Friday, December 18, 2009

Mtandao wamuweka Kikwete njia panda

-Lowassa, Sitta, Rostam, Membe watajwa
-Yeye ajipanga kuwatumia vijana kujihami

WAKATI Halmashauri Kuu (NEC) ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) ikisubiri matokeo ya kamati teule ya rais mstaafu, Ali Hassan Mwinyi, habari zinasema kwamba Rais Jakaya Kikwete anajipanga kuingia katika uchaguzi wa mwakani bila ya mtandao 'uliomsaidia' mwaka 2005 kwa vile amegundua unaweza kumponza.

Hiyo inafuatia mtafaruku ndani ya CCM unaoelezwa unachochewa zaidi na Katibu Mkuu wake, Yusuf Makamba kwa upande mmoja, mivutano ya makundi ndani ya mtandao wa 2005 na mfumo wa Rais wa kuchelea kuwaudhi baadhi ya watu, Raia Mwema imeambiwa.

Ingawa kila mara CCM kimedai kwamba hakina makundi, hali halisi inaonyesha kwamba chama hicho kimegawanyika katika makundi zaidi ya matatu, likiwamo kundi linaloongozwa na Rais Kikwete mwenyewe, na mengine yakiwa na wafuasi mchanganyiko.

Kwa mujibu wa habari hizo, sasa Rais Kikwete anachelea kushirikiana na mtandao wa mwaka 2005 lakini pia hataki kulibana sana kundi hilo ambalo kimsingi lilidandia katika mgongo wa umaarufu wake likiweka mazingira ya kuwa ndilo lililomwingiza madarakani, lililojumuisha wanasiasa kama Edward Lowassa, Samuel Sitta, Rostam Aziz, Bernard Membe na Makamba.

Kundi hilo sasa si la watu wamoja tena, miongoni mwao baadhi wamekuwa mahasimu wakubwa na baadhi wamefikia hatua hata ya kufikiria kumpinga Rais Kikwete katika Uchaguzi Mkuu wa mwakani, hata kama hadharani hawathibitishi hivyo.

Mbali ya kundi hilo maarufu la mtandao kumeguka na kuwapo mitandao mipya, kundi la wazee wastaafu nalo limeanza kujitokeza kuikosoa Serikali na CCM baada ya kuelezwa kwamba limekwama kutoa mchango wake katika mustakabali wa Taifa kupitia njia za vikao na ushauri.

Taarifa zilizothibitishwa na baadhi ya watendaji wa karibu na Rais zinaeleza kuwa, hakuna uwezekano wowote kwa Rais Kikwete kubwaga manyanga katika Uchaguzi Mkuu mwakani na ameanza harakati za kujihakikishia kurejea Ikulu, akikwepa rekodi ya kuwa Rais aliyekaa madarakani muda mfupi kuliko masharti ya Katiba.

Katiba inatamka Rais kukaa madarakani kwa miaka 10, lakini akiwa amechaguliwa kwa kura kila baada ya miaka mitano. Ni Mwalimu Julius Nyerere pekee aliyekaa madarakani kwa miaka zaidi ya 20 na baadaye kung’atuka kwa hiari yake.

Taarifa za kiintelijensia zinaeleza kwamba tayari Kikwete amekwisha kuanza kufanya mikakati ya chini kwa chini ikiwa ni pamoja na kuandaa makundi ya vijana ambao wameanza kuahidiwa nafasi kadhaa za kisiasa na kiutendaji baada ya Uchaguzi Mkuu wa 2010 kama njia ya kuwafanya wawe watiifu kwake.

Hata hivyo, habari hizo zinaelezwa kupokewa kwa hisia tofauti na baadhi ya wanachama wa CCM, huku baadhi ya vigogo wakibaini uwezekano mdogo wa Kikwete kung’oka si kutokana na kumudu kazi zake barabara bali kutokana na nguvu za madaraka, akiwa Rais na wakati huo huo, Mwenyekiti wa CCM.

“Tunadhani anayo nafasi ya kurudi na hata kama atajitokeza mtu kumpinga, kikubwa ni kwamba watagawana kura za wanachama wa CCM, hawezi kuzipata zote. Hali inaweza kuwa ngumu kama atatokea mtu mwenye maono mapya, akaweza kuwaeleza wana-CCM kwa nini anataka kumpinga Rais,” alieleza mmoja wa viongozi waandamizi serikalini kwa sasa na mwanachama wa muda mrefu wa CCM.

Kiongozi huyo ambaye hakutaka kutajwa jina lake gazetini, anaamini kuwa ripoti ya Kamati ya Mzee Mwinyi ndiyo inayoweza kumjenga Rais Kikwete au kumuharibia mbele ya wana-CCM wenye ushawishi mkubwa katika chama hicho na zaidi itategemea na jinsi uongozi wa juu utakavyoingilia kati maandalizi ya ripoti hiyo kabla ya kutolewa kwake hadharani.

“Kama itaonekana hakuna tija yoyote kutokana na kamati ya Mwinyi na bado, Rais kwa nafasi yake ya Mwenyekiti wa CCM akaonekana kutoeleweka anachokifanya katika kuongoza chama kama taasisi imara kwenye Uchaguzi Mkuu mwakani, nafasi yake itazidi kuwa finyu,” alisema lakini alipoulizwa na gazeti hili ni kwa nini amzungumzie Kikwete pekee wakati chama kinaongozwa kwa uamuzi wa vikao vya Kamati Kuu na Halmashauri Kuu, alijibu;

“Unajua pamoja na chama kutoa uamuzi wa baadhi ya masuala kupitia vikao vyake bado, Mwenyekiti anayo nafasi kubwa ya kushawishi mwelekeo wa chama. Kwa mfano, tumewahi kutoa matamko ya makundi kufutwa katika chama lakini yamekuwapo kwa muda mrefu, je, Mwenyekiti anaonyesha interest gani? Vitendo vya viongozi wenzake kwenye chama hasa sekretariati wanatenda kwa mtazamo huo au nao wanachochea makundi?

“Kwa hiyo katika utekelezaji wa tamko kama hilo, Mwenyekiti anapimwa kwa kutazama ametumia vipi influence yake kulifanikisha. Inapobainika Mwenyekiti amebaki kimya na wanachama wengi wanaamini influence yake vema maana yake amekwama. Mwenyekiti anapimwa namna anavyojikita kwa dhati katika kuonyesha njia.”

Kigogo huyo ambaye kwa sasa ni miongoni mwa watendaji waandamizi lakini wenye msimamo wa kuenzi Tanzania yenye maadili ya uongozi aliyoiacha Baba wa Taifa, Mwalimu Nyerere alikiri kuwapo kwa udhaifu kwa ujumla katika medani ya uongozi nchini na kwamba makundi yameendelea kukuzwa na viongozi wa sasa zaidi.

Wakati hayo yakijitokeza, kumekuwapo na taarifa kutoka kwa baadhi ya wajumbe wa NEC-CCM kujiandaa kulalamika wazi wazi ndani ya chombo hicho kuhusu mwenendo wa uongozi wa chama chao, ambao wanaamini ni wa kugawa wanachama zaidi kuliko kuwaunganisha, hatua ambayo huenda ikazidisha mpasuko kutokana na staili iliyojitokeza ya viongozi kutopenda kukosolewa.

Inaelezwa kuwa kati ya wanaotarajiwa kuzungumza ni pamoja na watu wenye rekodi makini ya utendaji nchini na ambao kwa kiasi fulani wamekwishaathirika na kauli za viongozi wa sasa wa CCM walioko madarakani.

Miezi michache iliyopita picha halisi ya kugawanyika kwa CCM ilijitokeza mjini Dodoma wakati kamati ya Mwinyi inayowashirikisha Pius Msekwa na Abdulrahaman Kinana, ilipowasilikiza wabunge wa CCM.

Wabunge hao walionyesha kuwapo katika kambi mbili kubwa moja ikitaka kurejeshwa kwa misingi ya kuanzishwa kwa CCM, ikiwa ni pamoja na kuwaengua uongozi wanachama wake watuhumiwa wa vitendo vya rushwa, hususan wale ambao wamekwishajiuzulu serikalini.

Kundi jingine ni lile lilijitokeza kutetea watuhumiwa wa ufisadi kwa madai kuwa hawajafikishwa mahakamani, bila kujali kuwa hata serikalini wamejiuzulu uongozi bila kufikishwa mahakamani.

Hata hivyo, karata ya mwisho sasa inabaki mikononi mwa Kikwete ambaye anakifahamu chama vyema kwa kuwa sehemu kubwa ya maisha yake ameitumia humo tena akiwa katika uongozi ngazi za chini.

Wachunguzi wa mambo wanaeleza kwamba dalili za wazi za kumeguka kwa CCM zimezidi kujitokeza kutokana na uongozi wa juu wa chama hicho kuashiria kuimarisha makundi badala ya kuyavunja.

Kauli ya hivi karibuni ya Makamba na baadaye Kikwete kuhusiana na matamko yaliyotolewa kwenye kongamano la Mwalimu Julius Nyerere, ni moja ya ishara mbaya kwa CCM kuelekea 2010, kutokana na viongozi hao kuonyesha wazi kuwa wanalo kundi wanalolisimamia.

Kauli ya Makamba kubeza na hata kuwakashifu viongozi wastaafu na watu mbalimbali waliotoa kauli za kuikosoa CCM na serikali yake, ilichochewa na kauli ya Kikwete kwamba kuna watu wenye chuki binafsi na kwamba anajiandaa kujibu mapigo, kauli ambazo zimeelezwa kwamba hazikustahili kutolewa na viongozi wa ngazi yao.

Kikwete alikwenda mbali zaidi kwa kutoa takwimu zilizoonyesha kuwakejeli zaidi ya nusu ya wapiga kura kwa kusema kuonyesha kwamba “asilimia 70 ya Watanzania hufuata upepo” huku akisema asilimia 15 ni watu wanaompinga akibakiwa na asilimia 15 tu ya wanaomuunga mkono kwa dhati.

Tathmini hiyo ya Kikwete imezidi kuwachanganya watu baadhi wakisema kwamba imedhihirisha kwamba inawezekana ameanza kuingiwa na wasiwasi badala ya kujifunza na kuchukua hatua kwa kuzingatia maoni na ukosoaji unaotolewa.

Wasomi wa kada mbalimbali wamekwisha kuwahi kutoa maoni yao kwamba hali tete ya uongozi nchini na hasa katika CCM, imechangiwa na Rais Kikwete kutokuyapatia ufumbuzi masuala nyeti ya kitaifa na chama chake kwa wakati.

Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Dk Ezavel Lwaitama, amewahi kukaririwa na gazeti moja nchini akisema, hatma ya malumbano au mpasuko unaoendelea kujitokeza ndani ya CCM utategemeana Rais ataegemea katika kundi lipi kati ya mawili yaliyopo hivi sasa ndani ya chama hicho.

Makundi hayo mawili ambayo yamekwishaigawa hata serikali, likiwamo Baraza la Mawaziri ni kati ya linalojinadi kupinga ufisadi na jingine likiwa upande wa utetezi likiundwa na majeruhi wa ufisadi.

Kundi linalopinga ufisadi linaundwa na Sitta na wabunge kadhaa, kama Dk. Harrison Mwakyembe, Anne Kilango-Malecela, Christopher ole Sendeka, Fred Mpendazoe, Stella Manyanya, Saidi Mkumba na wengine ambao wamekuwa wakiunga mkono chini kwa chini.

Kundi hili limekuwa na nguvu kubwa mno bungeni kiasi cha kulijengea picha nzuri mbele ya umma, lakini likionekana kuzidiwa nguvu ndani ya CCM, ambako kundi pinzani limejikita, likiongozwa na wabunge, Rostam Aziz na Lowassa, ambao ni wajumbe wa NEC.

Nguvu za kundi hili la Rostam na Lowassa limejiimarisha kuanzia katika sekretariati ya chama hicho, linakoungwa mkono dhahiri na Makamba kama ilivyojitokeza wakati wa mgogoro wa mkataba wa ujenzi wa jengo la eneo la Makao Makuu ya Umoja wa Vijana wa CCM, Dar es Salaam.

Katika sakata hilo, Makamba alitetea wahusika waliotuhumiwa na kada Nape Nnauye ambaye ni mjumbe wa NEC lakini ambaye anatajwa yu katika kundi la Sitta, ambalo pia linahusishwa na vigogo wengine wa CCM, akiwamo John Malecela.

Wengine wanaotajwa kuwamo kwenye kundi la Rostam na Lowassa ni Mwenyekiti wa Umoja wa Wanawake-CCM (UWT), Sophia Simba, Andrew Chenge, ambaye ni mjumbe katika kamati ya maadili ya CCM na Mbunge wa Kigoma Mjini, Peter Serukamba.

Kuhusu makundi hayo, kwenye maoni yake hayo, Dk. Lwaitama aliweka bayana kuwa kwa sasa CCM inakabiliwa na tatizo kubwa la uadilifu kwa viongozi wake, hali aliyoitaja kuwa ndiyo chanzo cha kuibuka makundi hayo mawili.

“Mustakabali wa Taifa pamoja na urais wa Kikwete katika uchaguzi ujao wa mwaka 2010 utategemeana atajiunga na kundi gani kati ya haya mawili,” alikaririwa akisema Dk Lwaitama na kuongeza; “Haya yote yanayotokea kwa sababu ya kutokuwapo kwa maadili ya uadilifu ndani ya viongozi wetu na hasa wa CCM.

“Haya mambo yanaweza kwisha tu endapo Rais Kikwete atakuwa na ujasiri wa kupigania kurudi kwa misingi ya chama cha TANU ambayo ilikataza kabisa rushwa kuwa ni adui wa haki na kutekeleza kauli hiyo kwa vitendo.”

Source:www.raiamwema.co.tz

No comments: