Thursday, November 29, 2012

Jaji chande aikwepa kesi ya Lema

JAJI Mkuu wa Tanzania, Mohamed Othman Chande amejitoa kusikiliza rufaa ya kesi ya aliyekuwa Mbunge wa Arusha Mjini, Godbless Lema, badala yake nafasi yake imechukuliwa na Jaji Bernard Luanda.
Kujitoa kwa jaji mkuu kumekuja ikiwa zimebaki siku tano kusikilizwa upya kwa rufaa hiyo Desemba 4, mwaka huu, baada ya awali Mahakama ya Rufani, kuona rufaa hiyo ilikuwa na dosari.
Mahakama hiyo ilikubali hoja ya wajiburufaa kuwa rufaa hiyo ilikuwa na dosari kutokana na tofauti ya vifungu vya sheria vilivyotumika katika hukumu iliyomvua ubunge Lema na vilivyotumika katika hati ya kukaza hukumu, iliyowasilishwa mahakamani sambamba na rufaa hiyo.
Hata hivyo, kilichomwokoa Lema ni kifungu cha 111 cha Kanuni za Mahakama, ambapo mahakama hiyo ilisema kuwa chini ya kanuni hiyo, dosari hizo zinaweza kurekebishwa.
Jaji Chande ndiye aliyekuwa kiongozi wa jopo la majaji watatu katika kesi hiyo akiwamo Salum Massati na Natalia Kimaro.
Jaji Mkuu aliingia kwenye kesi hiyo akichukua nafasi ya Jaji Mbarouk Salim Mbarouk aliyekuwa amepangwa awali, ambaye sababu za kuondolewa hazikuwekwa wazi.
Wakili wa  Lema, Method Kimomogoro alithibitisha kuwa amepata taarifa kuwa jaji mkuu hatasikiliza rufaa hiyo na badala yake Jaji Luanda ndiye atachukua nafasi yake.
“Ni kweli jaji mkuu hatakuwapo kusikiliza rufaa ya Lema nimewasiliana na Msajili Dar es Salaam ameniambia hatokuwepo kwenye hilo jopo,” alisema Kimomogoro na kuongeza:
Hata hivyo, Wakili Kimomogoro alisema “Huu ni utaratibu wa kawaida wa mahakama kwa kuwa huenda jaji mkuu akawa amesafiri au ana shughuli nyingine.”
Wakili wa wajiburufaa, Alute Mughwai alisema hajapata taarifa kama Jaji Mkuu ameondolewa kwenye jopo hilo kwa kuwa huo si utaratibu wa mahakama kutoa taarifa hizo.
“Mahakama huwa haitoi taarifa, zinawekwa (taarifa) kwenye ubao wa mahakama siku ambayo rufaa inasikilizwa,” alisema.
Aliendelea, “Jaji yeyote atakayepangwa sisi hatuna tatizo kwa kuwa wote ni majaji, wewe uko huko Dar na mimi niko huku bara (Arusha), hivyo unaweza ukazipata taarifa zaidi huko kwa kuwa ndiyo uko jikoni Dar.”

No comments: