Friday, July 10, 2009

Utenzi wa Haroub Othman

Hapa hakuna kulia
Japo ni kali hisia
Janga lilotufikia
Lino limepindukia

Katika za sasa zama
Tumezipata zahama
Mwenzetu anapohama
Kutuachia dunia

Ni wengi walotutoka
Walotambuka mpaka
Na huko walikofika
Tumeshawasabilia

Jeraha lilo moyoni
Na fundo lilo kooni
In’sani hatuoni
Tutavyoyavumilia

Ela tujipe nafasi
Tupunguze zetu kasi
Mola tusije muasi
Kwa chazi lilozidia

Kenda zake kwa Manani
Atakayebisha nani
Ilobaki ni kuhani
Wale waliobakia

Harubu kenda harudi
Ndiyo yetu sote sudi
Kifo kwetu sote budi
Ahadi ikiwadia

Ela tukome kulia
Matama kujishikia
Tuweze kufurahia
Urithi alotwachia

Japo hakuna rufaa
Kaenda ali shujaa
Na nyingi zake shufaa
Rijali alotimia

Harubu alo azizi
Katimiza yake kazi
Bila kufanya ajizi
Sote tumemridhia

Mwanazuoni mahiri
Wanojua wamekiri
Kaacha wake muhuri
Kila alikopitia

Kawafunza wengi wana
Kwa mawazo yenye kina
Bila kufanya hiyana
Na wala kujivunia

Aliwapenda talibu
Naye hakuwapa tabu
Kuwaonyesha vitabu
Vitavyowasaidia

Nje ya lake darasa
Vichwa alivitakasa
Akijadili siasa
Nchini pia dunia

Alipinga ubeberu
Siasa za makaburu
Akitetea uhuru
Wa insani jumuiya

Tulochunguza kwa dhati
Twajua yake sauti
Mashariki ilo Kati
Akitufafanulia

Wahanga wa Palestina
Na Amerika Latina
Walijua lake jina
Kazi alowafanyia

Mzanzibari halisi
Hakupoteza nafasi
Kuwanasihi watesi
Ghadhabu kupunguzia

Upemba na Uunguja
Hakuiona ni hoja
Nyie nyote ni wamoja
Na mimi ni wenu pia

Muhimu tutende haki
Tusitumie bunduki
Wala pinde na mikuki
Hazitufai ghasia

Lino sanduku la kura
Ndiyo njia ya busara
La sivyo twala hasara
Tutaja likumbukia

Masanduku msibebe
Kura hizo msiibe
Acheni wenu ubabe
Harubu kawaambia

Raia wakihamaki
Wakidai zao haki
Mbona mwaleta mikiki
Moto kuwafyatulia

Wakubwa hakuogopa
Ukweli wao kuwapa
Na waliotoka kapa
Hilo wamejitakia

Kituo ameanzisha
Raia kuwakumbusha
Ari zao kuamsha
Waweze jisimamia

Iko siku inakuja
Wapemba na Waunguja
Watapeana faraja
Harubu alinambia

Leo kinachotuzuga
Na akili kuvuruga
Siasa za lugaluga
Bado twazishabikia

Umma utapoamka
Na hekima kucharuka
Dunia itazinduka
Kuja kutushangilia

Kwa upole akinena
Hajawahi kutukana
Alikuwa muungwana
Wote wanashuhudia

Letu si kuomboleza
Bali ni kumpongeza
Ngwe yake kamaliza
Nyingine katuachia

Kazize tuendeleze
Kiporo tusikilaze
Mpaka nchi ipendeze
Alivyokiitakia

Tumshukuru Saida
Kwa alotupa faida
Mume aso kawaida
Umma kuutumikia

Salamu, binti Yahaya
Pokea za jumuiya
Kwa hii kubwa hidaya
Uliyotutunukia

Ya Harubu buriani
Buriani ya Harubu
Ya Harubu buriani
Sote twakushangilia

Utenzi na: Jenerali Ulimwengu

No comments: