Friday, October 19, 2012

RIPOTI YA UFUATILIAJI WA MCHAKATO WA UKUSANYAJI MAONI KWA AJILI YA UUNDAJI WA KATIBA MPYA TANZANIA (AWAMU YA PILI)



Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP)
P.O Box 8921 Dar es Salaam
RIPOTI YA UFUATILIAJI WA MCHAKATO WA UKUSANYAJI MAONI KWA AJILI YA UUNDAJI WA KATIBA MPYA TANZANIA (AWAMU YA PILI).

Tume ya mabadiliko ya Katiba mpya iko katika awamu ya pili ya ukusanyaji wa maoni ya wananchi kwa ajili ya uundaji wa katiba mpya.  Zoezi hili limekwenda vizuri hasa kwenye maandalizi na kuwepo kwa vifaa vya kuwezesha wananchi kuendelea kushiriki katika kutoa maoni yao ya masuala ambayo wangependa  yaingie katika katuba mpya. Vile vile kumekuwepo na utulivu na ukarimu kwa wananchi walioweza kuhudhuria zoezi la kutoa maoni hasa kwenye mikoa ambayo wajumbe wa Jukwaa la Katiba wameweza kufikia. 

Pamoja na mambo kadhaa mazuri, bado kumeendelea kujitokeza mapungufu ambayo yanahitaji kurekebishwa ili kuweza kuboresha ufanisi wa ukusanywaji wa maoni katika mikoa 15 ambayo imesalia sawa na Asilimia 50 ya mikoa yote ya Tanzania.

  • MUDA AMBAO MIKUTANO HUITISHWA BADO NI MBAYA !
Ilibainika kwamba mikutano mingi ilifanyika muda wa asubuhi kuanzia saa 3 asubuhi hadi saa 6 mchana na baadaye mchana kuanzia saa 8 hadi 11. Kwa uhalisia mikutano ya asubuhi haijawa muafaka hasa kwa wakazi wa vijijini, ambao wako katika uzalishaji mali. Katika kata ya Mwakaleli mkoani Mbeya JUKWAA LA KATIBA lililalamikiwa kuwa mikutano ya asubuhi iliwanyima fursa wananchi wengi sana waliokuwa katika shughuli za uzalishaji mashambani. Hata katika maeneo ya mijini kama vile Manispaa ya Morogoro na wilaya ya Mvomero, watumishi wengi wakiwemo wa umma na serikali walilalamikia kutokuwepo utaratibu unaojulikana kuwa siku Tume inapokusanya maoni katika maeneo yao basi wawe na ruhusa ya kutofika kazini au kuruhusiwa mapema

  • VITUO VYA KUKUSANYA MAONI KUWA VICHACHE KILA WILAYA
Waangalizi wetu walipokea malalamiko toka kwa wananchi juu ya Tume kuruka Kata nyingi mno katika kukusanya maoni. Hii ilichangia sana kwa Wananchi wengi hasa katika vijiji visivyopitiwa na barabara kuu za lami kutojua hata endapo wilaya zao zilikuwa zimeshapitiwa na Tume au bado. Katika moja ya Ziara ambazo JUKWAA LA KATIBA lilifanya katika mikoa ya Singida na Simiyu kupitia iguguno, Mwando, Nduguti, Kamlungu, Maheli, Gumanga, Igunia, Mkalama, Ibaga, Chemchem, Bukundi, Itaba hadi Meatu, wanavijiji wengi walionekana kutojua kabisa kama kuna mchakato unaoendelea wa Katiba Mpya na endapo mikoa na wilaya zao zilikuwa zimekwishafikiwa au bado.

  • RATIBA ZA TUME KUBANA UHAMASISHAJI NA MATANGAZO KUHUSU MIKUTANO YA UKUSANYAJI MAONI KABLA YA SIKU.
Pamoja na Tume kuchelewa kutoa Ratiba ya awamu ya pili, kwa maeneo mengi Tume ilitoa kwa kuchelewa matangazo ya kuwahamasisha wananchi kujitokeza kwa wingi kwenye mikutano ya kutoa maoni hivyo kusababisha wananchi wachache kuhudhuria mikutano hiyo tofauti na ilivyotarajiwa. Katika maeneo mengi ya Mkoa wa Morogoro, kulikuwa na malalamiko kuwa Tume ilichelewa sana kutangaza kuwa kutakuwa na mikutano na hivyo kusababisha wananchi wengi kukosa fursa ya kutoa maoni yao.. 

  • USHIRIKI MDOGO WA WANAWAKE
 Katika Mkoa wa Ruvuma, tatizo lilipelekea uwiano wa wanawake na wanaume katika kushiriki mchakato wa utoaji maoni kuwa mbovu sana. Kwa mujibu wa takwimu zilizopatikana, idadi ya wanawake walioshiriki mikutano katika mikutano takribani 21 ya wilaya za Tunduru na Namtumbo mkoani Ruvuma ilikuwa ni 1,949 tu kati ya jumla ya wananchi 8,915 sawa na asilimia 22% tu. Aidha, kutokana na makosa hayo ya uhamasishaji duni kwa wanawake, hata uchangiaji katika kutoa maoni ulishuhudia wanawake wakichangia kwa idadi ndogo sana ya 198 tu kati ya wananchi wote 2,074 waliotoa maoni kwa Tume, sawa na asilimia 9.5% tu, ambayo ni aibu.

  • MAKUNDI YENYE MAHITAJI MAALUM HASA WATU WENYE ULEMAVU BADO YAMESHINDWA KUSHIRIKI KATIKA KUTOA MAONI
Katika awamu hii pia bado watu wenye ulemavu wa kuona, kusikia na kuongea hawajaweza kupewa fursa kubwa ya kuweza kushiriki vema kutoa maoni yao. Hii ni kutokana na Tume kuendelea kuitisha mikutano hii mbali na makazi ya wananchi walio wengi. Pia Tume haijaweza kuandaa miundombinu kama vyombo maalum kwa wasioona na wakalimani wa lugha za alama kwa wale wasio na uwezo wa kusikia na kuzungumza. Katika hatua za awali za kupanga awamu hii ya ukusanyaji maoni, Tume ilijaribu kuwasiliana na wataalamu wa lugha za alama lakini kwa mshangao mkubwa Tume ikabadilika ghafla na kusema ingekuwa gharama mno kutumia wataalam hao wa lugha za alama kuongozana nao mikoani na mawilayani.

Hii imewanyima wananchi hawa haki yao ya kikatiba ya kuweza kuchangia maoni yao kwa ufasaha. Hivyo, JUKWAA LA KATIBA TANZANIA bado linaishauri Tume kurekebisha suala hili nyeti kwa haraka iwezekanavyo ili kutoa fursa kwa kundi hili la wananchi kutoa maoni yao kwa ufasaha, kwa kuwa fedha zipo tena kwa kiasi cha bajeti ya shilingi bilioni 34 kwa mwaka huu tu wa Fedha. Hiki ni kiasi kikubwa cha fedha kinacholingana na hata kuzidi baadhi ya wizara za serikali ya Tanzania!  

  • MAKADIRIO YA KATIBA MPYA KUPATIKANA IFIKAPO APRILI 2014 SI HALISIA.
Kutokana na kusuasua kwa mchakato unaendelea wa ukusanyaji maoni, na hamasa ndogo miongoni mwa wananchi juu ya Mchakato wenyewe wa Katiba Mpya huku sheria ya Mabadiliko ya Katiba, sura ya 83 ya Sheria (2012) ikiipa Tume ya Mabadiliko ya Katiba mamlaka hodhi ya kufanya karibu kila kitu katika Mchakato huu, inaanza kujidhihirisha wazi kuwa ni jambo lisilowezekana kukamilisha hatua zote za Mchakato wa Kupata Katiba Mpya ifikapo mwezi Aprili, 2014. Kwa mfano elimu ya uraia inayotolewa ni finyu na haba kutokana na kubanwa na sheria husika

MAPENDEKEZO
1)  Mchakato wa Katiba Tanzania hautazaa Katiba Mpya ifikapo Aprili, 2014 na hivyo ipo haja ya kuanza kujiandaa kwa hilo. 

2)  Kwa kuwa sababu kubwa ya kukimbiza mchakato wa katiba Mpya ni haja ya wanasiasa kupata Katiba Mpya itakayotumika katika uchaguzi wa mwaka 2015, JUKWAA LA KATIBA tunapendekeza kuwa zipo njia mbadala za kuwezesha uchaguzi ufanyike kwa salama, amani na utulivu hata bila kulazimika kukimbiza mchakato wa Katiba mpya 

3)  Kwa kuwa kikwazo kikubwa katika kufanyika kwa uchaguzi kwa kutumia Katiba ya sasa ni Tume ya sasa ya Taifa ya Uchaguzi ambayo uhuru na ufanisi wake unatiliwa mashaka, JUKWAA LA KATIBA tunapendekeza kuwa kufanyike marekebisho makubwa kupitia ibara ya 98 ya Katiba ya sasa katika vipengele vinavyohusiana na Tume ya Uchaguzi na usimamizi mzima wa uchaguzi ili ifikapo April 2014 tuwe tuna ibara za Katiba zinazoweka Tume huru na yenye ufanisi ili hatimaye ipewe jukumu la kusimamia chaguzi zote zitakazofuata baada ya April, 2014 ikiwemo: Uchaguzi wa serikali za Mitaa, mwishoni mwa 2014; uchaguzi mkuu 2015 na uchaguzi wa wajumbe watakaohitajika katika vyombo vya kujadili na kupitisha Katiba Mpya ya Tanzania. 

4)  Kuhusu Mchakato wa utungaji wa Katiba Mpya, JUKWAA tunapendekeza kuwa uendelee lakini kwa kasi ya kawaida na kwa umakini mkubwa bila kukimbizana ili tuweze kupitia hatua zote za uandishi wa Katiba ya Kidemokrasia hata baada ya uchaguzi Mkuu wa wa 2015.

No comments: