Monday, October 29, 2012

Ni Ndoto Kupata Katiba Mpya Ifikapo Mwaka 2014: Hali Halisi ya Ushiriki wa Wanawake katika Mchakato wa Kutoa Maoni



Na Kenny Ngomuo - TGNP
Watanzania tumeingia katika historia ya mchakato wa kuandika Katiba mpya ambao ni shirikishi huku  wengi wetu tukiwepo katika  harakati mbalimbali za kimaendeleo hasa zile zakutafuta kipato na kuwakomboa  kutokana na maisha duni yaliyojaa mifumo kandamizi inayotokana na mila na tamaduni zilizowazunguka hasa watanzania walioko pembezoni. 

Pamoja na wanawake kuwa wazalishaji wakuu katika jamii kuanzia ngazi ya familia wanawake wamekuwa waathirika wakubwa na michango yao imekuwa hautambuliki katika pato la taifa. Suala la kwa nini wanawake na wasichana wamebakia pembezoni katika nchi nyingi zinazoendelea ni dhana pana yenye mizizi ya kihistoria, utamaduni, dini na hata saikolojia yenyewe. Matokeo ya utafiti uliofanyika katika nchi za dunia ya tatu na Umoja wa Mataifa, yameonesha kuwa wanawake  walio wengi katika nchi nyingi zinazoendelea bado  wanazidi kuishi maisha duni siku hadi siku ikiongozwa na mifumo kandamizi.. 

Utafiti uliofanyika na Mtandao wa Jinsia Tanzania mwaka 2009  kuhusu kazi  wanazofanya wanawake zisizo na malipo, mfano kuhudumia wagonjwa majumbani, kulea watoto na  wazee ulionesha wazi kuwa wanawake wanatumia nguvu na muda mwingi ambao hautambuliki popote katika pato la taifa. Utafiti uliofanywa na Programu ya Chakula Duniani (World Food Programme)  pia umeonesha kuwa mwanamke anatumia  zaidi ya asilimia 90% ya pato lake kila mwezi  katika familia kwa njia ya aidha kununua  chakula, vitabu na madaftari ya watoto, dawa , neti za kujikinga na mbu kwa ajili ya watoto wao na huduma nyinginezo zinazofanana na hizo.

Pamoja na changamoto nyingi ambazo wanawake wamekumbana nazo katika harakati zao za kujikomboa, wanawake wamekuwa msitari wa mbele katika shughuli zote za kimaendeleo katika nyanja zote za kisiasa, kiuchumi na kiutamaduni.

Mchakato wa ukusanyaji wa maoni ya kuandika  Katiba mpya iko katika awamu ya pili .  Zoezi hili limekwenda vizuri hasa kwenye maandalizi na kuwepo kwa vifaa vya kuwezesha wananchi kuendelea kushiriki katika kutoa maoni yao ya masuala ambayo wangependa  yaingie katika Katiba mpya. Pamoja na mambo kadhaa mazuri, bado kumeendelea kujitokeza mapungufu ambayo yanahitaji kurekebishwa ili kuweza kuboresha ufanisi wa ukusanywaji wa maoni katika mikoa ambayo imesalia  ambayo ni takrikbali mikoa 15 sawa na asilimia 50% ya mikoa yote ya Tanzania. Hii ni kutokana na utafiti uliofanyika mwezi  Agosti na Septemba  2012 na Jukwaa la Katiba Tanzania.

Hata hivyo, imebainika kwamba mikutano mingi inafanyika muda wa asubuhi kuanzia saa 3 asubuhi hadi saa 6 mchana na baadaye mchana kuanzia saa 8 hadi 11. Kwa uhalisia mikutano ya asubuhi haijawa rafiki kwa wanawake hasa wale wanaoishi vijijini, ambao  muda mwingi wa asubuhi wako katika  shughuli za uzalishaji mali na kujitafutia kipato, ambapo hata mijini pia muda bado ni changamoto. 

Mfano, Jukwaa la Katiba Tanzania lilipewa taarifa walipotembelea Kata ya Mwakaleli mkoani Mbeya, kuwa mikutano ya asubuhi iliwanyima fursa  ya kutoa maoni wananchi wengi sana waliokuwa katika shughuli za uzalishaji mashambani ambao wengi wao ni wanawake. Katika Mkoa wa Ruvuma, tatizo lilipelekea uwiano wa wanawake na wanaume katika kushiriki mchakato wa utoaji maoni kuwa mbovu sana. Kwa mujibu wa takwimu zilizopatikana, idadi ya wanawake walioshiriki katika takribani mikutano 21 ya wilaya za Tunduru na Namtumbo mkoani Ruvuma ilikuwa ni 1,949 tu kati ya jumla ya wananchi 8,915 sawa na asilimia 22% tu. Aidha, kutokana na uhamasishaji duni kwa wanawake, hata uchangiaji katika kutoa maoni ulishuhudia wanawake wakichangia kwa idadi ndogo sana ya 198 tu kati ya wananchi wote 2,074 waliotoa maoni kwa Tume, sawa na asilimia 9.5% tu.

Kundi lingine ambalo limesahaulika ni hili lenye mahitaji muhimu hasa watu wanaoishi na ulemavu wa aina mbali mbali. Bado watu wenye ulemavu wa kuona, kusikia na kuongea hawajaweza kupewa fursa kubwa ya kuweza kushiriki vema kutoa maoni yao. Hii ni kutokana na Tume kuendelea kuitisha mikutano hii mbali na makazi ya wananchi walio wengi. Pia Tume haijaweza kuandaa miundombinu kama vyombo maalum kwa wasioona na wakalimani wa lugha za alama kwa wale wasio na uwezo wa kusikia na kuzungumza.
Natoa mapendekezo yafuatayo kwa Tume ya Mabadiliko ya Katiba mpya:

1) Tume ya Mabadiliko ya Katiba mpya ihakikishe inawafikia wananchi  walioko pembezoni hasa wanawake ambao kero zao nyingi zimekuwepo kwa muda mrefu bila kufanyiwa kazi kutokana na mifumo, sera na sheria ambazo bado kandamizi na mfumo dume uliokithiri

2) Tume ya Mabadiliko ya Katiba ni lazima iwasiliane na wataalam wa lugha za alama na wataalam wengine na kuongozana nao mikoani na wilayani ili watanzania wote wakiwemo walemavu waweze kufikiwa na kutoa maoni yao kwa ajili ya Katiba mpya ijayo

3) Tume  ifanye utafiti kwa kila eneo wanalokwenda  ili kubainisha muda ambao ni rafiki kwa kila mwananchi aweze kushiriki  na hili liende sambamba na matangazo ya kuwahamasisha wananchi kujitokeza kwa wingi kwenye mikutano ya kutoa maoni 

4)  Mchakato wa Katiba Mpya, uendelee kwa kasi ya kawaida na kwa umakini mkubwa bila kukimbizana ili tuweze kupitia hatua zote za kuandika Katiba mpya ambayo ni shirikishi ya kihistoria na ya kidemokrasia.

No comments: