya Richmond.

Mambo mengine yanayotajwa kuchukua nafasi katika mkutano huu ni madai ya Mgodi wa North Mara ya kutiririsha maji ya sumu katika Mto Tigite. Baadhi ya wabunge waliozungumza na gazeti hili, walisema miongoni mwa miswada muhimu ikizingatiwa na wakati uliopo wa kuelekea uchaguzi, ni wa gharama za uchaguzi.

“Bunge hili litakuwa limefanya kazi nzuri likipitisha muswada huu. Ipo changamoto kubwa, kwa sababu kuna baadhi ya watu hawaupendi. Lakini ni vizuri sheria hii iwepo,” alisema Mbunge wa Tabora Mjini, Siraju Kaboyonga (CCM).

Alisema anaona suala kuhusu mgodi wa Kiwira ambalo pia litajadiliwa bungeni na la Richmond, kwake hayana umuhimu mkubwa kama ilivyo kwa muswada wa Sheria ya gharama za uchaguzi.

“Muswada huu umekuja wakati muafaka. Naipongeza Serikali. Haya masuala sijui Richmond, Kiwira haya ni mambo ya kawaida. Kwa mfano suala la Richmond, Serikali inakuja kusema imefanya nini katika kutekeleza mapendekezo 23 na hatimaye suala hili lifungwe,” alisema Kaboyonga.

No comments: