Tuesday, January 19, 2010

Mgogoro wa ardhi Hanang': Kwanza wakulima, sasa wafugaji

BAADA ya jamii ya wafugaji wa Kibarbaig wa vijiji vya Mogitu, Ming’enyi na Dawar wilayani Hanang’ mkoani Manyara kuizuia serikali wilayani humo kugawa ardhi yao, mgogoro huo sasa umehamia kwa wakulima wa vijiji hivyo baada kamati iliyokuwa ikisuluhisha kupendekeza ardhi ya wakulima hao imegwe kwa ajili ya wananchi wanaohamishwa kutoka eneo la Mlima Hanang’.

Wafugaji wa Kibarbaig kati ya Desemba 16-19 mwaka jana walitangaza “vita” dhidi ya serikali kupinga mpango wa Halmashauri ya Wilaya ya Hanang’ wa kugawa ardhi ya iliyokuwa shamba la mradi wa ngano la Warett lenye ukubwa ekari zaidi ya 16,000.

Wafugaji hao wakiwa wamejihami kwa silaha za jadi walikimbilia katika msitu ulioko jirani na kijiji hicho baada Polisi kuwakamata baadhi ya wafugaji hao wakiwamo viongozi wa serikali za vijiji.

Wananchi hao pia walitoa madai mazito kuwa Polisi na watendaji waliokuwa wakiendesha operesheni ya kuwakamata walikiuka haki za binadamu kwa kuwapiga, kuwanyima chakula, na kuwaweka mahabusu kwa siku tatu bila ya kuwafikisha mahakamani.

Hata hivyo, baada vurugu hizo na kuhofiwa kutokea kwa umwagaji damu uongozi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Manyara ukiongozwa na Mwenyekiti Luka ole Mukusi, uliunda kamati maalumu ya kutafuta muafaka kuhusu mgogoro huo.

Baada ya kufanyika vikao vya usuluhishi kwa wiki nzima kamati hiyo ilikubaliana na wananchi kuwa Halmashauri imesitisha mpango wa kugawa eneo lililokuwa limetengwa kwa ajili malisho lakini kungefanyika uhakiki wa ardhi iliyogawiwa kwa wakulima.

Katika mapendekezo hayo kamati hiyo iliweka bayana kuwa wakulima ambao walikuwa na maeneo makubwa yangemegwa ili wananchi wanaohamishwa kutoka mlima Hanang’ wapatiwe ardhi.

Ole Mukusi alithibitishia Raia Mwema kuwa ni kweli walikubaliana kufanya zoezi la kuhakiki watu waliogawiwa ardhi na ukubwa wa maeneo yao kwa wananchi wenye kuhitaji ardhi.

“Zoezi tayari limekwisha kuanza kuanzia tarehe 5 Januari na linatarajiwa kumalizika Januri 20 ili wananchi waweze kuendelea na shughuli ya kilimo kwani huu ni msimu wake…..tumechukua uamuzi huu kutokana na wasiwasi kuwa ugawaji ardhi uliofanywa awali haukufuata taratibu,” alisema.

Mwenyekiti huyo alisema wakati wa utekelezaji wa zoezi hilo viongozi na watendaji wa serikali watashirikiana na wazee wa kimila wa makabila ya Wabarbaig na Wairaq na kila mkulima atalazimika kusimama katika eneo lake.

“Sababu kubwa ya kufanya hivyo ni kutokana na madai kuwa kuna baadhi ya watu wamepewa maeneo makubwa ya ardhi wakati wa mgao wa kwanza uliosimamiwa na viongozi wa vijiji husika, ”alisema.

Ole Mukusi alisema CCM kama chama tawala kiliona umuhimu wa kutafuta suluhu ya mgogoro huo kutokana na mazingira yaliyojitokeza ambapo wananchi walitaka kujichukulia sheria mkononi.

Soma zaidi

No comments: