Wednesday, October 31, 2012

TGNP Yalaani Vitendo Vya Mkuu wa Wilaya ya Handeni, Mhe. Muhingo Rweyemamu Vya Kuwakamata Wasichana Waliopata Ujauzito


Taarifa kwa vyombo vya habari


Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP), Shirika linalofanya kazi za kutetea masuala ya kijinsia, haki za wanawake na wasichana ikiwemo haki ya uzazi salama tumeshtushwa na kusikitishwa na kauli iliyotolewa na Mkuu wa Wilaya ya Handeni Mkoani Tanga Ndugu Muhingo Rweyemamu, kuhusu kukamatwa na kufungwa kwa wasichana waliopata mimba kama njia ya kushinikiza watoe majina ya wanaume waliowapa mimba. Habari hizi zimeandikaa katika gazeti la the Citizen la tarehe 26 Oktoba 2012 na athari zake kwa wasichana kuchambuliwa zaidi na gazeti hilo hilo tarehe 27 Oktoba 2012

Inasemekana kuwa wasichana mashuleni katika Wilaya ya Handeni wanalazimishwa kupimwa ujauzito na wanapokutwa na ujauzito wanafukuzwa shule. Wasichana hawa hupelekwa polisi kwa mahojiano zaidi endapo watakataa kuwataja wanaume waliowapa mimba.

Vitendo hivi vya udhalilishaji vimetolewa taarifa kwenye mikoa mingine ya Tanzania ikiwemo mikoa ya Mbeya na Iringa. Swali la kujiuliza ni kwa nini msichana aadhibiwe vikali namna hiyo?adhabu ya kwanza kupata ujauzito akiwa mwanafunzi/umri mdogo, adhabu ya pili anafukuzwa shule/ nyumbani na dhabu nyingine akamatwe na kupelekwa polisi. Tunaelewa kuwa kuna mazingira mengi hatarishi yanayochangia mtoto wa kike kubakwa na kupata ujauzito, ukiwemo umbali wa kutoka nyumbani hadi shuleni,ukosefu wa mabweni, gharama mbali mbali ikiwemo michango ya shule, mazingira duni ya kujifunzia na kufundishia, ukosefu wa chakula cha mchana, watoto wa kike hushawishiwa kujiingiza kwenye kubakwa na hatimaye kupata ujauzito na kukatishwa masomo.

Mfumo wa elimu yetu ya Tanzania unaendeleza matabaka kwani wasichana wachache wanakwenda kwenye shule nzuri na kwa gharama kubwa na hata wakipata ujauzito wanaweza kutoa hizo mimba!!!bali wasichana walio wengi wanakwenda kwenye shule zisizo na rasilimali za kutosha hasa maeneo ya vijijini na ndiyo wanaofukuzwa wakipata ujauzito. Mfano katika utafiti wa kiraghbishi uliofanywa na Mtandao wa Jinsia Tanzania mwaka huu kwenye vijiji vitatu vya Kata ya Songwa, Mkoa wa Shinyanga wasichana 38 kwa muda wa miaka 2 walikatishwa masomo kutokana na ujauzito.

Kutokana na vitendo hivyo vya udhalilishwaji, sisi kama wanaharakati wa masuala ya usawa wa kijinsia, haki za kibinadamu na demokrasia tumechukizwa sana na tunalaani vikali vitendo na kauli hii ya mkuu wa wilaya na tunakemea na kusema yafuatayo:

Madai yetu kwa Mkuu wa Wilaya ya Handeni

1. Kuacha mara moja kuwakamata wasichana wanaopata ujauzito na kuwatoa mara moja wale ambao tayari wamepelekwa jela. Pamoja na kuzindua hiyo KAMPENI ya NIACHE NISOME, atuambie kama imeingizwa kwenye mpango mkakati wa wilaya na umetengewe rasilimali kiasi gani na za kufanya nini???

2. Atuweke wazi utaratibu anaotumia kuwawajibisha wahusika kwani kuna taratibu za kisheria zinabidi kufuatwa ili kuwabana na kama hospitali ya Wilaya ya Handeni ina mashine ya kupima DNA itakuwa Hospitali ya Mfano? Je kama haina anapaswa kuwajibika??

Madai yetu kwa Serikali ya Jamhuri ya Tanzania

1.Kumlazimisha msichana kufanya vipimo vya ujauzito ni ukiukwaji wa haki na uhuru wa mwili wa msichana husika na ujauzito unatumiwa kama kigezo cha kumfukuza shule.

2. Elimu juu ya afya ya uzazi, ikiwemo mbinu za uzazi salama lazima ziwekwe wazi na kufikiwa na wasichana wote na zitolewe bila kuwepo na unyanyapaa wowote

3. Lazima kuwepo na ulinzi wa kutosha kwa wasichana na haki ya kufikia elimu bora na nafasi za ajira, maisha endelevu na huduma za afya ya uzazi ambazo zinathamini ustawi wa msichana

4. Sheria ya makosa ya kujamiiana ya mwaka 1998 lazima irekebishwe na kuwepo kipengele kinachotoa si adhabu kali tu kwa wanaume wanaowapa mimba wasichana, bali kiongezwe kipengele cha kuhakikisha matunzo ya mtoto na huyo binti na liwe ni suala la kikatiba

Kutokana na kauli ya DC tunatoa wito kwa mamlaka ya serikali ya wilaya ya Handeni na sehemu nyingine popote,ya kuweka mazingira endelevu kwa watoto wa kike kulindwa na kufikia malengo yao bila ya kukandamizwa zaidi.

Tunatoa wito kwa wahusika wote na mamlaka za serikali kuchukua hatua za haraka za kutoa elimu ya afya ya uzazi ikiwemo uzazi salama kwa wasichana na jamii nzima na uingizwe kwenye mitaala ya elimu; kusaidia upanuzi wa usalama wa maisha endelevu kwa wasichana na mazingira rafiki ya kufanyia kazi kwa wote wanawake, wanaume, vijana hasa walioko pembezoni.

Tunatoa wito kwa famillia zote, kutoa kipaumbele kwenye mahitaji maalum ya wasichana na kuwapa msaada wanaohitaji katika kufikia elimu bora, afya ya uzazi salama na maisha endelevu na yenye heshima.

Kamwe haki ya msichana haikuzwi kwa kumtupa jela ni kwa kumpa elimu bora ili aweze kufikia ndoto yake ya hapo baadae.

Imetolewa Dar es salaam leo 31/10/2012 na

......................

Lilian Liundi
Kaimu Mkrugenzi Mtendaji TGNP

No comments: